Hotuba Final[1]

Embed Size (px)

Citation preview

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    1/24

    1

    HOTUBA YA MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE,

    RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA,

    KWA WANANCHI, TAREHE 31 MACHI, 2013

    Ndugu Wananchi;

    Naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu

    kwa kutujaalia uhai na kunipa fursa ya kuzungumza

    nanyi kwa kupitia utaratibu wetu huu mzuri wa kila

    mwisho wa mwezi. Leo ninayo mambo matatu

    ninayopenda kuzungumza nanyi.

    Ziara ya Rais wa China Nchini Tanzania

    Ndugu wananchi;

    Jambo la kwanza ni ziara ya Mheshimiwa Xi Jinping,

    Rais wa Jamhuri ya Watu wa China aliyoifanya nchini

    kwetu kati ya tarehe 24 na 25 Machi, 2013. Lengo la

    ziara yake ilikuwa kuimarisha uhusiano wa kihistoria

    uliopo kati ya China na Tanzania. Napenda kuchukua

    nafasi hii kuwashukuru wakazi wa Dar es Salaam kwa

    kumpokea vizuri mgeni wetu na ujumbe wake.

    Wameondoka wakiwa na kumbukumbu nzuri ya nchi

    yetu na watu wake.

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    2/24

    2

    Kwa niaba yenu, nimepokea salamu za shukrani

    kutoka kwa Rais Xi Jinping akielezea kufurahishwa na

    mapokezi mazuri tuliyowapatia. Naomba tuendelee

    kuonesha moyo wa upendo na ukarimu kwa wageni

    wetu wengine mashuhuri watakaotutembelea siku za

    usoni.

    Ndugu wananchi;

    Nami pia, nimemshukuru sana Mheshimiwa XiJinping kwa kukubali mwaliko wangu na kufanya ziara

    ya kihistoria na yenye mafanikio makubwa kwa nchi

    yetu. Ameifanyia nchi yetu jambo la heshima kubwa na

    kumbukumbu isiyosahaulika. Tanzania imekuwa nchi

    ya kwanza Barani Afrika kuitembelea, tena siku kumi tu

    baada ya kuchaguliwa kuwa Rais wa nchi yake. Na,

    kubwa zaidi ni kutumia fursa ya ziara yake hapa nchini

    kutangazia dunia Sera ya China kwa Afrika katika

    kipindi cha uongozi wake.

    Tumefarijika sana kusikia kuwa uhusiano na Afrika

    bado unapewa kipaumbele cha juu na viongozi wapya

    wa China. Pia, kuwa China itaendelea kukuza biashara

    na uwekezaji na kuongeza misaada ya maendeleo kwa

    Afrika ikiwemo kutoa nafasi 18,000 za mafunzo kwa

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    3/24

    3

    vijana wa Kiafrika. Kama mtakumbuka nchi zetu mbili

    zilitiliana saini mikataka 16 ya ushirikiano katika nyanja

    mbalimbali. Misaada ya maendekeo kwa maeneo yetu

    ya kipaumbele nayo imejumuishwa.

    Ndugu Wananchi;

    Rais Xi Jinping alielezea na kusisitiza dhamira yake

    na ya Serikali na Chama cha Kikomunisti cha China ya

    kudumisha na kukuza uhusiano mzuri uliopo kati yaTanzania na China. Kama mjuavyo uhusiano huo

    ulianzishwa mwaka 1964 na waasisi wa nchi zetu, yaani

    Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyekuwa Rais wa

    kwanza wa Tanzania na Mwenyekiti Mao Zedong

    aliyekuwa Kiongozi Mkuu wa China na Waziri Mkuu

    wake Chou En Lai.

    Rais wa China aliahidi kuwa nchi yake itaendelea

    kushirikiana na Tanzania katika medani ya kimataifa na

    kuchangia katika jitihada zetu za kujiletea maendeleo

    kwa kuongeza misaada ya maendeleo. Katika miaka

    49 ya uhusiano na ushirikiano na China nchi yetu

    imepata misaada mingi ya maendeleo ikiwemo Ukumbi

    wa Kimataifa wa Mikutano wa Mwalimu Nyerere ambao

    ulizinduliwa na Rais Xi Jinping wakati wa ziara yake.

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    4/24

    4

    Ndugu wananchi;

    Kuna miradi kadhaa mikubwa inayoendelea

    kutekelezwa nchini, Bara na Zanzibar, kwa msaada waSerikali ya China. Wakati wa ziara yake, Rais Xi Jinping

    iliahidi kuendelea kutusaidia miradi mingine ya

    maendeleo kama tulivyoomba wakati wa mazungumzo

    yetu licha ya ile ambayo ilitiwa saini siku ile.

    Ajali ya Kuporomoka Jengo la GhorofaJijini Dar es Salaam

    Ndugu Wananchi;

    Jambo la pili ninalotaka kuzungumzia ni ajali ya

    kuporomoka kwa jengo la ghorofa 16 lililokuwa

    linajengwa katika jiji la Dar es Salaam. Ajali hiyo

    iliyotokea juzi tarehe 29 Machi, 2013 imeleta msiba na

    simanzi kubwa nchini. Mpaka sasa maiti za ndugu zetu

    30 zimepatikana. Watu 17 waliweza kuokolewa,

    wanne kati yao bado wanaendelea na matibabu katika

    Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Wengine walitibiwa na

    kuruhusiwa. Kazi ya kufukua eneo la ajali inaendelea

    na sasa inakaribia kufikia ukingoni.

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    5/24

    5

    Ndugu Wananchi;

    Mimi na viongozi wenzangu tulipata nafasi ya

    kwenda kuangalia eneo la ajali. Hali niliyoiona paleimenihuzunisha sana. Lazima nikiri, hata hivyo,

    kwamba nimeridhishwa sana na juhudi kubwa za

    uokoaji zilizokuwa zinafanywa na wanajeshi wetu

    wakishirikiana na taasisi, mashirika binafsi na

    wananchi. Napenda kutumia nafasi kutoa shukrani

    maalum kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Ndugu

    Saidi Meck Sadick kwa uongozi wake madhubuti. Pia

    nampongeza Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Ndugu Raymond

    Mushi, na Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es

    Salaam, Ndugu Suleiman Kova pamoja na Maafisa na

    askari wa JWTZ, na wale wote walioshiriki na

    wanaoendelea kushiriki katika juhudi za uokoaji.

    Nawapongeza pia madaktari na wauguzi wa

    Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na hospitali nyinginezo

    kwa jitihada zao za kuokoa maisha ya waliojeruhiwa.

    Nawapa pole wale wote waliofiwa na wapendwa, ndugu

    na jamaa zao katika ajali hii. Nawaomba wawe na

    moyo wa subira huku sote tukiungana nao kuwaombea

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    6/24

    6

    marehemu wetu wapate mapumziko mema peponi.

    Kwa waliojeruhiwa, tunawaombea wapone upesi.

    Ndugu Wananchi;

    Maneno mengi yanasemwa kuhusu chanzo cha

    ajali ile. Alimradi kila mtu ana dhana yake. Niliagiza

    vyombo na mamlaka husika wachukue hatua zipasazo

    kuchunguza sababu za ghorofa hilo kuanguka na

    watakaothibitika kusababisha maafa hayowachukuliwe hatua zipasazo. Wa kushtakiwa

    Mahakamani washitakiwe na wa kufutiwa leseni za

    kufanya shughuli za ujenzi au taaluma zao wafutiwe

    bila ajizi. Jambo la msingi la kusisitiza ni kuwa

    mamlaka zinazohusika na usimamizi wa ujenzi lazima

    zitimize ipasavyo wajibu wake. Naamini kama

    mamlaka hizo zingetimiza ipasavyo wajibu wake ajali

    hii ingeepukika. Halmashauri za miji na wilaya zina

    wajibu maalum kwenye ujenzi katika maeneo yao.

    Watimize wajibu wao. Yaliyotokea Dar es Salaam yawe

    fundisho kwa wote.

    Ndugu Wananchi;

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    7/24

    7

    Ni matumaini yangu kuwa Bodi ya Usajili wa

    Wakandarasi na Bodi ya Usajili wa Wahandisi

    itakamilisha mapema uchunguzi wake ili ukweli

    ujulikane. Bodi ya Usajili wa Wasanifu Majengo na

    Wakadiriaji Majenzi na Baraza la Taifa la Ujenzi nao

    washirikishwe kwa ukamilifu ili ukweli upatikane na

    hatua stahiki zichukuliwe. Pia naomba washauri namna

    bora ya kukomesha ajali za aina hiyo siku za usoni.

    Uhusiano wa Wakristo na Waislamu

    Ndugu Wananchi;

    Jambo la tatu ninalopenda kuzungumza nanyi leo

    ni uhusiano wa Waislamu na Wakristo nchini. Jambo

    hili nimeshalizungumzia mara kadhaa siku za nyuma,

    lakini nalazimika kulisemea tena kutokana na hali ilivyo

    sasa. Tumefikia mahali ambapo kama viongozi na

    waumini wa dini hizi kubwa mbili hawatakubali kubadili

    muelekeo wa sasa, tunakoelekea ni kubaya. Nchi yetu

    nzuri tutaivuruga na sifa yake ya miaka mingi ya

    Waislamu na Wakristo kuishi pamoja kidugu, kwa

    upendo, ushirikiano na kuvumiliana itatoweka.

    Tanzania itaacha kuwa kisiwa cha amani na kuingia

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    8/24

    8

    katika orodha ya nchi zenye migogoro na hata vita vya

    wenyewe kwa wenyewe.

    Ndugu Wananchi;

    Nyaraka na kauli kali kali zinazotolewa na viongozi

    wa dini za Kikristo na Kiislamu zinanishawishi kuamini

    haya niyasemayo. Nyaraka na kauli hizo zina mambo

    mawili makuu. Kwanza, kwamba kila upande

    unatuhumu, kushutumu na kulaumu upande mwinginekwa kufanya vitendo viovu dhidi ya dini yake. Kauli na

    mihadhara ya kudhalilisha dini za wengine, kunajisi

    vitabu vitakatifu, kuchoma moto nyumba za ibada,

    mzozo kuhusu nani achinje na kuuawa kwa viongozi wa

    dini ni baadhi ya mambo yanayotolewa mifano.

    Na, pili kwamba kila upande unailamu Serikali kwa

    kupendelea upande mwingine. Wakristo wanalaumu

    kwamba mihadhara ya kudhalilisha Ukristo

    inaendeshwa na Serikali haichukui hatua. Aidha,

    Wakristo wanateswa na viongozi wao kuuawa na

    Waislamu, lakini Serikali haichukui hatua. Kwa ajili hiyo

    wanadai kuwa Serikali imeshindwa kulinda uhai wa raia

    wake. Wanasema pia kwamba Serikali inapendelea

    upande wa Waislamu.

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    9/24

    9

    Ndugu Wananchi;

    Waislamu nao wanadai kuwa kitabu chao

    kitakatifu, yaani Quran Tukufu, kinadhalilishwa kwakuchanwa, kuchomwa moto na kukojolewa na Wakristo

    na Serikali haichukui hatua yo yote ya maana.

    Waislamu wananyanyaswa katika nchi yao,

    wanakamatwa ovyo, hawapewi fursa sawa na kwamba

    Serikali inawapendelea Wakristo. Wanasema nchi

    inaendeshwa kwa mfumo wa Kikristo. Mimi binafsi

    wananishutumu kuwa napendelea kushiriki zaidi

    kwenye shughuli za Wakristo kuliko za Waislamu kama

    vile harambee za kujenga Makanisa na shule za

    Makanisa. Naambiwa kuwa mwepesi kushiriki maziko

    ya Maaskofu kuliko Masheikh wanapofariki. Ipo Misikiti

    mitatu hapa Dar es Salaam wamenisomea itikafu nife.

    Katika itikafu hiyo wamewajumuisha Inspekta Jenerali

    wa Polisi, Said Mwema na Kamanda wa Polisi wa Kanda

    Maalum ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi

    Mwandamizi Ndugu Suleiman Kova.

    Ndugu Wananchi;

    Napenda kuwahakikishia Watanzania wenzangu

    kuwa mimi na Serikali ninayoiongoza, hatupendelei

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    10/24

    10

    upande wo wote. Hatufurahishwi na kitendo cha mtu

    kudhalilisha dini ya mwenzake ndiyo maana wapo

    wahadhiri wa dini ya Kiislamu na wahubiri wa dini ya

    Kikristo wamekamatwa na kufunguliwa mashtaka kwa

    nyakati mbalimbali. Vyombo vya usalama vinatambua

    wajibu wake huo na kama haifanyiki ni ulegevu wa mtu

    tu katika kutimiza wajibu wao na siyo kwamba ni sera

    na maelekezo yangu au ya Serikali. Mtakumbuka kuwa

    mara kadhaa nimewakumbusha Wakuu wa Mikoa na

    Wilaya na wakuu wa vyombo vya usalama kuacha ajizi

    katika kutimiza wajibu wao kwenye suala hili.

    Ndugu Wananchi;

    Mimi binafsi sibagui, hushiriki shughuli za

    Waislamu na Wakristo kila ninapoalikwa labda nikose

    nafasi kwa sababu nyinginezo. Nimeshafanya shughuli

    nyingi za Waislamu kama vile Maulid ya Mtume

    Muhamad S.A.W., safari za Hija, ujenzi wa misikiti na

    madrasa na mengineyo mengi. Nimeshashiriki mazishi

    ya Masheikh kama nifanyavyo kwa Maaskofu na watu

    mbalimbali Waislamu na Wakristo. Pale ambapo

    sikushiriki mazishi ya Sheikh au Askofu itakuwa ni kwa

    sababu ya kubanwa na shughuli nyingine ambazo

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    11/24

    11

    lazima nifanye mimi, au taarifa ilikuwa ya muda mfupi.

    Kwa upande wa Waislamu desturi yetu ya kuzika mara

    mtu anapofariki huwa kikwazo kwangu kushiriki hasa

    ikiwa ni nje ya Dar es Salaam kwa sababu ya taratibu

    za kumsafirisha Rais kutoka mahali pamoja kwenda

    pengine siyo nyepesi. Wakristo hawana utaratibu huo,

    huwa wanaweza kusubiri hivyo huniwia rahisi kushiriki.

    Ndugu Wananchi;

    Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali yetu

    haijashindwa kulinda usalama wa raia wake au viongozi

    wa dini na nyumba za ibada. Kama ingekuwa hivyo,

    tungeshuhudia mauaji ya raia, viongozi wa dini na

    matukio ya kuchomwa nyumba za ibada yakiwa mengi

    hapa nchini. Lakini hivyo sivyo. Nawasihi sana ndugu

    zangu Wakristo na Waislamu kuwa tusiyachakulie

    matukio ya kuuawa kwa Mchungaji Mathayo Kachila

    kule Buseresere, Geita, na Padri Evaristus Mushi kule

    Zanzibar, au kumwagiwa tindikali Sheikh Fadhili

    Soroga, Naibu Mufti wa Zanizbar, kupigwa risasi Padri

    Ambrose Mkenda na kuchomwa moto kwa Makanisa

    Zanzibar na Mbagala, Dar es Salaam kuwa ni kielelezo

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    12/24

    12

    na ushahidi wa Serikali kushindwa kutimiza wajibu

    wake.

    Kila tukio lina mazingira yake, hakuna ushahidi wavyombo vya Serikali kuzembea. Hakuna ushahidi wa

    matukio hayo kuunganika. Mpaka sasa hatujapata

    ushahidi wa kuwepo kikundi cha Waislamu wanaopanga

    kuua viongozi wa Kikristo na kuchoma moto Makanisa

    hapa nchini.

    Ndugu Wananchi;

    Kifo cha Mchungaji Mathayo Kachila wa Buseresere

    ni matokeo ya vurugu zilizosababishwa na mzozo kati

    ya Wakristo na Waislamu kuhusu kama nyama

    iliyochinjwa na Wakristo Kanisani nayo iuzwe kwenye

    bucha iliyopo pale kijijini ambayo kwa mazoea huuzwa

    nyama iliyochinjwa na Waislamu. Katika ugomvi na

    vurumai hizo ndipo watu kadhaa wa pande zote

    walijeruhiwa na Mchungaji kupoteza maisha. Si tukio

    unaloweza kulihusisha na mengineyo nchini. Ni la pale

    pale Buseresere na limeanzishwa na kuhusisha

    Wakristo na Waislamu wa Buseresere kwa sababu zao.

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    13/24

    13

    Hivi kama kusingekuwepo na mzozo wa nyama ile

    kuuzwa katika bucha ile kuumizana kule na mauaji yale

    yangetokea? Kabla ya mzozo ule Wakristo na Waislamu

    wa Buseresere hawakuwa na ugomvi baina yao.

    Walikuwa wanaishi kidugu na kushirikiana katika

    shughuli zao za kujitafutia riziki huku kila mmoja

    akimuabudu Mungu kwa misingi ya dini yake. Hivyo

    kutumia tukio hilo kutoa wito kwa Wakristo wote kuwa

    kuuawa kwa Mchungaji Kachila ni sawa na kuuawa kwa

    Wakristo wote nchini kulikofanywa na Waislamu ni

    kulikuza tatizo isivyostahili. Busara ituongoze kutafuta

    njia ya kuwapatanisha Wakristo na Waislamu wa

    Buseresere wazungumze, waelewane na waendelee

    kuishi pamoja kama ilivyokuwa awali. Hata mzozo wa

    kuchinja wanaweza kuumaliza. Mbona bucha za

    kitimoto zipo na watu hawajapigana. Kutumia mzozo

    wa Buseresere kueneza chuki kati ya Wakristo na

    Waislamu nchi nzima si sawa. Hatuwatendei haki

    Watanzania.

    Ndugu Wananchi;

    Kuuawa kwa Padri Evaristus Mushi wa Zanzibar ni

    tukio linalojitegemea halina uhusiano kabisa na lile la

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    14/24

    14

    Buseresere, Geita. Hapakuwa na mzozo kuhusu nani

    achinje. Bado uchunguzi wake unaendelea na

    tumehusisha vyombo vya upelelezi vya nje vishirikiane

    na vyetu kufanya uchunguzi. Tumefanya hivyo kwa

    sababu ya ugumu uliopatikana katika uchunguzi wa

    matukio ya kabla yake. Yaani ile la kupigwa risasi na

    kujeruhiwa kwa Padri Ambrose Mkenda na kumwagiwa

    tindikali kwa Naibu Mufti wa Zanzibar Sheikh Fadhili

    Soroga. Bado hakuna mafanikio ya kutia moyo. Na

    bado tunajiuliza kama matukio hayo matatu

    yanahusiana. Je, Makanisa kuchomwa moto kule

    Zanzibar nako kuna uhusiano wowote na matukio yale

    matatu? Uchunguzi unaoendelea unaweza kufumbua

    fumbo hilo.

    Kuna watu wanadhani yanahusiana na kwa sababu

    nzuri. Lakini inabaki kuwa ni dhana ya kibinadamu

    mpaka ukweli halisi utakapobainika. Bado kazi ya

    uchunguzi inaendelea kufanywa na vyombo vya

    usalama vya nchi yetu wakishirikiana na wenzao wanje. Katika mazingira hayo, ni mapema mno

    kumnyooshea kidole mtu ye yote na kuilaumu Serikali

    ya Muungano au Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    15/24

    15

    Serikali siyo mshirika katika mauaji hayo, na haina

    sababu ya kufanya hivyo. Ndiyo maana tunahangaika

    usiku na mchana kupata jawabu.

    Ndugu Wananchi;

    Hali kadhalika tukio la Makanisa ya Mbagala, Dar

    Es Salaam kuvamiwa, kubomolewa, mali kuibiwa na

    kuchomwa moto tarehe 12 Oktoba, 2012 nalo lina

    mazingira yake maalum. Chanzo chake ni mzozouliotokana na tukio la kusikitisha la kijana mmoja

    Mkristo kukojolea Kitabu Kitakatifu cha Waislamu, yaani

    Quran Tukufu. Pamoja na maelezo kuwa walikuwa na

    ubishi wa kitoto na kijana mwenzake, lakini kitendo

    hicho kiliwakasirisha Waislamu. Kijana huyo alifikishwa

    kituo cha Polisi. Baadhi ya Waislamu wenye msimamo

    mkali walifika kituoni hapo wakidai wapewe huyo kijana

    wamuadhibu wao. Jeshi la Polisi lilikataa. Kukatokea

    mzozo kati ya waumini hao na Polisi na baada ya

    kushindwa walichokitaka baadhi yao walipotoka pale,

    wakaenda kufanya uhalifu wa kuvunja, kuiba na

    kuchoma moto Makanisa.

    Ndugu Wananchi;

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    16/24

    16

    Baada ya tukio la Mbagala hapajakuwepo na tukio

    la kuchomwa Kanisa mahali popote kwa upande wa

    Bara. Aidha, hapajawahi kuwepo tishio lililothibitika la

    watu kutaka kuchoma Kanisa popote. Lakini maneno

    ya vitisho vya kuchoma Makanisa yako mengi hasa

    kupitia mitandao ya simu za mkononi. Kila ujumbe wa

    namna hiyo ulipofikishwa kwenye vyombo vya usalama

    uchunguzi umefanywa na hata hatua za tahadhari

    kuchukuliwa lakini hakuna hata taarifa moja

    iliyothibitika kuwa na chembe ya ukweli. Hata dalili

    hazijakuwepo.

    Tulichojifunza ni kuwa ujumbe na vitisho vya aina

    mbalimbali hupelekwa kote, kwa Wakristo na

    Waislamu. Upo unaowalenga Wakristo ukiwaambia

    wenzao Waislamu wanapanga kuwadhuru. Na upo

    wanaopelekewa Waislamu wakiambiwa Wakristo wanao

    mipango mibaya dhidi yao. Watanzania wenzangu

    nawaomba mtanabahi na mjue kuwa wapo watu

    wanacheza mchezo mchafu wa kuwagonganisha nakutaka kuwagombanisha Wakristo na Waislamu kwa

    sababu wanazozijua wao na kwa faida yao.

    Wanapandikiza chuki kwa lengo la kutaka Wakristo na

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    17/24

    17

    Waislamu wagombane. Wanapandikiza chuki baina ya

    Serikali na waumini wa dini zetu kuu mbili ili ionekane

    Serikali imewatelekeza raia wake. Ni mchezo mbaya,

    tusikubali kucheza ngoma tusiyoijua. Hivi ndugu zangu

    mmekaa chini na kujiuliza kumetokea nini kipya hata

    leo kuwa na mhemko kama huu kati ya Wakristo na

    Waislamu na kutishia kuleta vita baina nchini kote?

    Ndugu Wananchi;

    Serikali haijapuuzia kila palipotokea matukio ya

    uhalifu. Watu 76 wanaotuhumiwa kuharibu na kuchoma

    moto Makanisa kule Mbagala na kufanya fujo kituo cha

    Polisi wamekamatwa na kesi zao zinaendelea

    Mahakamani. Kwa upande wa tukio la Buseresere

    lililosababisha kifo cha Mchungaji Mathayo Kachila,

    watu 17, wakiwemo waumini wa dini ya Kikristo na

    Kiislamu walikamatwa na kesi zao zinaendelea. Wapo

    walioshitakiwa kwa mauaji na wapo walioshitakiwa kwa

    kufanya vurugu. Jeshi la Polisi bado linawatafuta watu

    wengine waliohusika na uhalifu huo ili na wao

    wakamatwe. Kwa upande wa Zanzibar, watu 10

    wanaotuhumiwa kuchoma Makanisa wamekamatwa na

    kesi zao zinaendelea. Bado hajakamatwa mtu kwa

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    18/24

    18

    tukio la mwisho la kuchoma Kanisa baada ya kuuawa

    Padri Evaristus Mushi. Uchunguzi unaendelea.

    Ndugu Wananchi;

    Kwa upande wa kujeruhiwa kwa Padre Mkenda,

    bado uchunguzi haujakamilika pamoja na kuwapo

    taarifa kadhaa zinazoendelea kufanyiwa kazi. Kuhusu

    uchunguzi wa mauaji ya Padre Mushi, baada ya jitihada

    kubwa kufanyika ikiwa ni pamoja na kushirikisha nchizilizobobea katika uchunguzi wa makosa ya aina hii,

    hatua ya kutia moyo imefikiwa. Mtu mmoja

    amekamatwa na wengine wanaendelea kutafutwa.

    Ndugu Wananchi;

    Kwa upande wa kanda na vituo vya redio nako piaSerikali imechukua hatua. Watu kadhaa

    wamekamatwa na kufikishwa Mahakamani katika

    maeneo mbalimbali hapa nchini kwa kurekodi na

    kusambaza kanda zinazochochea chuki na vurugu za

    kidini. Wapo Waislamu na Wakristo. Wapo watu

    wengine ambao wanaendelea kutafutwa. Zipo taarifa

    kuwa baadhi yao wamekimbilia nchi za nje. Jeshi la

    Polisi limeomba msaada wa Polisi wa Kimataifa, yaani

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    19/24

    19

    Interpol, kusaidia kuwatafuta na kuwarejesha nchini.

    Vituo viwili vya radio yaani Kwa Neema FM cha

    Sengereme na Radio Imani cha Morogoro vimefungiwa

    kwa muda wa miezi sita. Baada ya muda huo kupita,

    Kamati ya Maudhui ya Mamlaka ya Mawasiliano

    itaamua ipasavyo.

    Ndugu Wananchi;

    Nimeyaeleza haya kwa kirefu kuwahakikishia kuwaSerikali inajali usalama wa raia wake wa mali zao na

    amani na utulivu wa nchi yetu. Kamwe hatujashindwa

    kulinda raia wa nchi wa yetu na yapo mambo mengi

    yaliyofanyika na yanayoendelea kufanyika kuhakikisha

    kuwa Watanzania wa dini zote, makabila yote, rangi

    zote na mahali po pote walipo wako salama. Tunataka

    kuona watu wanaendelea kuishi kwa amani, upendo,

    ushirikiano na mshikamano kama tulivyokuwa tunaishi

    siku zote. Tunapenda kuona Watanzania wanaepuka

    mambo yanayowabagua na kusisitiza yale

    yanayowaunganisha. Tujiepushe kuyapa kipaumbele

    yale yanayotugawa.

    Ndugu Wananchi;

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    20/24

    20

    Athari za mzozo kuhusu kuchinja kule Geita iwe

    fundisho kwetu sote. Tuazimie sote kuwa yaliyopita si

    ndwele, tugange yajayo. Hebu tufikirie maisha yetu

    Watanzania yatakuwaje kwenye shughuli za kijamii

    kama vile sherehe, harusi, ngoma na misiba iwapo

    tutaanza kuwa na chakula tofauti kwa Waislamu na

    Wakristo. Fikiria itakuwaje kwenye hospitali, shule na

    vyuo pawe na majiko mawili au labda hata mabwalo

    mawili ya chakula kwa Waislamu na Wakristo. Jeshini

    nako kuwe na majiko na mabwalo ya Waislamu na

    Wakristo. Hali iwe hivyo hivyo kwenye migahawa na

    maeneo mengine yenye huduma ya chakula.

    Ndugu zangu, tunataka kuipeleka wapi nchi yetu?

    Tunataka kujenga nchi ya namna gani? Mimi naamini

    tukifanya hivyo huo utakuwa ndiyo mwanzo wa

    kubaguana kwa kila kitu na kila jambo na kuligawa taifa

    kwa namna ambayo hatutakuwa wamoja tena. Huko

    tunakoelekea siko, ni kubaya. Tubadilike, na wakati ni

    huu. Viongozi wa dini waongoze njia wawaepushewaumini wao na taifa letu na janga hili.

    Ndugu Wananchi;

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    21/24

    21

    Bado narudia kusisitiza umuhimu wa viongozi wa

    dini zetu kubwa mbili kukutana na kuizungumzia hali hii

    na kuipatia ufumbuzi. Ni wao kuliko mtu mwingine ye

    yote wenye majawabu ya matatizo haya. Ni masuala

    yanayohusu imani za dini na yanafanywa na viongozi

    wa dini na wafuasi wao kwa jina la dini zao. Serikali ina

    wajibu wa kulinda amani. Kazi yetu itakuwa rahisi kama

    waumini hawatafanya vitendo vitakavyosababisha

    uvunjifu wa amani. Wa kuongoza waumini lipi jema na

    lipi baya ni viongozi wa dini.

    Ndugu Wananchi;

    Nimeshakutana na viongozi kadhaa wa

    madhehebu na taasisi za dini za Kikristo na Kiislamu

    kuzungumza nao kuhusu jambo hilo. Nimepata faraja

    kuona kuwa wote wanasikitishwa na mambo

    yanayotokea hivi sasa na wameona busara ya viongozi

    wa dini kuzungumza ili kuondoa tofauti zilizojitokeza.

    Wanakiri kuwa hali ilivyo sasa siyo ya kawaida kwa

    Tanzania na Watanzania. Kuna upepo mbaya wa

    shetani unapita ambao viongozi wa dini wana wajibu

    wa kuhakikisha kuwa hali ya hewa inasafishwa na

    kurejesha nchi yetu na watu wake katika maisha

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    22/24

    22

    tuliyoyazoea. Maisha ambayo waumini wa dini tofauti

    wanaishi pamoja kwa udugu, upendo, ushirikiano na

    mshikamano kwa misingi ya ubinadamu wao na

    Utanzania wao.

    Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Pinda,

    ameshaeleza dhamira ya Serikali ya kuitisha mkutano

    wa viongozi wa dini mapema mwezi ujao. Ni

    matumaini yangu kuwa wote watashiriki wenyewe bila

    ya kutuma wawakilishi. Lazima tupate jawabu kwa

    maslahi ya taifa letu na watu wake.

    Ndugu Wananchi;

    Kabla ya kumaliza hotuba yangu napenda kutumia

    nafasi hii kuwaomba na kuwasihi waandishi wa habari

    wasaidie kuliepusha taifa letu kuingia katika vita vya

    kidini. Waache kushabikia taarifa zinazochochea na

    kujenga uhasama baina ya waumini wa dini zetu.

    Nawaomba wapime athari za taarifa zao kabla ya

    kuziandika au kuzitangaza. Wawe makini na maneno

    wanayotumia. Katika hali tuliyonayo sasa lazima sote

    tuazimie kuondoa tofauti za kidini na kujenga umoja

    miongoni mwa Watanzania wa dini zote. Wasipofanya

    hivyo, wataliingiza taifa katika mgogoro mkubwa

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    23/24

    23

    ambao hauna msingi kama ilivyotokea katika nchi

    jirani. Nawaomba wamiliki wa vyombo vya habari

    kutambua kuwa wanao wajibu wa kuhakikisha vyombo

    vyao havitumiki kuleta mifarakano kwa kuchochea

    uhasama baina ya Wakristo na Waislamu.

    Hitimisho

    Ndugu Wananchi;

    Naomba kumaliza kuwa kusisitiza kuwa wananchi

    wote kudumisha umoja na mshikamano wetu. Tuishi

    kwa upendo, umoja, mshikamano na ushirikiano bila

    kujali tofauti ya dini zetu, kabila, rangi au mahali

    atokako mtu. Hizo ndizo tunu za taifa letu la Tanzania

    ambazo hatuna budi kuzienzi, kuzilinda na

    kuzidumisha. Narudia kuwahakikishia kuwa Serikali

    haipendelei dini yo yote na wala haina mpango wa

    kushiriki kuangamiza dini yo yote au waumini wao.

    Serikali kupitia vyombo vyake vya usalama itaendelea

    kuhakikisha ulinzi na usalama wa raia wake na mali zao

    kama inavyofanya siku zote. Kama kuna mtu anaona

    kuwa maisha yake au mali zake zipo hatarini, aende

    kutoa taarifa Polisi. Hatua zipasazo zitachukuliwa.

  • 7/28/2019 Hotuba Final[1]

    24/24

    24

    Ndugu Wananchi;

    Mwisho nawatakia sikukuu njema ya Pasaka.

    Tusherehekee kwa amani na utulivu. Tusherehekeepamoja.

    Mungu Ibariki Afrika!

    Mungu Ibariki Tanzania!

    Asanteni kwa Kunisikiliza.