Click here to load reader
Upload
sirbus-gents
View
83
Download
1
Embed Size (px)
DESCRIPTION
Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uzinduzi wa uchunguzi wa saratani ya mlango wa uazi na matiti Morogoro
Citation preview
HOTUBA YA MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI
WA UFUNGUZI WA HUDUMA ZA UCHUNGUZI WA SARATANI YA MLANGO WA KIZAZI NA YA MATITI
MKOANI TABORA, TAREHE 7 JUNI, 2014
Mhe. Mama Salma Kikwete, Mlezi wa MEWATA;
Mhe. Kebwe Steven Kebwe (Mb.), Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa
Jamii;
Mhe Fatma Mwasa, Mkuu wa Mkoa wa Tabora;
Wakuu wa Wilaya – Tabora, Nzega na Urambo;
Wabunge Wote wa Mkoa wa Tabora Mliopo;
Dkt. Serafina Mkuwa, Mwenyekiti wa MEWATA;
Wawakilishi wa Washirika Wetu wa Maendeleo;
Dkt. Joseph Komwihangiro, Mwakilishi wa Marie Stopes;
Madaktari Wote wa MEWATA na Watumishi wa Sekta ya Afya;
Mwakilishi wa Shirika la Marie Stopes na Wawakilishi wa Mashirika
Yasiyo ya Kiserikali Waliopo;
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Shukrani na Pongezi
Niruhusuni nianze kwa kuwashukuru Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dkt. Seif
Rashid (aliyewakilishwa hapa leo na Naibu Waziri Mhe.Dkt. Stephen Kebwe) na
Mwenyekiti wa Chama cha Madakatari Wanawake Tanzania (MEWATA), Dkt.
Sarafina Mkuwa kwa kunialika kuja kuzindua huduma za uchunguzi wa saratani ya
mlango wa kizazi na saratani ya matiti Mkoani Tabora. Nawapongeza nyote kwa
maandalizi mazuri kwani ni ukweli usiopingika kuwa shughuli hii imefana
sana. Aidha, nawashukuru wenyeji wetu wa Mkoa wa Tabora wakiongozwa na Mkuu
wa Mkoa, Mheshimiwa Fatma Mwasa, kwa mapokezi mazuri mliyonipatia mimi, mke
wangu na wageni wenzetu. Sikutegemea kupata mapokezi tofauti na haya hapa
Tabora, kwani upendo wenu kwangu na ukarimu wenu tunaujua na unasifika na
wengi.
Madhumuni ya Ziara
Ndugu Wananchi;
Nimekubali kuja kujumuika nanyi katika uzinduzi huu, siku ya leo, ili kuongeza sauti
yangu na uzito kuhusu shughuli hii muhimu na adhimu inayofanywa na Madaktari
Wanawake hapa nchini. Ni ukweli ulio wazi kuwa MEWATA imesaidia kuokoa maisha
ya akinamama wengi nchini ambao, vinginevyo, wangepoteza uhai kwa saratani hizi
mbili zinazowapata wanawake. Hatuna budi kuvunja ukimya na kuungana na
Madaktari Wanawake kuzungumzia maradhi haya na kuelimishana ili wananchi,
wadau na Serikali kwa umoja wetu au mmoja mmoja, tuchukue hatua stahiki za
kukabiliana na maradhi haya.
Aidha, ni nafasi nzuri ya kutoa pongezi zangu kwa wanachama wa MEWATA kwa kazi
kubwa na nzuri waifanyayo na mafanikio yaliyopatikana. Sijui hali ya maradhi haya
ingekuwaje hapa nchini kama Madaktari Wanawake wasingeamua kufanya kazi hii
njema wanayoifanya. Kwa niaba ya wanawake na wanaume wote wa Tanzania
tafadhali pokeeni pongezi zetu za dhati. Endeleeni kufanya kazi hii njema na
Mwenyezi Mungu atawalipa kwa wema wenu na mioyo yenu ya huruma. Nawaahidi
kuendelea kuwaunga mkono kwa hali na mali na kwa kadri ya uwezo
utakavyoniruhusu.
Nimefurahi sana kwamba ndugu zetu wa MEWATA wameweza kufika hapa Tabora
siku ya leo. Mtakumbuka kuwa nilipokuja kwenye Sherehe za Siku ya Wanawake
Duniani tarehe 8 Machi, 2010, niliahidi kwamba nitawaomba MEWATA waje kufanya
uchunguzi wa saratani za mlango wa kizazi na matiti kwa akinamama. Hayawi hayawi
leo yamekuwa. Nawashukuru sana viongozi na wanachama wa MEWATA kwa kuja
kwenu. Mmenitoa kimasomaso. Wahenga walisema: “Ada ya Mja kunena,
muungwana na vitendo”. Ndugu zangu wa Tabora ahadi imetimia, kazi
kwenu. Jitokezeni kwa wingi kupima muokoe maisha yenu.
Hali ya Magonjwa ya Saratani ya Wanawake Nchini
Ndugu Wananchi,
Tanzania inatambulika kuwa ni moja ya nchi zenye kiwango kikubwa cha maradhi ya
saratani ya mlango wa kizazi hapa Afrika ya Mashariki. Inakadiriwa kuwa takriban
wanawake 56 katika kila wanawake 100,000 hupata saratani hii. Inakadiriwa pia kuwa
zaidi ya watu 35,000 wanapata saratani hii kila mwaka na zaidi ya watu 27,000
hupoteza maisha. Mwaka 2010 peke yake, wanawake wapatao 6,000 waligundulika
kuwa na saratani ya mlango wa kizazi na wanawake 4,000 kati yao walifariki dunia.
Wataalamu wanatuambia kuwa, saratani hii huwapata wanawake wa umri wa miaka
30 na 50. Aidha, wanawake wanaoishi na virusi vya UKIMWI wako katika hatari zaidi
ya kupata ugonjwa huo kwa asilimia 50. Pamoja na tatizo hili, bado tunayo
changamoto ya saratani ya matiti ambayo ni ya pili kwa kusababisha vifo vya
wanawake wengi nchini. Hivyo basi, hapa nchini wanawake wako kwenye hatari
kubwa ya kufa kwa saratani kuliko wanaume kwa sababu saratani nyinginezo,
hazibagui ukiacha ile ya tezidume inayowapata wanaume pekee.
Hatua za Tahadhari za Kuzingatiwa
Bahati nzuri, saratani ya mlango wa kizazi na saratani ya matiti zinaweza kutibika
ikiwa zitagunduliwa mapema. Njia pekee ya kuweza kugundua mapema ni kupima
mara kwa mara. Wataalamu wanashauri kuwa ni vyema wanawake wenye umri wa
kati ya miaka 30 na 50 wakachunguza afya zao walau mara moja katika kila miaka
mitatu. Na, kwa wanawake wanaoishi na virusi vya UKIMWI wanashauriwa
kuchunguzwa walau mara moja kwa mwaka.
Bahati mbaya sana, uzoefu umeonyesha kuwa wanawake wengi hufika hospitali wakati
ambapo ugonjwa umeshapea na kuenea sehemu nyingine za mwili. Wanakwenda
hospitali wakati maradhi yamefikia hatua isiyoweza kutibika na hivyo kupoteza
maisha. Hivyo basi, kupima na kugundulika mapema kwa saratani ni hatua muhimu
sana ya kuepusha vifo vinavyotokana na maradhi hayo. Bahati nzuri hivi karibuni
kumekuwepo na mwamko na mwitikio mzuri wa kujitokeza kwa wanawake wengi
kupima saratani ya matiti. Haya ni matunda ya kazi nzuri inayofanywa na
MEWATA. Juhudi hizi zinapaswa kuendelezwa. Zinastahili kuungwa mkono.
Hatua Zinazochukuliwa na Serikali
Ndugu Wananchi;
Serikali imechukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na saratani ya mlango wa
kizazi. Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeanzisha Programu inayoshughulikia
masuala ya Saratani za Uzazi katika Kitengo cha Afya ya Uzazi na Mtoto mwaka 2008.
Kupitia programu hii tuna Mpango Mkakati wa Kukinga na Kudhibiti Saratani ya
Mlango wa Kizazi (2011-2016). Mwongozo wa kutoa huduma umeandaliwa pamoja
na miongozo ya mafunzo kwa watoa huduma na ujumbe wa kuelimisha jamii kupitia
njia mbalimbali. Kupitia programu hii tumeweza kuanzisha vituo zaidi ya 130
vinavyotoa huduma ya uchunguzi wa Saratani ya Mlango wa Kizazi katika Mikoa 17
hapa nchini. Ukilinganisha na mwaka 2008 tulipokuwa na vituo vinne tu vilivyokuwa
vinatoa huduma hii ya uchunguzi wa Saratani ya Mlango wa Kizazi na tiba ya
mabadiliko ya awali, haya ni maendeleo makubwa.
Ndugu Wananchi,
Kupitia Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Serikali imeendelea kushirikiana na
wadau mbalimbali wakiwemo MEWATA, Marie Stopes, WAMA na wengineo
kutekeleza mpango wa “Utepe wa Pinki na Utepe Mwekundu” yaani “Pink Ribbon Red
Ribbon”. Kupitia program hiyo, kampeni ya uchunguzi wa saratani ya mlango wa
kizazi na matiti ilizinduliwa katika mkoa wa Mwanza mwezi Machi mwaka huu katika
kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani.
Kupitia mpango huo, tumekabidhi mashine 16 za kutolea huduma za matibabu ya
mabadiliko ya awali ya saratani ya mlango wa kizazi (Cryotherapy machine) kwa
mikoa ya Mwanza, Mara, Iringa, Njombe na Mbeya. Mipango inaendelea kwa mikoa
iliyosalia pamoja na Tabora kupatiwa mashine hizo kuendeleza juhudi za Serikali
kupanua upatikanaji wa huduma hizi katika mikoa yote nchini.
Lengo letu katika kufanya hivyo ni kutaka kupunguza mzigo mkubwa unaoielemea
Hospitali yetu ya kuu kansa ya Ocean Road. Pia, tunataka kuwapunguzia wanawake
adha na gharama ya kusafiri umbali mrefu hadi Dar es Salaam kwa ajili ya
uchunguzi. Tunatambua umuhimu wa huduma hizi kuwa karibu zaidi na walipo watu
ili ziwafikie wanawake wote bila kujali hali zao za kipato.
Ndugu Wananchi;
Katika jitihada za kutokomeza maradhi haya, Serikali, kupitia Mpango wa Taifa wa
Chanjo, imeanza kutoa chanjo ya kuzuia Saratani ya mlango wa Kizazi ya “Human
Papilloma Virus (HPV)”. Chanjo hii hutolewa kwa watoto wa kike wenye umri wa
miaka 9. Chanjo hii hukinga wasipate maambukizi ya virusi ambavyo husababisha
Saratani ya Mlango wa Kizazi. Wizara ya Afya tayari imezindua mpango huo wa utoaji
wa chanjo ya HPV kwa wasichana tarehe 29 Aprili, 2014 wakati wa Maadhimisho ya
Wiki ya Chanjo Duniani na mama Salma Kikwete. Mpango huo ulizinduliwa kwa
Halmashauri tano za Hai, Siha, Moshi Vijijini, Moshi Mjini na Rombo za Mkoa wa
Kilimanjaro, kuashiria kuanza kwa utekelezaji wa azma ya kutoa chanjo hii nchi nzima
ifikapo mwaka 2016.
Shukrani kwa Wadau
Ndugu Wananchi;
Napenda kutoa pongezi na shukrani za pekee kwa MEWATA kwa kazi nzuri na kubwa
ya kukuza uelewa wa jamii na kuhamasisha uchunguzi wa saratani zinazowapata
wanawake. Ni dhahiri kwamba ili jambo hili lifanikiwe lazima liwe na mshika bango
wake. Bahati nzuri ndugu zetu wa MEWATA wamejitoa kimasomaso na wamefanya
kazi ya Serikali kuwa rahisi. MEWATA imekuwa inafanya kazi kwa karibu na Serikali
pamoja na wadau wengine katika kuhamasisha jamii kuhusu masuala ya Saratani ya
Matiti na ya Mlango wa Kizazi. Kama nilivyokwisha kusema awali, juhudi hizo
zimewafikia wanawake wengi nchini na kuokoa maisha yao.
Aidha, napenda kuchukua fursa hii kutambua na kutoa shukrani maalum kwa Shirika
la Marie Stopes na wadau wote ambao wanashirikiana na Serikali katika kupambana
na tatizo hili kubwa la Saratani ya Mlango wa Kizazi. Vilevile, tunawashukuru wale
wote wanaotoa huduma ya afya ya uzazi na mtoto nchini. Napenda kwa mara nyingine
tena kuwahakikishia ushirikiano wa Serikali ya CCM ninayoiongoza kwenu. Ni,
dhamira yetu kupunguza na ikiwezekana hata kumaliza kabisa vifo vitokanavyo na
Saratani ya Mlango wa Uzazi na Saratani ya Matiti ambazo kwa kweli zinaweza
kuzuilika.
Wito kwa Wananchi
Ndugu Wananchi;
Natoa wito kwa wanawake wa Tabora kujitokeza kwa wingi kufanyiwa uchunguzi wa
saratani hizi na wataalamu walioko hapa. Napenda kuwatoa hofu kuwa saratani ya
mlango wa kizazi na saratani ya matiti siyo magonjwa ya aibu au ya mkosi au uchawi
au laana na wala siyo magonjwa yasiyotibika. Magonjwa haya huweza kumpata
mwanamke ye yote, awe ameolewa au hajaolewa, awe amezaa au hajazaa, awe tajiri au
maskini. Madhali ni mwanamke anaweza kupata. Sharti lake la kupona ni
kugundulika mapema na kuanza tiba mapema. Kuchelewa kugundulika na kuchelewa
kuanza matibabu ndiko kunakosababisha vifo kutokana na maradhi haya. Waswahili
wana msemo usemao, mficha maradhi kifo humuumbua. Hivyo ndugu zangu kina
mama nashauri mfanye uchunguzi mapema, ili kama kuna tatizo muanze tiba
mapema.
Napenda kutumia fursa hii, kuwaasa akina baba na walezi nao kusaidia katika juhudi
za kuzuia na kutibu magonjwa haya ya saratani ya wanawake. Mwanamke anayepata
magonjwa haya anahitaji matunzo na upendo siyo masimango na unyanyapaa.
Masimango na unyanyapaa huwafanya wanawake waogope kujitokeza kuchunguza
afya zao na kupatiwa tiba kwa kuogopa kubaguliwa au kuachwa. Magonjwa haya
yanatibika. Si kila mwanamke anayepata saratani hufariki dunia. Kinachotakiwa ni
baba na mama kushirikiana kumpeleka mama kufanyiwa uchunguzi na kupata tiba
iwapo atagundulika kuwa na maradhi. Saratani siyo ugonjwa wa zinaa, hivyo,
msiwanyanyapae akina mama bali muwalee na kuwatunza ili waweze kurejea katika
hali zao za kawaida. Akina baba muwe ndiyo nguzo ya mafanikio katika mapambano
dhidi ya saratani.
Na, kwa wanaume wenzangu, tujenge mazoea ya kupima afya zetu hususan kuhusu
saratani ya tezidume (prostate). Hii ni saratani inayoua wanaume wengi duniani na
hapa nchini. Lakini nayo kama zilivyo saratani za matiti na mlango wa kizazi
zinatibika kama zitagundulika mapema. Kila mkienda kupima afya pimeni afya ya
tezidume mjue mustakabali wenu.
Ndugu Wananchi;
Sote tukiungana pamoja tunaweza kutokomeza saratani ya mlango wa kizazi na
saratani ya matiti. Nia ya kutokomeza maradhi haya tunayo, sababu ya kutokomeza
tunayo na uwezo wa kuyatokomeza tunao. Kinachotakiwa ni kuunganisha nguvu zetu
pamoja. Mimi na mke wangu Mama Salma Kikwete tuko nanyi na tutaendelea kuwa
nanyi bega kwa bega katika vita hii sasa na hata baada ya kuacha Urais
mwakani. Inawezekana, timiza wajibu wako!
Ndugu Wananchi;
Kwa vile niko Tabora ni vyema nikatumia nafasi hii pia, kuyazungumzia baadhi ya
mambo niliyoyazungumzia au kuahidi kufanya safari zilizopita. Kwa upande wa
barabara, napenda kuwahakikishia kuwa barabara kuu zinazoendelea kujengwa hapa
Mkoani Tabora tutazimaliza. Subira yavuta heri. Barabara ya Urambo –Kaliua ujenzi
utaanza mwaka huu wa fedha na Chaya – Nyahua, mchakato wa kutafuta fedha
unaendelea ili nayo ujenzi wake uweze kuanza kabla ya mimi kumaliza kipindi changu
cha uongozi. Kuhusu kupata maji ya Ziwa Victoria, kwa Igunga, Nzega, Tabora,
Urambo na Sikonge hatua za awali zimeanza na kinachofuatia ni kutafuta fedha kwa
ajili ya mradi huo mkubwa. Tunakusudia kuiomba Serikali ya India ambayo ndiyo
iliyogharamia matayarisho ya mradi. Tuna matumaini ya kufanikiwa. Sote tuzidi
kuomba iwe hivyo.
Kwa upande wa tatizo la wakulima wa tumbaku kutokulipwa stahili zao na vyama vya
ushirika nimeelezwa na kulielewa. Kuna tuhuma za wizi na ubadhilifu. Nimemuagiza
Inspekta Jenerali wa Polisi atume watu wake wa upelelezi wa makosa ya Jinai waje
wafanye uchunguzi ili wahusika wakamatwe na kufikishwa Mahakamani na kupewa
adhabu zinazostahili. Ameniahidi kuwa keshokutwa Jumatatu watu hao
watakuja. Wapeni ushirikiano unaostahili ili tukomeshe uhalifu na dhuluma
zinazofanywa na Maofisa wa Vyama vya Ushirika na taasisi za fedha kwa muda mrefu
sasa.
Baada ya kusema hayo, naomba nitangaze sasa zoezi hili la uchunguzi wa Saratani ya
Mlango wa Kizazi na ya Matiti limefunguliwa rasmi.
Nawashukuruni sana.