Upload
others
View
4
Download
0
Embed Size (px)
Citation preview
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
MUHTASARI WA MFUMO WA SERA ZA JUMLA ZA UCHUMI NA MAENDELEO YA
JAMII KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2011/12-2015/16
Imetolewa na Wizara ya Fedha
Mei, 2011
2
MUHTASARI WA MFUMO WA SERA ZA JUMLA ZA UCHUMI NA MAENDELEO YA
JAMII KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2011/12-2015/16
3
YALIYOMO
UTANGULIZI ........................................................................................................................................ 1 MAPITIO YA MWENENDO WA UCHUMI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2010 .............................. 1 Mwenendo wa Uchumi wa Dunia .................................................................................................. 1 Ukuaji wa Pato la Taifa ................................................................................................................... 2 Mwenendo wa Bei ........................................................................................................................... 2 Mapato na Matumizi ya Serikali ..................................................................................................... 4 Deni la Taifa .................................................................................................................................... 5 Ujazi wa Fedha na Karadha ........................................................................................................... 6 Maboresho ya Sekta ya Fedha ....................................................................................................... 7 Sekta ya Nje .................................................................................................................................... 9 Ushirikiano wa Kiuchumi wa Kikanda ............................................................................................ 9 Uendelezaji wa Sekta Binafsi ......................................................................................................... 9 Tathmini ya Dira na Mpango wa Maendeleo wa Muda wa Kati na Mrefu ............................... 10 MKUKUTA na Malengo ya Maendeleo ya Milenia (MDGs) ......................................................... 10 Utafiti wa Afya na Demografía 2010-TDHS ................................................................................ 11
MASUALA MUHIMU YA KISERA YALIYOJITOKEZA MWAKA 2010/11 ........................................... 12 Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/12 – 2015/16) .............................................. 13
Vipaumbele Vya Kisekta ................................................................................................................... 14 MISINGI NA MALENGO YA UCHUMI JUMLA NA MAENDELEO YA JAMII 2011/12-2015/16 ...... 19 HITIMISHO ........................................................................................................................................ 20
1
UTANGULIZI
1. Taarifa hii inatokana na uchambuzi wa mwenendo wa viashiria muhimu katika
maendeleo ya kiuchumi na kijamii, na unyambuaji wa masuala muhimu
yaliyojitokeza nchini, kikanda na duniani katika mwaka 2009/10 hususan suala la
ukame uliojitokeza nchini mwishoni mwa mwaka 2010 na athari zake kwa sekta
mbalimbali za kiuchumi kama vile katika kilimo, nishati na uzalishaji viwandani na
kupanda kwa kasi bei za mafuta katika soko la dunia. Aidha, taarifa hii imezingatia
maamuzi ya msingi ya Serikali hasa suala la kuandaa mpango kwa kuzingatia mfumo
wa miaka mitano. Pia inalenga katika kukabiliana na athari za upatikanaji wa
umeme wa uhakika; kutengemaza na kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi;
kuboresha maendeleo ya jamii; na kupunguza umaskini katika miaka mitano ijayo.
Vile vile, taarifa hii inazingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 ambayo imefanyiwa
mapitio hivi karibuni, Malengo ya Maendeleo ya Milenia, Awamu ya Pili ya Mkakati
wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania (MKUKUTA II), na vipaumbele
vya uwekezaji vilivyoainishwa katika Mwongozo wa Mpango na Bajeti 2011/12
_2015/16.
MAPITIO YA MWENENDO WA UCHUMI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA
2010
Mwenendo wa Uchumi wa Dunia
2. Kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Fedha Duniani, uchumi wa dunia umekua
kwa asilimia 5 mwaka 2010 ikilinganishwa na ukuaji hasi wa asilimia 0.6 uliotokea
mwaka 2009 kutokana na msukosuko wa masoko ya fedha na mitaji uliotokea
mwaka huo. Kiwango kikubwa cha ukuaji wa uchumi mwaka 2010 kilitokana na
kuongezeka kwa kiasi kikubwa kwa mahitaji ya walaji katika nchi za Marekani na
Japan, pamoja na hatua za makusudi zilizochukuliwa na nchi mbalimbali kuweka
vichocheo vya kibajeti na kifedha vya kukuza uchumi (“stimulus package”). Kiwango
cha ukuaji wa uchumi katika bara la Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara kilikuwa
asilimia 5 mwaka 2010 ikilinganishwa na asilimia 2.8 mwaka 2009 kutokana na
kuanza kuimarika kwa bei za bidhaa zinazouzwa nje na kuongezeka kwa mahitaji
2
katika soko la ndani. Changamoto bado ipo hususan ikizingatia kuwa nchi nyingi
katika ukanda huu zinatemegea misaada na mikopo kutoka nchi zilizoendelea
ambazo zimepunguza bajeti zao ili kuziba nakisi iliyopatikana wakati wa msukosuko.
Hali kadhalika, tetemeko la ardhi lililotokea nchini Japan linatarajia kuathiri uchumi
wa dunia na upatikanaji wa mikopo na misaada kwa nchi zinazoendelea ingawa
taarifa za hivi karibuni zinaeleza kuwa Japan itaendelea kutoa misaada yake kama
ilivyopangwa licha ya matatizo iliyoyapata.
Ukuaji wa Pato la Taifa
3. Ukuaji halisi wa Pato la Taifa ulikuwa asilimia 7.0 mwaka 2010 sawa na
ilivyokadiriwa ikilinganishwa na asilimia 6.0 mwaka 2009. Ukuaji huu ulitokana na
kuongezeka kwa viwango vya ukuaji katika kilimo kufuatia kuwepo kwa hali nzuri ya
hewa katika msimu wa kilimo wa mwaka 2009/10, na hatua za serikali za kutoa
ruzuku ya pambejeo za kilimo na kuimarika kwa miundombinu ya umwagiliaji na ya
barabara na utekelezaji wa mpango wa dharura wa kunusuru uchumi (rescue
package). Sekta zilizochangia ukuaji huu ni pamoja na biashara na matengenezo,
kilimo na ufugaji, usafirishaji na mawasiliano na uzalishaji viwandani.
Mwenendo wa Bei
4. Ofisi ya Taifa ya Takwimu ilibadilisha mwaka wa kizio wa Fahirisi za Bei za
Taifa kutoka mwaka 2001 kuwa mwaka 2007 kwa kutumia matokeo ya Utafiti wa
Mapato na Matumizi ya Kaya Binafsi wa mwaka 2007. Mabadiliko haya yalifanywa
kwa kutumia makundi yaliyokubalika Kimataifa yanayoitwa Mchanganuo wa Matumizi
Binafsi “Classification of Individual Consumption by Purpose (COICOP)” na maeneo
ambayo mara nyingi jamii hununua bidhaa au hupata huduma mbalimbali (Outlets).
Mfumo huu mpya wa ukokotoaji wa fahirisi za bei unatumia wastani wa kijiometria
(geometric mean) badala ya wastani wa kawaida (arithmetic mean) katika
kutengeneza Fahirisi za Bei katika ngazi za mwanzo kama inavyokubalika kimataifa
kwa ulinganisho. Mizania mpya zinajumuisha matumizi ya kaya zote binafsi kutoka
mijini na vijijini wakati mizania iliyokuwa inatumika zamani ilijumuisha kaya binafsi
za maeneo ya mijini tu. Bidhaa na huduma mbalimbali za jamii zimeboreshwa kwa
3
kujumuisha bidhaa na huduma mpya na kuondoa zile ambazo zimeonesha
kutotumiwa sana na walaji kwa sasa.
.
5. Mfumo huu wa kutumia wastani wa kijiometria ulianza kutumika Oktoba 2009,
kwa kipindi cha miezi 12 ulitoa mfumuko wa bei wa asilimia 4.2 kwa mwezi Oktoba
2010. Hii ilikuwa ni badiliko la asilimia 0.3 ikilinganishwa na mfumuko wa bei
uliotumia wastani wa kawaida wa mwezi Septemba 2010 ambao ulikuwa asilimia
4.5. Aidha, kama wastani wa kawaida ungetumika, mfumuko wa bei ungekuwa
asilimia 4.1 kwa mwezi Oktoba 2010 ikilinganishwa na asilimia 4.2 kwa kutumia
wastani wa kijiometria. Kwa wastani, mfumo wa awali unaonesha kutoa mfumuko
wa bei ambao hautofautiani sana na unaotolewa kwa kutumia mfumo mpya.
6. Pamoja na mfumuko wa bei kuendelea kuwa tarakimu moja, umekuwa na
mwelekeo wa kupanda hususan katika robo ya kwanza ya mwaka 2011. Mfumuko
wa bei umeongezeka kutoka asilimia 5.6 kwa kipindi kilichoishia Desemba 2010 hadi
asilimia 6.4 Januari 2011 na kuendelea kupanda hadi asilimia 8.6 mwezi Aprili 2011.
Kasi hiyo ya ongezeko la bei ilitokana hasa na kuongezeka kwa wastani wa fahirisi ya
bei za umeme, gesi, chakula na vinywaji visivyo na kilevi.
7. Mfumuko wa bei ambao haujumuishi vyakula na nishati kwa mwaka ulioishia
Aprili 2011 ulipungua kufikia asilimia 5.7 kutoka asilimia 6.3 Machi 2011. Aina hii ya
Fahirisi haijumuishi vyakula vilivyoliwa majumbani na hotelini, vinywaji baridi, petroli,
dizeli, gesi, mafuta ya taa, mkaa na umeme. Vyakula na nishati vina sifa ya kuwa na
bei ambazo hubadilika mara kwa mara na kisera inakuwa vigumu kusimamia bei hizi.
Hivyo vikiondolewa kwenye Fahirisi ya bidhaa na huduma zote hubakia Fahirisi
ambayo ina mwelekeo imara kisera hususan kwa kutumia sera za fedha na mapato
na matumizi kusimamia mwenendo wa bei. Mfumuko wa bei wa nishati uliongezeka
kufikia asilimia 22.1 na wa vyakula ulifikia asilimia 9.2 Aprili 2011 ikilinganishwa na
asilimia 17.2 na 8.3 Machi 2011 kwa mtiririko huo.
4
Mapato na Matumizi ya Serikali
8. Mapato ya ndani yaliongezeka kwa asilimia 8.2 mwaka 2009/10 kufikia
shilingi bilioni 4,661.540 kutoka shilingi 4,293.074 bilioni mwaka 2008/09. Hata
hivyo, kiasi hicho kilichokusanywa ni pungufu ya makadirio kwa asilimia 8.8 kwa
mwaka 2009/10. Wastani wa makusanyo kwa mwezi unaonesha kuwa mapato ya
ndani yalikuwa yakiongezeka mfululizo kutoka wastani wa shilingi bilioni 174.8 kwa
mwezi mwaka 2005/06 hadi shilingi bilioni 388.5 kwa mwezi mwaka 2009/10.
Misaada ya nje katika mwaka 2009/10 ilikuwa shilingi bilioni 1,405.3, mikopo ya nje
ilikuwa shilingi bilioni 1,379.6 na mikopo ya ndani ilikuwa shilingi bilioni 568.5. Katika
kipindi cha nusu ya kwanza ya mwaka 2010/11 (Julai – Disemba 2010), mapato ya
ndani yakijumuisha mapato ya Halmashauri yalifikia shilingi bilioni 2,778.9, ikiwa ni
asilimia 10 chini ya makisio ya shilingi bilioni 3,079.1 kwa kipindi hicho. Upungufu
huu ulitokana hasa na athari za msukosuko wa kiuchumi duniani. Pamoja na
kupungua kwa mapato ikilinganishwa na makisio, mapato yaliyopatikana katika
kipindi hicho yalikuwa asilimia 17.6 zaidi ya mapato yaliyokusanywa katika kipindi
kama hicho mwaka 2009/10.
9. Matumizi ya Serikali yalifikia shilingi bilioni 8,173.7 mwaka 2009/10 sawa na
asilimia 90.0 ya makadirio. Matumizi ya maendeleo yalikuwa asilimia 8.0 chini ya
lengo hasa kutokana na kuchelewa kwa utekelezaji wa miradi kulikosababishwa na
baadhi ya Wizara, Idara, Mikoa na Halmashauri kuchelewa kukamilisha taratibu za
ununuzi na kutoa taarifa za matumizi ya fedha za miradi. Matumizi ya kawaida pia
yalikuwa asilimia 8.0 chini ya malengo. Katika kipindi cha Julai - Desemba 2010,
matumizi ya Serikali yalifikia shilingi bilioni 5,052.7 ikiwa ni asilimia 83.4 ya makisio
ya matumizi ya shilingi bilioni 6,058.0. Matumizi ya maendeleo na ya kawaida
yalikuwa asilimia 19.0 na 15.8 chini ya makadirio kwa kipindi hicho kwa mtiririko
huo. Kupungua kwa matumizi hayo kunatokana na upungufu wa mapato katika
kipindi hicho.
5
Deni la Taifa
10. Deni la Taifa liliongezeka kwa asilimia 6.1 hadi Dola za Kimarekani milioni
11,380.2 katika kipindi kilichoishia Desemba 2010 kutoka Dola za Kimarekani milioni
10,725.92 Desemba 2009. Kati ya deni hilo, Dola za Kimarekani milioni 8,363.3
zilikuwa ni deni la nje, sawa na asilimia 73.5 ya deni lote na zilizobaki ni deni la
ndani. Kati ya kiasi hicho cha deni la nje, Dola za Kimarekani milioni 7,699.6
(asilimia 91.7) ni bakaa ya deni (Disbursed Outstanding Debt_DOD) na kiasi
kilichobaki cha Dola za Kimarekani milioni 693.7 ni malimbikizo ya riba. Kati ya kiasi
hicho cha deni la nje, Dola za Kimarekani milioni 1,863.4 (22.3%) ni deni la sekta
binafsi na kiasi kilichobaki cha Dola za Kimarekani milioni 6,529.6 zilikuwa ni deni la
sekta ya umma. Deni la ndani hadi kufikia Desemba 2010 lilikuwa shilingi bilioni
4,385.4, ikiwa ni ongezeko la asilimia 14.3 ikilinganishwa na kipindi kama hicho
mwaka 2009. Asilimia 62 ya deni hili ilikuwa ni hati fungani za Serikali. Ongezeko la
deni la Taifa limetokana na malimbikizo ya riba ya deni la nje hasa kwenye nchi
zisizo wanachama wa kundi la Paris ambazo hazijatoa misamaha ya madeni
kulingana na makubaliano, mikopo mipya ya ndani na nje kwa ajili ya kugharamia
miradi mbalimbali ya maendeleo na kushuka kwa thamani ya shilingi. Malipo ya deni
la nje katika kipindi cha nusu mwaka ulioishia Desemba 2010 yalikuwa shilingi
bilioni 62.8, na kati ya hizo, shilingi bilioni 38.8 zikiwa ni malipo ya riba. Malipo ya
deni la ndani kwa nusu mwaka ulioishia Desemba 2010 yalikuwa shilingi bilioni
632.4. Kati ya hizo, shilingi bilioni 424.7 zilitumika kulipia dhamana za Serikali
zilizoiva kwa utaratibu wa kukopa na kulipia dhamana zilizoiva (rollover) na shilingi
bilioni 107.7 zilikuwa ni malipo ya riba. Katika kutekeleza Mkakati wa Deni la Taifa,
Serikali imeendelea kusimamia kwa umakini deni la Taifa kwa kukopa zaidi kutoka
vyanzo nafuu kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo na kuchambua athari
zinazotokana na mikopo mipya. Kwa mujibu wa tathmini ya kuangalia uhimilivu wa
deni (Debt Sustainability Analysis) iliyofanyika mwezi Oktoba 2010 inaonesha kuwa
viashiria muhimu vya madeni ni himilivu na linahimilika. Kwa maana nyingine ni
kuwa, tunakopesheka kwa kuzingatia uwezo wetu wa kulipa na kufuata sheria ya
Mikopo, Dhamana na Misaada ya mwaka 1974 (iliyorekebishwa mwaka 2004) na
kanuni zake.
6
Ujazi wa Fedha na Karadha
11. Katika kipindi cha mwaka 2010/11, sera ya fedha ililenga kuwa na kiwango
cha ongezeko la ujazi wa fedha kinachoenda sambamba na mahitaji halisi ya
uchumi, kasi ya upandaji bei, ongezeko la mikopo ya ndani lisiloathiri uzalishaji mali
na ambalo linalingana na malengo ya ujazi wa fedha, na kuwa na akiba ya fedha za
kigeni itakayoweza kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje
kwa kipindi kisichopungua miezi mitano. Hadi Desemba 2010, ujazi wa fedha kwa
tafsiri pana (M2)1 ulikua kwa asilimia 21.8 kiwango ambacho kilikuwa chini ya
kiwango cha ukuaji cha asilimia 26.3 kwa mwaka ulioishia Juni, 2010. Hata hivyo,
kiwango hicho kilikuwa juu kidogo, kikilinganishwa na makadirio ya kiwango cha
asilimia 20.8 hadi Desemba 2010. Katika kipindi hicho, M3 ilikua kwa asilimia 25.4,
ikilinganishwa na asilimia 25.1 kwa mwaka ulioishia Juni, 2010, na hali kadhalika
ikilinganishwa na makadirio ya ukuaji wa asilimia 23.5 ifikapo Desemba 2010. Kasi
ya ongezeko la ujazi wa fedha kwa tafsiri pana zaidi ilitokana na kasi ya ongezeko la
amana katika fedha za kigeni, ambapo ziliongezeka kwa asilimia 23.3 kutoka dola za
kimarekani milioni 1,657.3 mwezi Desemba 2009 hadi dola milioni 2,043.6 mwezi
Desemba 2010, pamoja na kuimarika kwa dola ya kimarekani dhidi ya sarafu
nyingine. Akiba ya fedha za kigeni imeendelea kuongezeka hadi kufikia Dola za
Kimarekani milioni 3,948.0 Desemba 2010, kiasi ambacho kinatosha kuagiza bidhaa
na huduma nje kwa muda wa miezi 6.3. Kiwango cha ukuaji wa mikopo inayotolewa
kwa sekta binafsi kiliendelea kuongezeka na kufikia asilimia 20.0 Desemba 2010
kutoka asilimia 16.3 Juni 2010. Hii inatokana na kuanza kujengeka kwa imani ya
mabenki dhidi ya sekta binafsi kufuatia kuanza kuimarika kwa hali ya uchumi wa
dunia baada ya kupitia katika kipindi cha msukosuko wa Masoko ya Fedha na Mitaji.
Tofauti kati ya viwango vya riba vinavyotozwa kwenye mikopo na vile vinavyotolewa
kwenye amana kama faida vimeendelea kuwa juu, licha ya kuongezeka kwa
ushindani katika sekta ya kibenki. Hii imechangiwa kwa kiasi kikubwa na kukosekana
kwa taarifa sahihi za wakopaji (credit reference data bank) na kutokuwepo kwa
taasisi ya utoaji wa taarifa sahihi za waombaji mikopo (Credit Rerefence Bureau)
1 M0 ni fedha zilizo kwenye mzunguko nje ya mabenki; M1=M0 + amana za hundi; M2 = M1 + amana za muda maalum + amana za
akiba; M3 = M2 + amana za fedha za kigeni (foreign deposits)
7
nchini. Aidha, gharama kubwa za kufanya biashara kutokana na miundombinu
hafifu, nazo zimechangia kuongeza viwango vya riba vinavyotozwa kwenye mikopo.
Maboresho ya Sekta ya Fedha
12. Serikali ilianza kutekeleza Awamu ya Pili ya Mageuzi katika Sekta ya fedha
mwaka 2006/07. Mageuzi haya ni pamoja na kuimarisha sekta ya mabenki kwa
lengo la kuimarisha mazingira ya ushindani katika utoaji wa huduma, kuimarisha
masoko ya fedha, mageuzi katika usimamizi wa uwekezaji rasilimali kwa Mifuko ya
Hifadhi za Jamii, kuboresha utoaji wa mikopo ya muda mrefu ikiwa ni pamoja na
mikopo kwa ajili ya kilimo,mikopo ya makazi (Mortgage Finance) na Mikopo ya
karadha (Finance Leasing) na kuboresha taarifa za wakopaji kwa kuanzisha chombo
cha kutoa taarifa hizo (Credit Reference Bureau). Hadi sasa mafanikio makubwa
yamekwisha patikana ikiwa ni pamoja na Sekta ya fedha nchini kuendelea kukua
kwa kasi nzuri. Kulingana na vigezo na viashiria vya uimara wa sekta ya fedha,
mabenki yote nchini yanakidhi viwango vya mtaji unaoweza kuhimili madai (capital
adequacy ratio), yana ukwasi wa kutosha kukidhi malipo kwa wateja (liquidity ratio)
na ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi wa kuridhisha. Aidha, mfumo wa malipo
nchini umeboreshwa na kuleta ufanisi katika kutekeleza sera za kiuchumi na fedha.
Mfumo wa malipo baina ya mabenki nchini ulioanza kutumika rasmi mwaka 2004
umeendelea kuboreshwa kwa kuhakikisha kwamba unatumika kurahisisha
ukusanyaji wa mapato ya Serikali na baadhi ya malipo yanayofanywa na serikali. Hali
kadhalika, mfumo wa malipo ya hundi umeendelea kuboreshwa (kwa kutumia TISS2)
na kupunguza muda wa malipo ya hundi.
13. Katika mwaka 2010, Serikali iliendelea na maboresho ya sekta ya fedha
ambapo Kanuni zitakazotumika katika masuala ya taarifa za mikopo zilichapishwa
kupitia Tangazo la Serikali namba 177 na 178 la mwaka 2010 na kuanza kutumika
rasmi mwezi Oktoba 2010. Hali kadhalika, Serikali ilihitimisha mchakato wa
uanzishwaji wa Mamlaka ya Kusimamia Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (Social Security
Regulatory Authority - SSRA) ambayo jukumu lake ni kukuza ufanisi na kuongeza
2 TISS ni Tanzania Interbank Settlement System
8
ushindani katika mifuko ya pensheni na hivyo kuchangia zaidi kwenye ustawi wa
uchumi. Aidha, serikali inaendelea na mchakato wa kuboresha taratibu za mafao ya
mifuko yote ya hifadhi ya jamii ili ilingane na iwe endelevu. Aidha, maboresho
mengine ni pamoja na kuiwezesha Benki ya Rasilimali Tanzania kutoa mikopo ya
muda mrefu. Serikali pia inandaa mfumo kabambe wa kisera na kisheria wa
utaratibu wa upatikanaji na utoaji wa mikopo ya muda mrefu.
14. Licha ya mafanikio yaliyopatikana chini ya programu ya uboreshaji wa sekta
ya fedha, zipo changamoto ambazo Serikali itaendelea kutafuta ufumbuzi wake.
Changamoto kubwa ni viwango vikubwa vya riba kwenye mikopo ambavyo
vimeendelea kutozwa na benki zetu ikilinganishwa na faida ndogo inayolipwa kwa
amana (interest rate spread). Serikali inaendelea na mkakati wa kuimarisha soko la
dhamana za serikali ili kufikia viwango halisi vya riba vinavyotokana na nguvu za
soko na visivyobadilika mara kwa mara. Hali kadhalika, Serikali inaendelea kubuni
mikakati yenye lengo la kuimarisha miundombinu katika sekta ya fedha pamoja na
kuimarisha mazingira ya ushindani katika sekta hiyo. Vile vile, changamoto nyingine
ni ufinyu wa mikopo ya muda mrefu pamoja na wananchi wengi, hasa wa vijijini,
kutofikiwa na huduma za kibenki. Hata hivyo, wananchi wengi zaidi hasa wa vijijini
ambako huduma za kawaida za kibenki zilikuwa hazipatikani wameanza kunufaika
kutokana na ongezeko la matumizi ya simu za mkononi katika kupata huduma za
kifedha. Hadi mwezi Mei mwaka 2010, kulikuwa na zaidi ya watumiaji milioni 6 wa
huduma hizi. Baadhi ya huduma zinazopatikana ni pamoja na kutuma fedha kwa
ndugu na jamaa, kulipa ankara za maji (DAWASCO), umeme (LUKU), bima, na
kulipa madeni. Changamoto kuu kwa sasa ni juu ya suala la usimamizi kwani
makampuni ya simu yanayotoa huduma hizi yanasimamiwa na chombo (TCRA)
ambacho hakihusiki na masuala ya kifedha bali ya mawasiliano. Hata hivyo, Benki
Kuu inakamilisha mazungumzo na TRCA kuiwezesha kushiriki katika kusimamia
masuala ya huduma za kifedha zinazofanywa na makampuni ya simu.
9
Sekta ya Nje
15. Katika mwaka 2010 thamani ya mauzo ya bidhaa na huduma nje iliongezeka
kwa asilimia 21.9 kutoka Dola za Kimarekani milioni 4,780.4 mwaka 2009 hadi Dola
za Kimarekani milioni 5,828.2. Hii ilichangiwa na kuongezeka kwa thamani ya mauzo
ya bidhaa zisizo asilia ambayo iliongezeka kwa asilimia 33.7 na mapato ya huduma
(asilimia 12.8). Kwa upande mwingine, thamani ya bidhaa na huduma zilizoagizwa
toka nje mwaka 2010 ziliongezeka kwa asilimia 18.8 kufikia Dola za Kimarekani
milioni 8,974.7 kutoka Dola za Kimarekani milioni 7,543.2 mwaka 2009. Hii ilitokana
na kuongezeka kwa uagizaji wa bidhaa hususan zitakazowezesha kuongeza
uzalishaji.
Ushirikiano wa Kiuchumi wa Kikanda
16. Katika kuongeza juhudi za kuimarisha mtangamano wa Jumuiya ya Afrika
Mashariki (EAC) nchi wanachama wa Jumuiya zimeridhia uanzishwaji wa, na
zimeanza utekelezaji wa Umoja wa Forodha na Soko la Pamoja la Jumuiya ya Afrika
Mashariki. Kuhusu Jumuiya ya Uchumi Kusini Mwa Afrika (SADC), nchi wanachama
zinaendelea na jitihada za kuimarisha utekelezaji wa makubaliano ya “Eneo Huru la
Biashara: (Free Trade Area) ili ifikapo mwaka 2012 nchi zote ziwe zimeingia katika
makubaliano na ushuru kwa bidhaa nyingi ufikie sifuri. Hadi sasa nchi za Demokrasia
ya Kongo, Angola na Seychelles hazijarithia mpango huo wa eneo huru la biashara.
Kufuatia hatua zilizochukuliwa za kuimarisha biashara miongoni mwa nchi
wanachama, biashara kati ya Tanzania na nchi hizi za Jumuiya ya Afrika Mashariki
na Jumuiya ya Uchumi Kusini Mwa Afrika iliendelea kukua ambapo mauzo ya bidhaa
za Tanzania katika nchi hizi kwa pamoja yaliongezeka kwa Dola milioni 437.1
mwaka 2010, sawa na asilimia 68.5 wakati ambapo uagizaji wa bidhaa uliongezeka
kwa Dola milioni 69.2 sawa na asilimia 6.6.
Uendelezaji wa Sekta Binafsi
17. Katika mwaka 2010, Serikali iliendelea kuchukua hatua za makusudi katika
kuimarisha na kuendeleza sekta binafsi. Mwezi Agosti 2010, Bunge lilipitisha sheria
10
ya Ubia Kati ya Sekta ya Umma na Binafsi - PPP No. 19 ya mwaka 2010. Vitengo
vya PPP tayari vimeshanzishwa katika Wizara ya Fedha na Ofisi ya Waziri Mkuu ili
kuratibu masuala yanayohusiana na PPP. Kupitia vitengo hivyo, Serikali inaandaa
mkakati na mwongozo wa utekelezaji wa sheria ya PPP, hususan katika miradi
mikubwa ya miundombinu. Serikali inakamilisha maandalizi ya kanuni
zitakazoongoza utekelezaji wa Sheria ya PPP.
Tathmini ya Dira na Mpango wa Maendeleo wa Muda wa Kati na Mrefu
18. Tathmini ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 ilibainisha
kwamba dhana ya Dira ya Taifa ya Maendeleo bado ni sahihi na inatekelezeka iwapo
kutaongezwa msukumo katika utekelezaji. Aidha, tathmini ilibainisha haja ya kuwa
na mfumo linganishi wa utayarishaji na utekelezaji wa mipango ya muda wa kati na
mrefu. Serikali iko katika mchakato wa kuandaa Mpango wa Muda Mrefu ambao
utekelezaji wake utafanyika kuanzia mwaka 2011/12 kwa vipindi vya muda wa kati
wa miaka mitano mitano hadi 2025. Mchakato huu ambao bado unaendelea ulianza
kwa kupitia mifumo ya mipango iliyoko na kuangalia namna bora ya kuioanisha.
Utekelezaji wa mpango huu unakusudia kwanza kufungua fursa za kijiografia tulizo
nazo ili tuweze kufaidika na soko la nchi za Jumuiya ya Africa Mashariki, SADC na
Maziwa Makuu na kuweza kuhudumia nchi majirani zisizokuwa na bahari. Aidha,
Mpango unakusudia kuhakikisha tunafaidika na rasilimali asili tulizonazo kama vile
ardhi yenye rutuba, madini, vivutio vya kitalii, n.k.
MKUKUTA na Malengo ya Maendeleo ya Milenia (MDGs)
19. Utekelezaji wa awamu ya kwanza ya MKUKUTA ulifikia kikomo Juni 2010.
Mafanikio kadhaa yalipatikana kutokana na utekelezaji wake, kama vile ukuaji wa
uchumi, ongezeko katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, usimamizi thabiti wa fedha
za umma, uimarishaji wa barabara vijijini, pamoja na uboreshaji wa sekta za elimu,
afya na maji. Hata hivyo, zipo changamoto zilizojitokeza ikiwa ni pamoja na kasi
ndogo ya kupungua kwa kiwango cha umaskini, upatikanaji na ubora wa huduma
kwa viwango vilivyokusudiwa, ushiriki mdogo wa sekta binafsi, na ufinyu wa bajeti.
Changamoto nyingine zilikuwa nje ya uwezo wa Serikali, zikiwemo ukame
uliojitokeza nchini mwaka 2006 na kuyumba kwa uchumi wa dunia kulikoanza
11
mwishoni mwa mwaka 2008. Pamoja na ufinyu wa bajeti, Serikali ilikuwa ikiongeza
mwaka hadi mwaka kiasi cha fedha kinachoenda katika utekelezaji wa MKUKUTA
kutoka asilimia 54.1 ya bajeti yote mwaka 2005/06 wakati MKUKUTA ulipoanza hadi
asimia 71.2 mwaka 2009/10. Katika kuongeza juhudi za kuondoa umaskini na
kukuza uchumi, Serikali iliridhia uanzishwaji wa awamu ya pili ya MKUKUTA mwezi
Oktoba 2010. Mchakato wa uandaaji wa awamu hii ya pili uliwashirikisha wadau
wengi na ulizingatia zaidi mikakati ya kukabiliana na changamoto zilizojitokeza katika
utekelzaji wa awamu ya kwanza ya MKUKUTA.
20. Mapitio ya utekelezaji wa Malengo ya Milenia, yanaonesha kuwa Tanzania
inafanya vizuri katika baadhi ya viashiria kama vile vya elimu ya msingi na usawa wa
jinsia. Hata hivyo, changamoto bado zipo katika viashiria vingine vya umaskini
kama vile afya ya uzazi wa mama na kupunguza vifo vya watoto. Hivyo, kipaumbele
sasa kimewekwa katika kuongeza ufanisi katika maeneo hayo ya changamoto na
kuimarisha zaidi utekelezaji pale ambapo Tanzania imepata mafanikio kiasi. Hata
hivyo, kuna haja ya kuchambua viashiria hivi kwa umakini zaidi kwani kuna baadhi
ambavyo vimepitwa na wakati. Mfano, MDG inasisitiza zaidi juu ya uandikishaji
katika elimu ya msingi na kusahau masuala ya msingi ya ubora wa elimu. Vile vile
viashiria vingine havina namna ya kuvipima mfano vinavyohusiana na masuala ya
mazingira.
Utafiti wa Afya na Demografía 2010-TDHS
21. Kulingana na ripoti ya Utafiti wa Afya na Demografía (Tanzania Demographic
and Health Survey – (TDHS) ya mwaka 2010, kiwango cha udumavu wa watoto
walio chini ya miaka mitano kilipungua kutoka asilimia 37.7 mwaka 2004/05 hadi
asilimia 35.4 mwaka 2010; upungufu wa uzito kwa watoto walio chini ya miaka
mitano ulipungua kutoka asilimia 22 mwaka 2004/05 hadi asilimia 21 mwaka 2010;
na hali ya ukondefu iliongezeka kutoka asilimia 3 mwaka 2004/05 hadi asilimia 4
mwaka 2010. Aidha, watoto walio chini ya umri wa miaka mitano wenye uzito
uliozidi au kiribatumbo walikuwa asilimia 5 . Hali kadhalika kwa mujibu wa ripoti
hiyo, vifo vya watoto wenye umri chini ya miaka mitano vimepungua kutoka watoto
12
112 kwa kila watoto 1,000 wanaozaliwa hai mwaka 2007 hadi watoto 81 mwaka
2010 na vile vya watoto wachanga vimepungua kutoka watoto 68 hadi watoto 51
kwa kila watoto 1,000 wanaozaliwa hai mwaka 2010. Vile vile, kiwango cha jumla
cha uzazi (total fertility rate) kimepungua kutoka wastani wa watoto 6.3 mwaka
1991/92 kwa mwanamke mmoja hadi wastani wa watoto 5.4 kwa mwanamke
mmoja. Kiwango hiki kwa sasa ni kikubwa kwa maeneo ya vijijini (6.1)
ikilinganyishwa na maeneo ya mijini (3.7). Pamoja na viashiria hivi vya afya
kuonesha mwenendo mzuri, bado kuna haja ya kuongeza mikakati ya kuboresha
zaidi huduma za afya hasa katika maeneo ya vijijini.
MASUALA MUHIMU YA KISERA YALIYOJITOKEZA MWAKA 2010/11
22. Mwaka 2010, uchumi wa dunia ulianza kuimarika na kurudi katika hali yake ya
kawaida baada ya kuyumba katika mwaka 2008/09 kufuatia kuzorota kwa masoko
ya fedha na mitaji katika masoko ya Ulaya na Marekani. Uchumi wa Tanzania nao
ulianza kuimarika siyo tu kwa sababu ya kuimarika kwa uchumi wa dunia bali pia
kutokana na mpango wa Serikali wa kuunusuru uchumi, pamoja na hatua
zilizochukuliwa na serikali katika kuongeza ruzuku ya pembejeo za kilimo na
utekelezaji wa ASDP kulikoenda sambamba na kuwepo kwa hali nzuri ya hewa . Hata
hivyo, katika nusu ya pili ya mwaka 2010/11, matatizo ya ukame yalianza kuikumba
nchi yetu ambapo sekta mbalimbali ziliathirika moja kwa moja kama vile kilimo na
nishati ambazo hutegemea zaidi mvua. Kufuatia hali hiyo ya ukame, Serikali
ililazimika kuanza mgao wa umeme mwishoni mwa mwaka 2010 kutokana na
kupungua kwa kina cha maji katika mabwawa ya kuzalishia umeme. Mgao huu
uliathiri sekta nyingine zinazotegemea umeme kama vile viwanda na hivyo kuna
hatari ya kutofikia malengo tuliyojiwekea na itapelekea pia kudumaza jitihada za
kufikia malengo ya Dira ya Maendeleo 2025 na MDG. Hali kadhalika, kuongezeka
kwa bei za mafuta katika soko la dunia ambako kunachochewa pia na machafuko ya
kisiasa katika nchi za kiarabu kunaweza kuathiri pia ukuaji wa uchumi wetu.
Kutokana na hali hii, ni dhahiri kuwa pana haja ya kuongeza kasi ya ukuaji uchumi.
13
23. Masuala mengine ya kisera yaliyojitokeza mwaka 2010 ni pamoja na
utekelezaji wa MKUKUTA II ambao ulipitishwa rasmi mwezi Oktoba 2010, maandalizi
ya mpango wa “SAGCOT”, maendeleo ya rasilimali watu na maandalizi ya Mpango
wa Maendeleo wa Miaka Mitano.Utekelezaji wa Mradi wa Ukanda wa Kilimo wa
Kusini mwa Tanzania (Southern Agricultural Growth Corridor of Tanzania_ SAGCOT)
ambao ni sehemu ya Kilimo Kwanza utasaidia kupunguza umaskini miongoni mwa
wananchi wanaoishi vijijini kwa kuwaongezea mavuno ya mazao yao na kukuza ajira
miongoni mwa watanzania. SAGCOT ni mpango mkakati wa kuleta mapinduzi ya
kilimo unaotekelezwa kwa pamoja kati ya serikali na kwa kushirikiana na wadau
mbalimbali wa kilimo yakiwemo mashirika ya kimataifa.
Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/12 – 2015/16)
24. Mchakato wa kuandaa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/12 –
2015/16) unaendelea kufanyika na kwa sasa uko katika ngazi za maamuzi, chini ya
uongozi na usimamizi wa Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango. Mpango huu ni awamu ya
kwanza ya mpango elekezi (roadmap) wa miaka 15 wa kutekeleza Dira ya Taifa ya
Maendeleo 2025 kwa utaratibu maalum (systematically) ukiwa na viashiria vya
kupima mafanikio ya utekelezaji. Mpango wa Miaka Mitano unajengwa juu ya na
unazingatia malengo ya MKUKUTA II na pia unajumuisha malengo mapana zaidi.
Dhana ya Mpango huu ni kufungulia fursa za ukuaji wa uchumi wa Taifa na
unalenga kabadili mtazamo wa kupanga maendeleo ya Taifa kutoka kupanga
kulingana na rasilimali zilizopo pekee kwenda kwenye kupanga ili kutumia kikamilifu
fursa zinazojitokeza. Mpango pia umebainisha nguzo kuu nne ambazo zitakuwa
vipaumbele vya kitaifa na utekelezaji wake utasaidia kufikia malengo ya Dira. Nguzo
hizo ni kama zifuatazo:
I. Kuendeleza Utengamavu wa Uchumi Jumla: Katika nguzo hii, Serikali
itaimarisha viashiria vya uchumi jumla kwa kuimarisha sera ya mapato na
matumizi ya Serikali, kudhibiti mfumuko wa bei, kuweka viwango sahihi vya
ujazi wa fedha vinavyowiana na kasi ya ukuaji wa Pato la Taifa na upandaji
wa bei, kuimarisha usimamizi wa mabenki na mfumo wa malipo nchini. Vile
vile utawala bora utaimarishwa katika sekta zote ili kuongeza kasi ya ukuaji
14
wa uchumi katika ngazi zote. Sambamba na hili, Serikali itaendeleza
mafanikio yaliyopatikana katika huduma za jamii na msukumo utakuwa katika
kuongeza ubora wa elimu, huduma za afya, maji na ustawi wa jamii katika
ngazi zote;
II. Kutumia fursa za rasilimali zilizopo katika kukuza uchumi: Eneo la
msisitizo hapa ni kufanya mapinduzi ya kijani ili Tanzania ijitosheleze kwa
chakula na kuuza ziada nje.;
III. Kutumia Fursa za Kijiografia: Mwelekeo wa Mpango ni kutumia kimkakati
fursa ya kupakana na bahari ya Hindi na Maziwa pamoja na nchi zisizokuwa
na bahari inayoifanya Tanzania kuwa lango kuu la biashara na usafirishaji
katika nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu. Hivyo, msukumo utaelekezwa katika
kuboresha (kukarabati na kujenga) miundombinu ya bandari, reli, nishati,
barabara na mkongo wa Taifa pamoja na kuongeza ufanisi katika utoaji wa
huduma hizo na zile za Mamlaka ya Mapato; na
IV. Kuboresha na kukuza matumizi ya TEKNOHAMA: Katika kipindi hiki cha
Mpango, msukumo utawekwa katika kuboresha teknolojia ili kusaidia katika
kuongeza thamani na tija hususan katika viwanda, madini, usindikaji wa
mazao ya kilimo na matumizi ya TEKNOHAMA katika kuboresha huduma kama
vile ‘e_Government”. Maeneo mengine yatakayopewa msisitizo ni katika
kuongeza kiwango na ubora wa elimu hasa ya sayansi, na ufundi stadi.
Vipaumbele Vya Kisekta
25. Serikali imebainisha maeneo ya kipaumbele ya Kitaifa yatakayotekelezwa
katika kipindi cha muda wa kati. Lengo ni kuwekeza katika shughuli za kiuchumi na
kijamii zenye kuchochea ukuaji endelevu wa uchumi kwa upana zaidi na kupunguza
umaskini. Aidha, pamoja na maeneo yaliyobainishwa kama vipaumbele, maeneo ya
kimkakati yatakayozingatiwa kwa mwaka wa mpito wa 2011/12 ni umeme, bandari,
reli, maji na chakula cha hifadhi. Kila sekta itahakikisha kuwa inaweka msukumo
15
katika matumizi endelevu ya maliasili zilizopo kama vile ardhi, maji, madini, gesi
asilia, wanyama pori, mazao ya misitu na vivutio vya utalii ili kuchangia katika ukuaji
wa uchumi. Maeneo yaliyobainishwa na sekta husika kama vipaumbele vya muda wa
kati ni kama ifuatavyo:
I. Elimu
a. Kuinua ubora wa elimu katika ngazi zote ikiwemo ufundishaji na ujifunzaji
kwa njia ya TEKNOHAMA;
b. Kuboresha sera ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi pamoja na mikakati ya
utekelezaji, ikiwemo kutoa elimu inayoimarisha ujuzi wa wahitimu; na
c. Kuimarisha ugharamiaji wa elimu ya juu.
II. Kilimo, Mifugo na Uvuvi
a. Kuendeleza na kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji na ujenzi wa
mabwawa kwa ajili ya upatikanaji wa maji ya mifugo na umwagiliaji;
b. Kuhakikisha upatikanaji wa pembejeo na zana za kilimo, mifugo na uvuvi;
c. Kuboresha huduma za ugani;
d. Kuiwezesha sekta binafsi kuwekeza katika kilimo, mifugo na uvuvi; na
e. Kuboresha upatikanaji wa masoko na usindikaji wa mazao ya kilimo,
mifugo na uvuvi.
III. Nishati
a. Kuongeza uzalishaji wa umeme kwa kutumia vyanzo mbalimbali;
b. Kupanua na kuimarisha miundombinu ya uzalishaji, usafirishaji na
usambazaji wa nishati ya umeme, sawia na kuongeza uhakika wa
upatikanaji na unafuu wa bei yake;
c. Kuendeleza utafiti wa upatikanaji na utumiaji wa umeme wa gesi asilia na
mafuta; na
d. Kupanua miundombinu ya gesi asilia.
16
IV. Uendelezaji wa Miundombinu na Usafirishaji
a. Ujenzi na ukarabati wa barabara, madaraja na vivuko na kupunguza
msongamano wa magari mijini;
b. Kuanzisha mfuko wa ujenzi wa barabara (Road Development Fund) na
kupanua wigo wa mfuko wa matengenezo ya barabara;
c. Ujenzi na ukarabati wa majengo/nyumba za Serikali;
d. Ukarabati na ujenzi wa reli pamoja na viwanja vya ndege;
e. Uimarishaji wa huduma za hali ya hewa;
f. Ujenzi na ukarabati wa bandari pamoja na utengenezaji wa meli katika
maziwa: na
g. Kujenga uwezo wa kufanyia ukarabati mitambo, magari na vifaa vingine
vya Serikali.
V. Maendeleo ya Viwanda
a. Kuendelea kuboresha mazingira ya viwanda, biashara na kuvutia
uwekezaji nchini;
b. Kukuza teknolojia sahihi kwa wajasiriamali wadogo na wa kati katika
kuongeza thamani ya bidhaa hususan usindikaji wa bidhaa za kilimo;
c. kuendeleza Kanda maalumu za uzalishaji kwa ajili ya kuuza nje kwa
kushirikisha sekta ya umma na sekta binafsi; na
d. Kuendeleza viwanda vya msingi na kuvipa kipaumbele viwanda
vinavyotumia malighafi inayopatikana nchini.
VI. Afya
a. Kuimarisha huduma za tiba, kinga na utengamavu wa afya katika ngazi
zote;
b. Kujenga na kukarabati vituo vya kutolea huduma za afya; na
c. Kuajiri madaktari wote wanaohitimu katika vyuo mbalimbali.
VII. Maji
a. Kuendeleza program ya maji na usafi wa mazingira vijijini;
17
b. Kutekeleza program maalumu ya maji safi na maji taka katika jiji la Dar es
Salaam;
c. Kutekeleza miradi inayoendelea kwa kuongeza upatikanaji wa maji safi na
salama; na
d. Kuimarisha usimamizi na uendelezaji wa rasilimali za maji.
VIII. Ardhi
a. Kuboresha upatikanaji wa nyumba za gharama nafuu katika maeneo ya
mijini na vijijini na kuboresha uelewa wa wananchi kuhusu huduma za
mikopo ya nyumba;
b. Kuanzisha kituo cha kitaifa cha kupokea picha za anga ili kurahisisha
upimaji wa ardhi na utayarishaji wa ramani;
c. Kuimarisha na kupanua mfumo wa kisasa wa utunzaji wa kumbukumbu za
ardhi ili kuboresha usimamizi wa ardhi na kurahisisha mfumo wa Taifa wa
anuani za makazi;
d. Kutekeleza Mpango wa taifa wa matumizi ya ardhi; na
e. Utayarishaji wa mipango miji kukabiliana na changamoto za ukuaji wa
miji.
IX. Maendeleo ya Raslimali watu
a. Kuimarisha ujuzi na utaalamu unaokidhi mahitaji ya soko kwa kuzingatia
sekta ya umma, sekta binafsi na masoko ya kikanda;
b. Kujenga uwezo wa sekta mbalimbali kuandaa mipango thabiti ya raslimali
watu na kuchambua mahitaji ya ujuzi katika sekta husika;
c. Kuimarisha uwajibikaji na uadilifu katika utendaji kazi;
d. Kukamilisha mradi wa vitambulisho vya Taifa; na
e. Kuwashirikisha watanzania wafanyao kazi nje ya nchi (diáspora) ili waweze
kushiriki na kuchangia katika uchumi.
X. Sayansi na Teknolojia
a. Kuendeleza miundombinu na huduma za TEKNOHAMA nchini ikiwa ni
pamoja na kukamilisha ujenzi wa mkongo wa Taifa;
18
b. Kuboresha na kujenga taasisi za Sayansi, Teknolojia na Ubunifu
zinazojumuisha mafunzo ya ufundi stadi, (ikiwemo Taasisi ya sayansi na
Teknologia ya Nelson Mandela) vituo mahiri vya utafiti wa kisayansi na
viatamizi; na
c. Kuimarisha utafiti na maendeleo (R&D) na kutumia matokeo yake
kibiashara.
XI. Mtangamano wa Kikanda
a. Kuendeleza uwezo na ujuzi unaohitajika ili kuiwezesha Tanzania kutumia
kikamilifu fursa zilizopo na zinazojitokeza katika mtangamano wa kikanda;
b. Uendelezaji wa miundombinu ya kikanda inayojumuisha sekta za
barabara, reli bandari, TEKNOHAMA na nishati;
c. Kukamilisha Mkakati wa Utekelezaji wa Soko Huru la Pamoja; na
d. Kukamilisha mkakati wa utekelezaji wa habari, mawasiliano na ufahamu
unaolenga kuwafikia wadau wengi zaidi.
XII. Mamlaka ya Serikali za Mitaa
a. Kuendelea kutekeleza sera ya kupeleka madaraka mikoani (D by D);
b. Kujenga na kukarabati miradi ya miundombinu na kutoa vivutio
vitakavyowashawishi wataalamu kubaki na kuendelea kutoa huduma
katika Serikali za mitaa hasa maeneo ya pembezoni;
c. Kupanua wigo na kuimarisha usimamizi wa kodi;
d. Kuboresha mfumo wa usimamizi wa fedha za umma na uwajibikaji katika
ngazi zote;
e. Kujenga ofisi za makao makuu ya mikoa, halmashauri na wilaya mpya; na
f. Kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji, tathmini na utoaji wa taarifa kwa wakati;
XIII. Sekta ya Fedha
a. Kuongeza mtaji wa Banki ya Rasilimali Tanzania na Benki ya Wanawake;
b. Kuanzisha Benki ya Maendeleo ya Kilimo;
19
c. Kuongeza na kuimarisha huduma za kifedha pamoja na uelewa wa
masuala ya kifedha (financial education) kwa wakopaji na wakopeshaji
hasa katika maeneo ya vijijini;
d. Kuanzisha chombo cha kutoa taarifa za masuala ya mikopo (Credit
Reference Bureau/Databank); na
e. Kukuza ufanisi na kuongeza ushindani katika mifuko ya hifadhi ya jamii;
MISINGI NA MALENGO YA UCHUMI JUMLA NA MAENDELEO YA JAMII
2011/12-2015/16
26. Malengo ya sera za uchumi jumla katika kipindi cha mwaka 2011/12 –
2015/16 yatakuwa yafuatayo:
(i) Pato halisi la Taifa litakua kwa asilimia 6.8 mwaka 2011, asilimia 7.5
mwaka 2012, na kuendelea kuongezeka hadi asilimia 8.5 mwaka 2015;
(ii) Kuendelea kudhibiti kasi ya upandaji bei ili ibaki kwenye viwango vya
tarakimu moja;
(iii) Kuongezeka kwa mapato ya ndani yatakayofikia uwiano na Pato la
Taifa kwa asilimia 17.2 ya Pato la Taifa mwaka 2011/12 na kuendelea
kuongezeka kwa wastani wa asilimia 17.5 karika kipindi cha muda wa
kati;
(iv) Kudhibiti ongezeko la ujazi wa fedha kwa tafsiri pana zaidi unatarajiwa
kukua kwa asilimia 19.0 mwaka 2011/12; asilimia 18.6 mwaka 2012/13
na asilimia 18.1 mwaka 2013/14. Ukuaji huu unalenga kuwiana na
malengo ya ukuaji wa uchumi, na kasi ya upandaji bei;
(v) Kuwa na akiba ya fedha za kigeni itakayoweza kukidhi mahitaji ya
uagizaji wa bidhaa na huduma toka nje kwa kipindi kisichopungua
miezi 4.6;
(vi) Kupunguza tofauti ya viwango vya riba; na
(vii) Kuwa na kiwango imara cha ubadilishaji wa fedha kitakachotokana na
mwenendo wa soko la fedha.
20
27. Malengo tuliyokusudia ya Sera za uchumi jumla katika kipindi cha muda wa
kati (2011/12-2015/16) yatafanikiwa kwa kuzingatia misingi ifuatayo:-
(i) Kuendelea kuimarika kwa amani, utulivu na utengamano;
(ii) Vyanzo vya maji vitaendelea kuhifadhiwa na kukidhi mahitaji;
(iii) Kuendelea kuimarika kwa utengamavu wa viashiria vya uchumi jumla
na maendeleo ya jamii;
(iv) Kuongezeka na kuboresha mapato ya ndani ikiwa ni pamoja na kubuni
vyanzo vipya vya kodi, kuimarisha ukusanyaji wa kodi ya majengo, na
kupunguza misamaha ya kodi ili kuweza kugharamia vipaumbele
vilivyoainishwa;
(v) Kuimarisha usimamizi katika matumizi ya fedha za umma;
(vi) Rasilimali zitaelekezwa kwenye maeneo yanayochochea ukuaji wa
uchumi kwa haraka zaidi kama yalivyoainishwa hapo juu na katika
Mwongozo wa Mpango na Bajeti wa mwaka 2011/12 – 2015/16;
(vii) Kutekelezwa kwa MKUKUTA II kama ilivyopangwa;
(viii) SAGCOT na Nguzo 10 za Kilimo Kwanza zitatekelezwa kama
ilivyopangwa;
(ix) Kuendeleza ushirikishwaji wa sekta binafsi na kuboresha mazingira ya
biashara; na
(x) Kuimarika kwa sera ya fedha (monetary policy) ili iendane na sera za
bajeti (fiscal policies) zitakazosaidia kupunguza mfumuko wa bei na
tofauti ya riba za kukopa na amana, na kuongeza mikopo kwa sekta
binafsi;
HITIMISHO
Dhamira kuu ya Serikali ni kuhakikisha kuwa yote yaliyosemwa hapo juu
yatatekelezwa kwa ushirikiano wa karibu na asasi zisizo za kiserikali ikijumuisha
sekta binafsi na washirika wa maendeleo ili kufikia malengo ya millenia, Dira na ya
MKUKUTA II. Kama kila mmoja atatekeleza wajibu wake, inawezekana kabisa kufikia
malengo yetu ya muda mfupi, kati na mrefu tuliyojiwekea kama yalivyoainishwa
katika Mpango wa Maendeleo wa Muda wa Kati.