Upload
others
View
16
Download
0
Embed Size (px)
Citation preview
1
HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. JAKAYA MRISHO KIKWETE,
RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE
SHEREHE YA KILELE CHA MBIO ZA MWENGE WA UHURU,
KUMBUKUMBU YA BABA WA TAIFA MWALIMU JULIUS
KAMBARAGE NYERERE NA WIKI YA VIJANA KITAIFA
TAREHE 14/10/2013 MKOANI IRINGA
Mheshimiwa Anne Makinda, Spika wa Bunge;
Mheshimiwa Dkt. Fenella Mukangara, Waziri wa Habari,
Vijana, Utamaduni na Michezo;
Mheshimiwa Zainab Mohamed, Waziri wa Uwezeshaji, Ustawi
wa Jamii, Vijana, Wanawake na watoto - Zanzibar;
Waheshimiwa Mawaziri na Nanaibu Mawaziri;
Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, Mkuu wa Mkoa wa
Iringa;
Waheshimiwa Wabunge na Wajumbe wa Baraza la
Wawakilishi;
Makamu Mwenyekiti wa CCM (wa Mkoa) na Viongozi wa
Vyama vya Siasa mliopo;Waheshimiwa Mabalozi na
Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa, Viongozi wa Serikali
wa Ngazi mbalimbali za Taifa na Mkoa;
Wageni Waalikwa;
Ndugu Wananchi;
2
Mabibi na Mabwana;
Shukrani
Niruhusuni nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu,
mwingi wa rehema, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha
kukutana tena mwaka huu kuadhimisha Kilele cha Mbio za
Mwenge wa Uhuru, kumbukumbu ya Baba wa Taifa hayati
Mwalimu Julius Nyerere na Wiki ya Vijana. Namshukuru sana
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, na viongozi wenzake pamoja na
wananchi wa Iringa kwa kutupokea vizuri na ukarimu wenu. Pia
nawapongeza kwa kukubali kuwa wenyeji wa maadhimisho
haya. Kazi ya kuandaa sherehe kubwa kama hizi siyo jambo
jepesi hata kidogo. Bahati nzuri mambo yamefana sana kama
tunavyoshuhudia sote. Hongereni sana.
Pongezi Wizara
Ndugu wananchi;
Niruhusuni pia nitoe pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Dkt.
Fenella Mukangara, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na
3
Michezo na Mheshimiwa Zainab Omary, Waziri wa Uwezeshaji,
Ustawi wa Jamii, Vijana, Wanawake na Watoto wa Zanzibar
kwa uongozi wao makini wa shughuli za Mbio za Mwenge.
Kama tujuavyo shughuli za Mbio za Mwenge husimamiwa na
Wizara zetu hizi mbili. Tunawapongeza kwa kazi nzuri
waifanyayo. Ni ukweli ulio wazi kuwa kila mwaka tunashuhudia
mambo yakiwa bora zaidi kuliko mwaka uliopita. Mcheza kwao
hutunzwa. Hongereni sana.
Pamoja na Mawaziri napenda kuwatambua viongozi na
wafanyakazi wote wa Wizara zetu mbili waliohusika na Mbio za
Mwenge kwa kazi yao nzuri tunayojivunia sote. Aidha,
nawapongeza Wakuu wa Mikoa na Wilaya, viongozi na
watumishi wa Serikali zetu mbili na wajumbe wote wa kamati
mbalimbali walioshiriki katika kuratibu Mbio za Mwenge wa
Uhuru mwaka huu. Wamefanya kazi nzuri inayostahili
kupongezwa na kila mmoja wetu.
4
Kwa namna ya pekee nawapongeza ndugu Juma Ali Sumai,
kiongozi wa Mbio za Mwenge na Wakimbiza Mwenge wenzake
kwa kutimiza kwa ufanisi wa hali ya juu jukumu kubwa na zito
la kukimbiza Mwenge wa Uhuru nchi nzima. Nawapa pole
nyingi kwa changamoto mbalimbali walizokumbana nazo katika
safari ya kilomita nyingi. Kazi hiyo wameimaliza salama na leo
wameukabidhi Mwenge ukiwa salama. Nawapongeza sana kwa
kuufikisha ujumbe wa Mwenge kwa uhodari mkubwa.
Waheshimiwa Mawaziri;
Ndugu wananchi;
Nafurahi kusikia kuwa kama ilivyokuwa miaka iliyopita,
mwaka huu watu walijitokeza kwa wingi kila mahali Mwenge
wa Uhuru ulipopita. Pia nimeambiwa ujumbe wa Mwenge
ulifikishwa kwa ufasaha na kwamba umepokelewa vizuri. Miradi
mingi ya maendeleo imezinduliwa na kuwekewa mawe ya
msingi.
5
Napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza kwa dhati
kabisa wananchi wa Tanzania kwa ushiriki wao mzuri katika
Mbio za Mwenge. Ushiriki wao ni kielelezo tosha cha kutambua
umuhimu wa Mwenge wa Uhuru na cha moyo wa uzalendo kwa
nchi yetu na kuwaenzi waasisi wa taifa letu. Kwa niaba ya
Serikali nawahakikishia kuwa tutaendelea kuwahimiza viongozi
wa ngazi mbalimbali kuhakikisha kuwa miradi yote
iliyozinduliwa na kuwekewa mawe ya msingi wakati wa mbio za
Mwenge wa Uhuru inaendelea kutekelezwa kama
ilivyokusudiwa.
Kwa namna ya pekee nawapongeza waandishi na vyombo
vya habari kwa kuwa nasi bega kwa bega kuhamasisha watu na
kueneza ujumbe wa Mwenge. Mchango wao umesaidia sana
kufanikisha malengo ya Mbio za Mwenge kwani siku zote
wapotoshaji hawakosekani.
6
Kumbukumbu ya Baba wa Taifa
Ndugu Wananchi;
Kama mjuavyo siku ya kilele cha Mbio za Mwenge pia ni
siku ya kuadhimisha kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa
letu la Tanzania kilichotokea miaka 14 iliyopita. Ni siku ambayo
tunawajibika kukumbuka mema mengi aliyoifanyia nchi yetu,
mafundisho yake na urithi aliotuachia. Nia yetu ni kutaka watu
wasimsahau kiongozi wetu huyu maalum na muhimu sana
katika historia ya nchi yetu.
Miongoni mwa mambo ya kukumbuka hasa wakati huu wa
Mchakato wa Katiba Mpya ni (jambo la busara kutumia muda
wetu) kujikumbusha mawazo ya Mwalimu kuhusu umoja wa
nchi yetu pamoja na Muungano wa Zanzibar na Tanganyika.
Hotuba zake na maandishi yake kuhusu mambo hayo yana
mafundisho mengi mazuri ambayo tukiyaelewa vyema na
kuyazingatia yatatusaidia sana katika mjadala na ukamilishaji wa
mchakato wa Katiba mpya.
7
Mimi naamini fikra za Mwalimu na mtazamo wake kuhusu
umoja wetu na Muungano bado vina maana hata leo. Tujiepushe
na kuyapuuza tusije tukawa na Katiba itakayolibomoa taifa
badala ya kulijenga. Ninaposema hivyo sipendi nieleweke kuwa
sitaki mabadiliko ila napenda tuwe makini katika kufanya
mabadiliko. Nataka tufanye mabadiliko yatakayotupeleka mbele
na siyo kuturudisha nyuma.
Ndugu wananchi;
Pamoja na kuadhimisha siku ya kifo cha Baba wa Taifa
(Mwalimu Julius Nyerere), nadhani ni vyema pia tukawa
tunaikumbuka siku ya kuzaliwa kwake yaani tarehe 13 Aprili
(1922). Nisingependa kujiingiza katika mjadala wa siku ipi bora
zaidi kwani zote ni siku muhimu katika historia ya maisha ya
mwanadamu. Tofauti yake ni kuwa siku ya kuzaliwa ni ya furaha
na siku ya kufa ni ya majonzi. Kama tutakubaliana tuikumbuke
na siku yake ya kuzaliwa pengine siku hiyo tungeiita Nyerere
Day. Tuiadhimishe siku hiyo kusheherekea maisha yake kwa
8
kujadili kazi zake na kufanya shughuli mbalimbali kuenzi
mambo mema aliyosimamia na kuifanyia nchi yetu na dunia kwa
ujumla.
Kauli Mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru 2013
Ndugu Wananchi;
Kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri kila mwaka Mbio za
Mwenge wa Uhuru huwa na ujumbe maalum unaobebwa na
kauli mbiu ya mwaka huo. Mwaka huu ujumbe ulikuwa
“Watanzania ni Wamoja: Tusigawanywe kwa Msingi wa
Tofauti Zetu za Dini, Itikadi, Rangi na Rasilimali”. Ujumbe
huu ni muafaka kabisa hasa ukikumbuka misukosuko na
majaribu makubwa nchi yetu iliyopitia mwaka huu. Hivyo
kutumia Mbio za Mwenge wa Uhuru kukumbushana haja na hoja
za kuziba nyufa zilizoanza kujitokeza ni jambo la busara sana. Ni
jambo la kuungwa mkono na kila mwananchi na hasa kila
mzalendo.
9
Bahati nzuri upepo huo mbaya umepita na tuombe usirudi
tena. Hivi sasa hali ni shwari na Watanzania tunaendelea
kushirikiana vizuri bila ya kubaguana kwa dini zetu, vyama vya
siasa na kadhalika kama tulivyozoea kuishi miaka yote.
Waliotaka kutufarakanisha hawakufanikiwa lakini, lazima tuwe
makini kwani wanaweza kujaribu tena kutugawa ama kwa yale
yale au mambo mengine.
Ndugu wananchi;
Kwa kweli nafarijika sana kuona Watanzania wakiendelea
kukataa ushawishi na uchochezi wa kugawanywa kwa misingi ya
dini au mambo mengine. Ndugu zangu naomba tuendelee hivyo
na hayo ndiyo mafundisho mema na urithi aliotuachia Baba wa
Taifa tunayemkumbuka leo. Tukigawanyika, nchi yetu
itavurugika na sote tutakuwa tumeharibikiwa. Dhambi kubwa ya
kubaguana kwa misingi yo yote ile ni kupotea kwa amani na
utulivu. Bila amani, hatuwezi kuishi kwa furaha katika nchi yetu
hii nzuri. Bila amani, jamii haiwezi kujishughulisha kwa
10
ukamilifu na shughuli za kujiletea maendeleo. Amani
ikituponyoka nchi yetu itayumba na hakuna atakayebaki salama.
Napenda kuwahakikishia wananchi wenzangu wote, kuwa
sisi Serikalini tutaendelea kufanya kila tuwezavyo kujenga,
kulinda na kudumisha umoja na mshikamano wetu ambao ndio
msingi mkuu wa kuwepo kwa amani na utulivu nchini.
Tutaendelea kukemea kwa nguvu zetu na uwezo wetu wote
vitendo vinavyosababisha mmomonyoko wa umoja na
mshikamano wetu. Serikali haitasita kuchukua hatua za kisheria
dhidi ya mtu au kikundi cha watu watakaojihusisha na vitendo
vya kuvuruga amani ya nchi yetu. Naomba Watanzania
wenzangu mtuelewe hivyo. Napenda kusisitiza na kuwasihi
kuwa tuendelee kuaminiana, kuheshimiana na kuvumiliana
pamoja na tofauti zetu.
11
Mapambano Dhidi ya UKIMWI
Ndugu wananchi;
Pamoja na ujumbe huu maridhawa ambao kimsingi ndiyo
ujumbe mkuu wa Mbio za Mwenge tangu kuasisiwa kwake,
mwaka huu wananchi waliendelea kuhimizwa kuendeleza
mapambano dhidi ya ugonjwa wa UKIMWI, rushwa na dawa za
kulevya. Tangu ugonjwa wa UKIMWI uingie nchini kwetu
mwaka 1983, inakadiriwa kuwa zaidi ya ndugu zetu milioni 2
wamepoteza maisha kutokana na maradhi haya. Hali kadhalika
zaidi ya watoto milioni 1.3 wamekuwa yatima na watu zaidi ya
milioni 1.5 wanaishi na VVU hivi sasa. Bahati mbaya karibu
asilimia 65 ya hao ni wanawake.
Kitaifa, takwimu zinaonesha kuwa maambukizi ya UKIMWI
yanazidi kupungua kutoka asilimia saba mwaka 2005 hadi
asilimia 5.7 mwaka 2010 na kufikia asilimia 5.1 mwaka 2012.
Hapa Iringa napo maambukizi yamekuwa yanapungua ingawaje
bado yapo juu na kwamba ni Mkoa wa pili nchini kuwa na
12
kiwango cha juu cha maambukizi. Takwimu zinaonesha kuwa
kiwango cha maambukizi Mkoa wa Iringa ni asilimia 9.1,
wanaume asilimia 6.9 na wanawake asilimia 10.9. Mkoa wa
Njombe ndiyo unaoongoza ukiwa na asilimia 14.8.
Kwa sababu ya maradhi haya idadi ya watoto yatima ni
kubwa katika mkoa huu (inakadiriwa kuwa waliopo ni 3400).
Inahuzunisha sana kusikia au kuona baadhi ya watoto hawa
wamelazimika kukatisha masomo yao baada ya wazazi wao
kufariki ili kuwalea wadogo zao. Kwa ajili hiyo, wamelazimika
kufanya kazi zisizostahili kufanywa na watu wa umri wao.
Wapo pia wazee ambao kwa umri wao wanahitaji kulelewa lakini
wamebaki peke yao na wakati mwingine wanalazimika kulea
watoto walioachwa na watoto wao.
Ndugu wananchi;
Nilishaagiza viongozi siku za nyuma na leo narudia tena
kuwa, tuwatambue watoto yatima kisha tutengeneze mipango
thabiti ya kuwasaidia. Lengo letu hapa ni kutaka tuwawezesha
13
kupata fursa ya kukua na kuishi kama watoto wengine. Jambo
moja muhimu nililolisisitiza ni kuwa tuhakikishe kuwa vijana
hawa wanapata elimu ambayo ndiyo ufunguo wa maisha yao.
Ndugu wananchi;
Tuongeze ari, nguvu na kasi ya kupambana na gonjwa hili
hatari. Ni kweli tunapata mafanikio lakini hayatoshi. Kiwango
bado ni cha juu mno. Nawaomba viongozi wa Serikali, dini, asasi
za kijamii, wanasiasa na wananchi tuendelee kuhamasisha jamii
kujiepusha na ugonjwa huu. Tuwahimize watu wajitokeze
kupima wajue mustakabali wao, waepuke ngono nzembe na hasa
hasa wawe na subira na waaminifu kwa ndoa zao au wapenzi
wao. Sisi katika Serikali tutaendelea kutimiza wajibu wetu wa
kuelimisha na kuhakikisha kuwa dawa za kufubaza vijijidudu
vya UKIMWI zinapatikana bure kwa waathirika waliofikia hatua
ya kutumia dawa hizo.
14
Natoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Iringa kuongeza
juhudi maradufu kutokana na ukweli kwamba kiwango cha
maambukizi kiko juu mno. Watu waendelee kujitokeza kwa
wingi kupima kwa hiari ili kujua afya zao. Katika zoezi la
kupima kwa hiari hapa Iringa, watu 388,071 wamejitokeza
kupima. Jambo hili ni jema sana. Napenda pia kuchukua fursa
hii kuwasihi akina mama wajawazito wawe mstari wa mbele
kupima VVU ili wale walioathirika waitumie ipasavyo huduma
ya kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa
mtoto. Huduma hii inamfanya mtoto anayezaliwa na mama
aliyeathirika kuwa salama. Huduma hii ipo kote nchini na
inatolewa katika hospitali zote za Serikali.
Ndugu wananchi;
Ombi langu maalum kwa wanaume, kote nchini ambao
bado hawajafanyiwa tohara wajitokeze kwa wingi kufanya hivyo.
Madaktari wanasema kuwa mwanaume aliyefanyiwa tohara
anapunguza kwa kiasi kikubwa hatari ya kuambukizwa VVU
15
wakati wa kujamiiana. Naomba ieleweke kuwa sisemi mtu
akifanyiwa tohara hapati UKIMWI. La hasha. Ninachosema ni
kwamba ukimlinganisha na yule ambaye hakufanya hivyo,
uwezekano wa kuambukizwa unapungua. Wanasema asiye na
tohara ana uwezekano mkubwa zaidi wa kupata michubuko
ambayo hurahisisha virusi kuingia kwenye mwili wake. Narudia
kusisitiza mtu akipata tohara asidhani yuko salama kabisa. Watu
wote lazima wachukue tahadhari stahiki.
Ndugu wananchi;
Ombi langu la pili ni kwa watu wanaotumia dawa za
kufubaza virusi vya UKIMWI wasiache kuzitumia. Wakiacha
kwa sababu yo yote ile wanavipa vijidudu nafasi kujiimarisha na
hivyo kuhatarisha maisha yao. Ombi langu la tatu ni kwa jamii
kuendelea kuwasaidia na kuwahudumia wenzetu ambao
wameathirika badala ya kuwanyanyapaa na kuwatenga. Na,
muhimu zaidi tuwasaidie watoto yatima na wazee ambao
wameachwa bila msaada wowote.
16
Nawataka viongozi wote katika ngazi mbalimbali washiriki
kwa ukamilifu katika mapambano dhidi ya maradhi ya UKIMWI.
Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Afya na TACAIDS waendelee
kuongoza mapambano hayo bila kuchoka. Mimi bado naamini
Tanzania bila UKIMWI inawezekana iwapo tutazingatia masharti
ya kuepuka ugonjwa huu na kuwahudumia ipasavyo
walioathirika. Ushindi hauko mbali sana.
Mapambano dhidi ya Rushwa
Ndugu wananchi;
Mwaka huu, katika Mbio za Mwenge wa Uhuru wananchi
waliendelea kukumbushwa wajibu wao katika kupambana na
rushwa, kwa kauli mbiu isemayo “chukua hatua dhidi ya
rushwa sasa”. Ujumbe huu unakwenda sambamba na juhudi za
serikali za kupambana na rushwa nchini. Tunafahamu kuwa
rushwa ni adui wa haki na kikwazo kikubwa cha maendeleo ya
jamii na taifa. Nchi ikiwa imegubikwa na vitendo vya rushwa
itakosa maendeleo stahiki na watu watadhulumiwa haki zao.
17
Hizo ndizo sababu kuu zilizoifanya serikali yetu ichukie
rushwa na kuchukua hatua za kupambana na uovu huu, tangu
nchi yetu ilipopata uhuru mpaka sasa. Kazi hiyo ngumu na yenye
changamoto nyingi inaongozwa na Taasisi ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa (TAKUKURU). Serikali imechukua na
itaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha chombo
hiki ili kiweze kutimiza majukumu yake kwa ufanisi zaidi.
Matokeo yake TAKUKURU sasa ina mtandao mpana zaidi. Ina
ofisi kila Mkoa na kila Wilaya, watumishi wameongezeka na
vitendea kazi pia.
Nafurahi kuona kuwa mafanikio ya kutia moyo yanaendelea
kupatikana ingawaje kazi iliyo mbele yetu bado ni kubwa. Sote
tunasoma na kusikia kupitia vyombo vya habari taarifa za
watumishi wa serikali, taasisi za umma pamoja na watu wengine
wanavyokamatwa na TAKUKURU kwa kujihusisha na vitendo
vya rushwa. Tangu mwaka 2006, kesi 63 zinazohusu rushwa
kubwa zimefikishwa Mahakamani. Baadhi zimeisha na
wahusika waliopatikana na hatia wameadhibiwa kwa mujibu wa
18
sheria. Zipo pia tulizoshindwa, ni sawa katika nchi inayoheshimu
utawala wa sheria. Nyingine zinaendelea. Vile vile juhudi za
TAKUKURU zimeokoa fedha nyingi za umma. Kwa mfano, kwa
kipindi cha miaka mitatu, yaani kati ya 2010 hadi 2013, zaidi ya
shilingi bilioni 28 zimeokolewa ambazo zingeweza kunufaisha
watu wachache wanaoendeleza vitendo vya rushwa badala ya
taifa.
Naomba wananchi waendelee kutoa taarifa zitakazosaidia
kuwatambua na kuwakamata watoaji na wapokeaji rushwa.
Tukumbuke kuwa mafanikio katika mapambano haya
hayategemei Serikali au TAKUKURU peke yake. Ni mapambano
ambayo jamii ikijihusisha kwa ukamilifu ushindi mkubwa
utapatikana. Yanatuhusu sote kwani tukishinda, matunda yake
yatawafaidisha watu wote. Pia, napenda kutumia nafasi hii
kutoa wito kwa taasisi na idara zote za serikali zinazohusika moja
kwa moja katika vita dhidi ya rushwa zitimize ipasavyo wajibu
wake. Aidha pakiwepo na ushirikiano mzuri na mshikamano wa
dhati miongoni mwetu kwa hakika ushindi utapatikana.
19
Tukifanya hivyo nina imani tutapata mafanikio makubwa zaidi
tena kwa haraka.
Dawa za Kulevya
Ndugu Wananchi;
Tatizo la biashara na matumzi ya dawa za kulevya
limeendelea kuwa moja ya changamoto kubwa zinazolikabili
taifa letu. Serikali imeendelea kufanya jitihada kubwa
kupambana na changamoto hiyo. Yapo mafanikio
yanayopatikana lakini bado tuna kazi kubwa ya kufanya mbele
yetu. Ukubwa wa kazi hiyo unaletwa na ule ukweli kwamba
watu wanaohusika ni wengi na wanazidi kuongezeka kila
kukicha kwa tamaa ya kupata utajiri wa haraka. Isitoshe wakati
wote washiriki wake wanabuni mbinu mpya za kusafirisha,
kusambaza na kuuza dawa hizo haramu. Pia ni kazi hatari kwani
wapambanaji kupoteza maisha si jambo la ajabu.
Pamoja na changamoto hizo, kwa vile matumizi ya dawa za
kulevya yana athari mbaya kwa watu wanaotumia na jamii kwa
20
ujumla, Serikali haitachoka kufanya kila tuwezalo kupambana na
uhalifu huu mpaka ushindi upatikane. Wakibadili mbinu na sisi
tutabadili maarifa ya uchunguzi na utambuzi mpaka tuwapate.
Tutawahami ipasavyo watu wanaojitolea muhanga kupambana
na uovu huu. Mafanikio yanaendelea kupatikana. Kwa mfano,
kuanzia Januari hadi Septemba, mwaka huu (2013) watu 2000
(wafanya biashara na watumiaji wa dawa za kulevya)
wamekamatwa na aina mbalimbali ya dawa za kulevya ikiwa ni
pamoja na kilo 681 za dawa hatari ya heroine, zimekamatwa.
Watu hao kama wasingekamatwa wangeendelea kuuza na
kusambaza dawa za kulevya na kuathiri maelfu ya watu na hasa
vijana ambao ni nguvu kazi muhimu ya taifa letu na warithi wa
jamii na taifa wa kesho. Inatia uchungu sana kuona kuwa
tegemeo letu hilo linaangamizwa na watu wachache wenye
uroho usio na kifani wa kujipatia utajiri wa haraka, tena kwa
gharama yoyote ile.
21
Ndugu wananchi;
Kwa niaba yenu, napenda kutumia nafasi hii kutoa pongezi
zangu za dhati kwa viongozi na wafanyakazi wote wa Tume ya
Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya na vyombo vingine
vya dola kwa kazi kubwa na nzuri inayoendelea kufanyika ya
kukabiliana na tatizo hili. Katika mapambano yetu
tunashirikiana na nchi na taasisi za nchi mbalimbali duniani.
Hivyo basi nazipongeza kwa dhati nchi na taasisi hizo rafiki kwa
ushirikiano wao ambao umetusaidia kupata mafanikio haya kiasi
tunayojivunia leo. Naomba ushirikiano huu uendelee kwani
umetusaidia kwa namna nyingi na umekuwa wa manufaa
makubwa.
Ndugu wananchi;
Nilishawahi kusema siku za nyuma kuwa ni makusudio
yangu na ya serikali kuanzisha chombo chenye uwezo na nguvu
kubwa zaidi ya kupambana na tatizo la dawa za kulevya nchini.
Mchakato wa kuunda chombo hicho umeanza na unaendelea
22
vizuri. Hivi sasa tunayo Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za
Kulevya. Chombo hicho kipya kitakuwa na nguvu kubwa zaidi
kuliko Tume na hata kuliko kikosi kazi cha vyombo vyote vya
dola nilichokiunda kuipa Tume meno.
Ndugu wananchi;
Ili juhudi hizo zifanikiwe na ushindi upatikane itategemea
sana msaada, ushirikiano na ushiriki wa wananchi. Nawaomba
sana ndugu zangu wananchi wenzangu mshirikiane na vyombo
vya dola katika kupambana na usafirishaji, uuzaji na usambazaji
wa dawa za kulevya. Baadhi yenu mnawajua watu
wanaojihusisha na biashara hii haramu. Watajeni
washughulikiwe ipasavyo.
Wiki ya Vijana
Ndugu wananchi;
Kama nilivyosema awali leo pia tunaadhimisha wiki ya
vijana. Nimepata fursa ya kutembelea mabanda ya maonesho ya
23
vijana ili kuona shughuli wanazozifanya. Nimefurahi na
kufarijika sana na kile nilichokiona. Vijana wanafanya kazi nzuri
na kwa kweli ni uamuzi wa busara kuwashirikisha katika sherehe
hizi kwani wanapata fursa ya kuonesha kazi wanazozifanya
katika kuboresha maisha yao na kuleta maendeleo ya taifa. Hii
pia ni nafasi nzuri kwa vijana kukutana, kufahamiana na
kubadilishana mawazo, ujuzi na taarifa muhimu zinazohusu
maisha na maendeleo yao. Kwa kuzingatia umuhimu na faida ya
maonesho haya, ni vyema kuangalia uwezekano wa
maadhimisho ya Wiki ya Vijana yakafanyika katika ngazi ya
Mikoa na kuhitimishwa Kitaifa kama tulivyofanya leo.
Ndugu wananchi;
Mimi na wenzangu Serikalini tunatambua na kuthamini
sana nafasi na mchango wa vijana katika kuchochea maendeleo
ya nchi yetu. Ndio maana Serikali inawekeza sana katika elimu
na mafunzo yao. Ndiyo maana pia Serikali imeamua katika
mwaka huu wa fedha kuongeza uwezo wa bajeti ya Wizara ya
24
Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ili iweze kuwahudumia
vijana vizuri zaidi. Tutaendelea kuongeza bajeti hiyo ili Wizara
iweze kuwaongezea vijana mitaji ya biashara kupitia Mfuko wa
Taifa wa Maendeleo ya Vijana.
Nimefurahi kumsikia Mheshimiwa Waziri akiahidi hapa
kwamba baadhi ya vijana walioshiriki katika maonesho
niliyoyaona leo watafikiriwa kupewa mikopo kwa mujibu wa
taratibu zilizowekwa. Nawasihi vijana watakaopata mikopo
kupitia Mfuko huu pamoja na mifuko mingine ya uwezeshaji
wahakikishe wanaitumia vizuri kwa malengo yaliyokusudiwa na
kuirejesha kwa wakati ili wengine nao wapate.
Maendeleo ya Mkoa wa Iringa
Ndugu wananchi;
Jana jioni nilipokea taarifa ya maendeleo ya Mkoa wa Iringa
kutoka kwa Mkuu wa Mkoa, Dokta Christine Ishengoma. Natoa
pongezi nyingi kwa wananchi wa Iringa kwa juhudi zenu na
mafanikio mnayoyapata katika kujiletea maendeleo. Mkoa
25
umeendelea kuwa wa kutegemewa katika kulipatia taifa chakula
hasa mahindi na sasa mwelekeo ni mzuri kwa mazao ya chai,
mpunga, mboga na matunda. Nawaomba muendelee na juhudi
zenu. Ongezeni maarifa na matumizi ya zana za kisasa na
pembejeo za kilimo ili tija iongezeke mpate mavuno mengi zaidi.
Mtatosheleza mahitaji yenu na mtapata ziada kubwa
itakayotumika kwingineko nchini na hata kuuzwa nje ya nchi.
Sisi katika Serikali tutaendelea kuwasaidia kwa upande wa
upatikanaji wa pembejeo, zana za kilimo, masoko, huduma
mbalimbali zikiwemo za ugani, fedha na kadhalika. Mkoa wa
Iringa utanufaika kupitia Mpango wetu wa Matokeo Makubwa
Sasa (Big Result Now) na SAGCOT.
Ndugu wananchi;
Serikali itaendelea kununua mahindi ya wakulima kupitia
Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula. Hata hivyo ni vyema
nikaeleza wazi kuwa Hifadhi ya Taifa ya Chakula haitanunua
mahindi yote yaliyovunwa nchini. Ukomo wetu kwa sasa ni tani
26
250,000 lakini tunaendelea kupanua uwezo wa maghala hadi
kufikia tani 400,000 ifikapo mwaka 2015. Tayari Hifadhi ya Taifa
wameshanunua tani 209,000 hivyo bado tani 41,000. Hivyo
nashauri wenzetu wa sekta binafsi nao wajitokeze kununua
mahindi ya wakulima.
Kwa kuwa hakuna kizuizi cha kuuza nje wanaweza kufanya
hivyo wakipenda. Hata hivyo, sisi tungependa kwanza wauze
hapa nchini. Naomba ieleweke kuwa hatutawauzia watu akiba
yetu ya mahindi katika Hifadhi ya Taifa ya Chakula kwa ajili ya
kuuza nje.
Ndugu wananchi;
Pamoja na kuendeleza kilimo katika Mkoa wa Iringa,
tutaendelea kuboresha barabara, na huduma za umeme, maji,
elimu na afya. Ninyi ni mashahidi kwamba utekelezaji wa ahadi
ya kujenga barabara ya lami kutoka Iringa hadi Dodoma
unakwenda vizuri na ukarabati wa barabara ya Morogoro –
27
Tunduma kupitia Iringa na Mbeya umekamilika. Tunajipanga
kutekeleza ahadi zetu kwa baadhi ya barabara za Mkoa huu.
Kwa upande wa umeme vijijini tunaendelea kuvipatia
umeme vijiji 38 vya Mkoa huu na wakati huo huo tunajiandaa
kuvipatia umeme vijiji vingine 86. Tutaendelea kuongeza
upatikanaji wa maji vijijini na mijini. Aidha, tumeanza kutekeleza
mkakati kabambe wa kuboresha elimu kwa shabaha ya kutoa
fursa ya elimu kwa vijana wetu wengi na kuongeza kiwango cha
ufaulu. Haya yote tunayafanya chini ya mkakati mpya wa
kupata Matokeo Makubwa Sasa. Tutaongeza mara dufu juhudi za
kuboresha huduma ya afya.
Hitimisho
Ndugu wananchi;
Kabla ya kumaliza hotuba yangu niwakumbushe
Watanzania wenzangu kuwa mwaka ujao ni wa aina yake katika
nchi yetu. Kwanza tunasherehekea miaka 50 ya Mapinduzi
Matukufu ya Zanzibar, pili, tunasherehekea miaka 50 ya
28
Muungano. Na tatu, kama mambo yatakwenda sawa tutapata
Katiba Mpya. Niwaombe Watanzania wenzangu tujiandae vyema
kufanikisha mambo yetu hayo matatu ya kihistoria. Naomba
nimalize kwa kuwashukuru tena wananchi na viongozi wa Mkoa
wa Iringa kwa kufanikisha sherehe hii muhimu. Nawashukuru
pia wadau mbalimbali ambao wamechangia kwa hali na mali
kufanya sherehe hizi zifanikiwe na kufana sana kama hivi.
Napenda kutumia nafasi hii pia kuwatakiwa ndugu zetu
Waislamu na Watanzania wenzangu wote heri ya Sikukuu ya Idd
El Hajj.
Baada ya kusema hayo sasa natamka rasmi kwamba
shughuli za Mbio za Mwenge wa Uhuru, kumbukumbu ya Baba
wa taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Wiki ya Vijana
kwa mwaka 2013 zimefikia kilele chake.
Asante sana kwa kunisikiliza.