13
1 Hotuba ya kufunga mwaka ya Mhe: Zitto Kabwe (Mb), wakati wa mkutano wa pamoja wa hadhara na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, mjini Mtwara (31/12/2014). Ndugu Profesa Ibrahimu Lipumba Mwenyekiti wa Taifa wa CUF, Ndugu Viongozi mbalimbali mliopo hapa leo, Ndugu Wananchi Mtwara Hakiii Mtwara kuchele? Mtwara kumekucha? MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, nashukuru sana kwa mwaliko wako kuja kuzungumza na watu wa Mtwara na kujumuika nao katika kufurahia mafanikio makubwa waliyoyapata katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Speech by Zitto Kabwe

Embed Size (px)

DESCRIPTION

31-12-14 in Mtwara.

Citation preview

Page 1: Speech by Zitto Kabwe

1

Hotuba ya kufunga mwaka ya Mhe: Zitto Kabwe (Mb), wakati

wa mkutano wa pamoja wa hadhara na Mwenyekiti wa CUF,

Profesa Ibrahim Lipumba, mjini Mtwara (31/12/2014).

Ndugu Profesa Ibrahimu Lipumba

Mwenyekiti wa Taifa wa CUF,

Ndugu Viongozi mbalimbali mliopo hapa leo,

Ndugu Wananchi

Mtwara Hakiii

Mtwara kuchele? Mtwara kumekucha?

MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba,

nashukuru sana kwa mwaliko wako kuja kuzungumza na watu wa

Mtwara na kujumuika nao katika kufurahia mafanikio makubwa

waliyoyapata katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Page 2: Speech by Zitto Kabwe

2

Nakushukuru kwa kipekee kwa upendo wako kwangu. Umekuwa mlezi

wangu kisiasa na kimaisha. Hata pale nilipopitia mikiki mikiki na

mihemko ya kisiasa, kamwe hukunikatia hukumu, bali uliona namna bora

zaidi ya kunijenga kiuongozi. Wakati baadhi ya watu wakiandikia tanzia

yangu ya kisiasa, uliniita na kufuturu nawe nyumbani kwako ukiwa katika

moja ya sunna zako unazofunga kila wiki. Nakushukuru sana sana, na

ninaomba uendelee kunilea katika maisha yangu ya kisiasa, kifamilia,

kijamii na hata kitaaluma. Ukiwa mbobezi wa kimataifa katika taaluma ya

uchumi nami nafuata nyayo zako, nataka nipite humohumo ulimopita na

inshallah na hata zaidi.

Ndugu wananchi,

Ni kwa sababu ya upendo wa Profesa Lipumba kwangu nilishindwa

kukataa kukubali mwaliko wake kuja hapa kujumuika nanyi katika siku

hii muhimu sana. Hakuna namna bora zaidi ya kushukuru zaidi ya

kuendelea kufanya kazi pamoja katika kuwatetea Watanzania na Tanzania

yetu. Umoja wa upinzani ndio silaha dhidi ya mabwenyenye wa kiuchumi

na kisiasa hapa nchini. Najua huko waliko inawauma sana wanapoona

wapinzani wanaungana bila kujali tofauti ndogondogo zinazojitokeza

miongoni mwao. Tutaendelea kushirikiana kwa maslahi mapana ya nchi

yetu na katika kuhakikisha kwamba utawala wa Chama cha Mapinduzi

ambacho sasa ni chama cha mabwenyenye unakoma katika nchi yetu

mapema iwezekanavyo.

Page 3: Speech by Zitto Kabwe

3

Nimekuja pia Mtwara kwa sababu huu ni Mkoa wa kipekee katika historia

ya nchi yetu. Mtwara ni Mkoa ambao kwa miaka zaidi ya miaka 25 baada

ya nchi yetu kupata uhuru ulibaki kuwa ngome imara dhidi ya mabeberu

wa Kireno na waasi wa nchi jirani ya Msumbiji. Wakati mikoa mingine

ikisonga mbele katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii, Mikoa ya

Mtwara na Lindi ilibaki nyuma kwa sababu ya kulinda heshima ya mipaka

ya nchi yetu. Hii ni historia muhimu sana ambayo vijana wetu inabidi

waijue na waithamini.

Katika miaka ya hivi karibuni Mkoa wa Mtwara umechukua sura mpya

kabisa kitaifa kufuatia kugunduliwa kwa gesi. Na katika hili wananchi wa

Mtwara mmeonyesha kwamba watanzania wanaweza kupigania maslahi

ya Taifa wakiamua. Mmesimama kidete kuhakikisha kwamba utajiri huu

hauporwi na kwamba haturudii makosa yaliyofanyika Kanda ya Ziwa pale

tuliporuhusu madini kuporwa na mabeberu wa kimagharibi kwa msaada

wa mabwenyenye uchwara nchini mwetu. Nyie wananchi wa Mtwara

mmesimama kidete katika kulinda maliasiali hii iliyogunduliwa kwa niaba

ya wananchi wenzenu nchi nzima ya Tanzania.

Najua bado mnalia kuhusu Bomba la kupeleka Gesi Asili Dar es Salaam.

Machozi yenu yatafutika tu kwani tayari habari za ufisadi mkubwa katika

ujenzi wa Bomba hili zimeanza kuchomoza. Kiongozi wa Upinzani

Bungeni ametamka mara kadhaa kuwa atatoa hoja kuhusu ufisadi katika

ujenzi wa Bomba la Gesi. Sisi wengine, pale atakapohitaji msaada wetu,

tutamsaidia kwani tunaamini gharama za mradi huu zimezidishwa mara

mbili na inawezakana kabisa kuwa zaidi ya dola za Marekani 600 milioni

Page 4: Speech by Zitto Kabwe

4

zimegawanywa kwa watu kama rushwa kuanzia Uchina mpaka hapa

Tanzania. Machozi yenu wana Mtwara yatafutwa tu, kwa uwezo wa mola.

Kwa hiyo kwangu mimi Mtwara ni alama ya harakati za kupigania haki za

wananchi kumiliki, kuendesha na kufaidika na mali asili za Taifa.

Tutaendelea kushirikiana nanyi kuhakikisha kwamba utajiri unaoendelea

kugunduliwa hapa Mtwara na Tanzania kwa ujumla unasaidia wananchi

katika kuboresha maisha yao, elimu zao na kumaliza umaskini.

Mimi kama mwana michezo na ambaye napigania maendeleo na

mafanikio ya timu za hapa nyumbani Tanzania, niwapongeze pia wana

Mtwara kwa sababu ya timu yenu ya mpira ya Ndanda FC ambayo imeleta

changamoto sana kwenye maendeleo ya soka nchini kwetu. Napenda

kuitakia kheri timu yenu ya Ndanda FC katika mashindano ya Ligi Kuu ya

Tanzania yanaendelea hivi sasa.

Ndugu Wananchi,

Imekuwa baraka na neema sana kufunga mwaka huu hapa Mtwara, ikiwa

ni alama ya harakati za mapambano dhidi ya mabeberu na vibaraka wao

popote walipo. Mtwara ni uwanja wa mapambano ya uwajibikaji na

demokrasia. Ndio maana nasema imekuwa neema na baraka kufungia

mwaka huu hapa. Kama Mwalimu Nyerere alivyotanagza Azimio la

Arusha mwaka 1967 katika kujenga Nchi ya kijamaa, wana mabadiliko

wote nchini wanapaswa kutangaza Azimio la Mtwara la Uwajibikaji

katika Uvunaji wa Maliasili ya Nchi yetu.

Page 5: Speech by Zitto Kabwe

5

Mwaka huu tunaouaga leo ulianza kwa matumaini makubwa sana kwa

Taifa letu katika kupata Katiba Mpya ilitayozamiwa kuweka misingi imara

zaidi ya Uwajibikaji wa Serikali kwa Wananchi. Bahati mbaya mwaka

umemalizika kwa kubwaga chini mioyo ya Watanzania wengi sana baada

ya kupata Katiba Inayopendekezwa yenye mambo yale yale

yaliyotufikisha hapa tulipo zaidi ya nusu karne tangia tupate Uhuru.

Hatutakubali nchi yetu irudi nyuma katika maendeleo ya demokrasia na

kuruhusu watu wachache wapore uhuru wa wananchi kwa maslahi yao na

vyama vyao vilivyogeuka mapango ya uporaji wa mali asili zetu kupitia

mabeberu wa kimagharibi na vibaraka wao. Hatutakubali katiba mpya

kwa jina. Hatutakubali mvinyo huohuo katika chupa mpya na muda

ukifika tutawaambia namna ya kuikataa katiba hii inayopendekezwa.

Busara inataka kura ya maoni ifanyike baada ya Uchaguzi Mkuu, lakini

wakiileta tukusanye nguvu zetu zote kuikataa Katiba Inayopendekezwa.

Ndugu Wananchi,

Mwaka 2014 unaisha kwa hasira. Tumeshuhudia Bunge letu likijadili moja

ya kashfa kubwa kabisa kupata kutokea katika nchi yetu. Zaidi ya shilingi

Bilioni mia tatu zimechotwa na kugawaiwa kama njugu tena na watu

wenye mamlaka na waliopewa heshima kubwa na umma. Hakuna kashfa

kubwa kama wizi uliofanyika kupitia Akaunti ya Tegeta Esrow. Ni wizi

mkubwa na tumewakamata wezi mchana kweupe kabisa. Nawakikishieni

kwamba juhudi zinazoendelea kufanywa na baadhi ya wezi wa fedha hizi

na vibaraka wao zitashindwa vibaya kwa sababu ukweli haujawahi

Page 6: Speech by Zitto Kabwe

6

kushindwa. Watashindwa kwa aibu. Na mimi nawashauri wanyamaze na

wakubali yaishe kwa sababu wataumbuka zaidi wakiendelea na

ujasiriamali wao wa kupika uwongo barabarani.

Kilichofanyika bungeni katika Mkutano wa 16 na 17 uliomalizika mwezi

Novemba mwaka 2014 kimeonyesha namna ambavyo umoja ni nguvu.

Wabunge wote bila kujali itikadi za vyama vyao walisimama kidete katika

kuhakikisha kwamba maazimio yaliyopendekezwa na Kamati ya PAC

yanatekelezwa kikamilifu.

Somo moja tunalojifunza ni kwamba tukishirikiana hakuna linaloweza

kushindikana katika kupigania maslahi ya taifa letu pendwa la Tanzania.

Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ni ushahidi tosha wa faida za kushirikiana.

Wananchi pia wameonyesha hasira zao dhidi ya Wizi wa fedha za Umma

kupitia uchaguzi huu.

Katika shilingi bilioni 306 zilizokuwa na zilizopaswa kuwa katika akaunti

ya Tegeta Escrow kuna fedha za Umma. Serikali inasema hazikuwa 306

bilioni bali 202 bilioni! Hii sio hoja ya msingi. Hoja ya msingi ni kwamba

hata zingekuwa bilioni moja, bado ndani yake kuna fedha za

umma na ilipaswa utekelezaji wa hukumu ya kupunguza kiwango cha

tozo ya uwekezaji kufanyika ili kujua kiasi cha fedha za umma.

Tapeli Harbinder Singh Seth alilipwa hizo zilizokuwemo katika

akaunti na akaendelea kulipwa bakaa na TANESCO kiasi kwamba shirika

hili linalofilisika linamlipa kila siku bwana huyu shilingi milioni 400.

Page 7: Speech by Zitto Kabwe

7

Kila siku inayokwenda kwa mungu tunamlipa mtu ambaye hajawekeza

hata senti tano nchini mwetu. Alikuja na briefcase tu. Kule Kigoma kuna

neno jipya siku hizi, linaitwa umazwazwa. Ni kama ujuha hivi. Huu ni

umazwazwa ambao wananchi hawapaswi kuukubali.

Watu watatu tu ambao ni raia wa kigeni walichora wizi huu kwa miaka

mitatu. Mtu mmoja anaitwa Bwana Baharuddin kutoka Malaysia, Bwana

Issa Ruwaih kutoka Oman na Bwana Singh kutoka Kenya na anaishi

Afrika Kusini.

Walidanganya nyaraka za kuuziana makampuni, bwana Baharuddin

akauza hisa za IPTL kutoka Mechmar kwenda kwa Bwana Issa wa

kampuni ya PiperLink na Bwana Issa naye akauza hisa hizo zikiwa

zimezuiwa na Mahakama kwa Bwana Seth wa kampuni PAP.

Mabwana hawa wanajua Watanzania ni mazwazwa na hawafanyi

uchunguzi wa kina, yaani ‘due diligence’ kwani hata kwenye EPA fedha

ziliibiwa kwa kutofanya due diligence na kwa kutumia kitu kinaitwa ‘deed

of assignment’.

Mabwana hawa wanajua kuwa Watanzania wenye ofisi za umma wana

njaa na watawahonga kidogo tu na kupitisha kila kitu. Ndivyo

ilivyofanyika.

Kama viongozi wetu wangefanya ‘due diligence’ kwenye manunuzi ya

makampuni haya kama Sheria ya Kodi ya Mapato inavyowataka,

tusingekuwa na skandali ya Tegeta Escrow.

Page 8: Speech by Zitto Kabwe

8

Mfumo uliganzishwa kwa rushwa. Ukitazama miamala ya malipo kutoka

akaunti ya Bwana Seth katika akaunti ya StanBic utaona fedha

zimekwenda benki za UAE na baadaye Oman na Malaysia. Fedha hizo

zilikwenda kuwalipa mabwana Baharuddin na Issa.

Serikali lazima ichukue hatua mara moja kuhakikisha fedha zilizokuwamo

kwenye akaunti ya Tegeta Escrow zinarudi, uamuzi wa mahakama ya

kimataifa unatekelezwa na fedha za umma zinarejeshwa TANESCO na zile

za binafsi zinalipwa kwa wamiliki halali. Tanzania haiwezi kuwa nchi ya

kubariki utapeli wa kimataifa na kuchafua sura ya nchi yetu mbele ya jamii

ya kimataifa.

Baraza la Taifa yaani Bunge, kupitia wawakilishi wa wananchi, tayari

wameamua na kupitisha maazimio. Kilichobakia ni maazimio hayo

kutekelezwa na Serikali. Hakuna mjadala katika maazimio ya Bunge,

maana katika maazimio hayo Serikali nayo imo; ilishiriki kikamilifu katika

kuyandaa na hatimaye kupitishwa na Bunge. Hakuna namna ya kukwepa

kutekeleza maazimio ya Bunge kwa ukamilifu wake; nasema hakuna, ni

utekelezaji tu.

Ndugu Wananchi,

Nataka niwambie watanzania kupitia mkutano huu muhimu wa Mtwara

kwamba yaliyotokea Bungeni ni mwanzo na si mwisho. Ni mwanzo wa

safari ndefu wa kujenga utamaduni wa uwajibikaji katika nchi yetu.

Page 9: Speech by Zitto Kabwe

9

Dhana ya Uwajibikaji ni dhana inayotaka kila kiongozi kuwajibika kwa

matendo yake katika utekelezaji wa shughuli za umma. Ni dhana ambayo

ni lazima kuienzi kama tunataka nchi yetu ibakie salama na yenye utulivu

kwani kukosekana kwa uwajibikaji kunaleta rushwa na ufisadi. Tusikubali

watu wachache kwa maslahi yao binafsi waendelea kuharibu heshima ya

nchi yetu. Tusikubali kamwe.

Ufisadi unarudisha nyuma maendeleo, unaleta umasikini, unaleta

vita na umwagaji damu. Ndio maana ni lazima kuimarisha taasisi za

uwajibikaji katika nchi yetu. Kufukuza mawaziri wanaposhindwa

kutekeleza wajibu, japo haitoshi, sio udhaifu bali ni mchakato wa

kuimarisha taasisi za Uwajibikaji na kukuza demokrasia kwa ujumla.

Mwalimu Nyerere alituasa kwamba cheo ni dhamana. Ukipewa heshima

ya kuongoza lazima ujiheshimu, ukishindwa kujiheshimu lazima uondoke,

kwa hiari au kwa kulazimishwa.

Waziri Mkuu mstaafu, Mzee wangu, Jaji Joseph Warioba, alipata

kunihadithia alivyojiuzulu wadhifa wake huo mwezi Machi mwaka

1990. Rais Mwinyi alihutubia Taifa kuingia mwaka mpya wa 1990 kwamba

rushwa imeshamiri ‘mpaka muuza njugu anaombwa rushwa’. Wizara

takribani nane zikahusishwa na rushwa ikiwamo Wizara ya Sheria

(mahakama), Wizara ya Mambo ya Ndani (uhamiaji na polisi) na Wizara

ya Ardhi.

Page 10: Speech by Zitto Kabwe

10

Mawaziri hawa nane walipaswa kuwajibika kwa kujiuzulu, lakini Mzee

Warioba aliona hiyo ni takribani nusu ya Serikali akamwomba Rais

ajiuzulu yeye ili Serikali mpya iundwe. Baada ya majadiliano marefu Mzee

Mwinyi akakubali na akalitaka Baraza zima la Mawaziri kujiuzulu. Lote

kabisa.

Akaunda upya Serikali, akamrejesha Warioba kama Waziri Mkuu lakini

akaondoa baadhi ya mawaziri. Mwaka 1990 ulikuwa mwaka wa Uchaguzi,

lakini Mzee Mwinyi hakusita kuunda upya Serikali. Maamuzi hayo ndio

yaliyomwingiza kwenye Baraza la Mawaziri ( kama Waziri Kamili) Meja

(wakati huo) Jakaya Mrisho Kikwete ambaye sasa ni Rais wa Jamhuri yetu.

Hivyo Rais akifanya leo sio jambo jipya. Uwaziri sio usultani, ni dhamana

tu ya kuongoza sehemu ya idara za Serikali.

Ndugu Wananchi,

Ni katika nchi ya Tanzania pekee ambapo waziri anaweza kutukana

wananchi waziwazi mchana kweupe na kuwaambia kwamba ni wajinga

na wapumbavu na akabaki katika ofisi ya Umma. Ni Tanzania tu ndipo

Katibu Mkuu wa Wizara anaweza kutukana wabunge kuwa ni washenzi

akaachwa bila kuchukuliwa hatua za kinidhamu. Huwezi kuwa na Taifa

lisiloheshimu wananchi na wawakilishi wao. Uwajibikaji ni suluhisho.

Uwajibikaji unaweka nidhamu. Uwajibikaji unatoa matumaini kwa watu

kuwa viongozi wao wanawajali.

Page 11: Speech by Zitto Kabwe

11

Mwenyezi Mungu ameweka utajiri wa nchi yetu wa mafuta na gesi asilia

kwenye mikoa ya Pwani na Kusini. Mikoa mingine pia mungu amejaalia

utajiri. Kanda ya Ziwa kuna dhahabu na almasi, nyanda za juu makaa ya

mawe, Kaskazini Mlima Kilimanjaro na Tanzanite na kadhalika. Hata

hivyo katika dhahabu yote iliyochimbwa na kuuzwa nje ya thamani ya

dola za kimarekani bilioni 13 kati ya mwaka 1998 na mwaka 2013, yaani

miaka 15, nchi yetu ilipata mapato ya dola za Kimarekani 650 milioni tu,

sawa na asilimia tano.

Naomba kurudia. Kwa miaka 15 ambayo dhahabu yetu ilichimbwa na

kuuzwa, Watanzania tumepata shilingi tano tu katika kila shilingi 100 !

Shilingi 95 zote zimekwenda kwa wageni. Kama sio umazwazwa ni nini?

Yote ni kwa sababu ya mikataba ya siri yenye makosa makubwa na yenye

kupendelea wawekezaji. Tunataka mikataba ya gesi iwe wazi kabla ya

uvunaji mkubwa kuanza ili kama kuna makosa turekebishe. Ndiyo maana

Kamati yenu ya PAC iliamuru viongozi wa TPDC waswekwe ndani kwa

kukataa kuweka mikataba hii wazi kwa wajumbe wa Kamati ili

waitathimini kwa niaba ya wananchi.

Hatutaki viongozi ambao kazi yao ni kuombaomba kwa wawekezaji ili

kuwasaidia katika miradi yao ya kisiasa. Tunataka, kwa mfano, mtu kama

DANGOTE anapowekeza hapa Mtwara, watu wa Mtwara na Watanzania

wafaidike na sio wanasiasa. Kuomba omba rushwa kunatia doa heshima

yetu mbele ya mataifa ya ulimwengu.

Page 12: Speech by Zitto Kabwe

12

Ndugu Wananchi,

Tunaingia mwaka 2015 kifua mbele katika vita dhidi ya ufisadi na katika

kusimika uwajibikaji nchini. Tunataka Watanzania wote wenye

uzalendo kwa nchi yao kuungana na vyama vya upinzani katika

kuhakikisha uwazi na uwajibikaji nchini kwetu. Kwa upande wa Kamati

ya PAC tunawahakikishia utendaji uliotukuka zaidi. Katika Bunge la

mwezi Januari, mkutano wa 18 moja ya jambo tutakalolitolea taarifa ni

ukwepaji mkubwa wa kodi katika mauzo ya Korosho nje ya nchi, uagizaji

holela wa Sukari na nguo. Fuatilie Bunge hili kwa makini.

Tunautangaza Mwaka 2015 kuwa ni mwaka wa kuwajibishana.

Uwajibikaji unahitajika zaidi mwaka 2015 kuliko wakati mwingine wowote

katika miaka mitano iliyopita. Tuungane kuhakikisha Serikali

inawajibika kwa wananchi badala ya kuweka mipango ya kuchakachua

uchaguzi.

Lakini nimalizie kwa kusema wazi wazi kwamba kujaribu kuiajibisha

serikali ya CCM kupitia Bunge ni kazi kubwa na ngumu mno. Hawa watu

ni sawa na kumpigia mbuzi gitaa. Hawasikii. Hawaoni. Hawaambiliki.

Wameshazibwa mifumo ya fahamu. Hiyo ndiyo hatatari ya rushwa na

ufisadi. Yote tunayoyafanya bungeni na nje ya Bunge kama wapinzani ni

mambo ya muda mfupi. Suluhu ya kudumu ya uwajibikaji kwa serikali ya

CCM mnayo ninyi wananchi. Nami nawaomba mtusaidie muda ukifika

mwakani mchukue HATUA kupitia kura zetu.

Page 13: Speech by Zitto Kabwe

13

Hakuna tena muda wa kuwachekea hawa CCM. Tuwaweke pembeni na

hili linawezekana kwa sababu tayari mmeshaonyesha kwamba mnaweza

kupitia uchaguzi wa serikali za mitaa.

Tunapouanza mwaka mpya, kila mwenye mapenzi ya kweli ya nchi hii

aungane na kufanya kazi pamoja na kwa bidii katika kuijenga Tanzania

bora kwa kila Mtanzania. Tanzania imara, yenye kujali haki na utu wa raia

wake na yenye demokrasia na uwajibikaji inawezekana. Tuchukue hatua

sasa!

Namshukuru tena ndugu yangu, mjomba wangu Profesa Ibrahimu

Lipumba, msomi mwana mapinduzi, kwa fursa hii adimu.

Asanteni sana kwa kunisikiliza

… Hakiiii…..