16
TUME YA UCHAGUZI YA ZANZIBAR MWONGOZO NA MAADILI YA WAANGALIZI WA NDANI NA WA NJE WA CHAGUZI ZA ZANZIBAR Kimetayarishwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar July, 2015

Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

Embed Size (px)

DESCRIPTION

MWONGOZO NA MAADILI YAWAANGALIZI WA NDANI NA WA NJE WA CHAGUZI ZA ZANZIBAR

Citation preview

Page 1: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

TUME YA UCHAGUZI YA ZANZIBAR

MWONGOZO NA MAADILI YA

WAANGALIZI WA NDANI NA WA NJE WA

CHAGUZI ZA ZANZIBAR

Kimetayarishwa na

Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar

July, 2015

Page 2: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

1

MWONGOZO NA MAADILI YA WAANGALIZI WA NDANI

NA WA NJE WA CHAGUZI ZA ZANZIBAR

DIBAJI

Napenda kuchukuwa fursa hii adhimu kuwakaribisheni nyote, kwa niaba ya Tume ya

Uchaguzi ya Zanzibar na watu wa Zanzibar kwa kukubali mwaliko wa kuwa

Waangalizi wa Uchaguzi katika hali yoyote ile uwe Mwangalizi wa Ndani au

Mwangalizi wa Nje.

Kila Mzanzibari ana haki ya kutumia haki ya kisheria ya kupiga kura kupitia karatasi

ya kura na kuyafanya mawazo au uamuzi wake huo kuheshimiwa. Tume itahakikisha

kila kura iliyo halali inahesabiwa katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Katika

kuhakikisha hilo, Tume imewakaribisha watu wote na wenye nia na lengo jema

wakiwemo Waangalizi wa Uchaguzi.

Tume imefanya matayarisho ya kutosha ili kuhakikisha, Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar

wa 2015, unakuwa ni uchaguzi huru na wa haki na unakidhi matarajio ya wadau,

wakiwemo wapiga kura na wananchi wa Zanzibar. Kila jitihada imefanywa

kuhakikisha watendaji na wasimamizi wa uchaguzi wamepatiwa mafunzo ya kutosha

na wana tabia nzuri. Tume haikusahau suala la uagiziaji wa vifaa ambao umefanywa

kwa wakati ili kuweka mazingira bora ya uchaguzi.

Waangalizi wa Uchaguzi, wana wajibu na wanashauriwa kuweka bayana mafanikio

na kuibuwa changamoto yoyote inayoweza kutokea kupitia Mwngozo huu.

Waangalizi wana umuhimu mkubwa katika kujiridhisha kuwa wapiga kura wanapiga

kura zao katika mazingira ya usalama na amani bila ya vitisho au kulazimishwa

kupiga kura kwa namna fulani na taratibu za upigaji kura zinafuatwa kikamilifu.

Waangalizi, pia watashuhudia iwapo matokeo yaliyotangazwa na Tume yanaendana

na kura zilizohesabiwa. Waangalizi wanapaswa kujua kuwa, ripoti zao za uangalizi

zinatoa taarifa muhimu kwa kuboresha upigaji kura Zanzibar hasa zikizingatia

umuhimu wa ushiriki wa makundi yaliyo katika hatari ya kukandamizwa wakiwemo

wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Matayarisho ya kutosha yamefanywa na Tume kwa kufanikisha uangalizi wa

uchaguzi katika hatua zote za uangalizi kabla, wakati na baada ya uchaguzi. Kituo

kinaanzishwa cha kuwasaidia Waangalizi kupata ruhusa zao na pia kuwarahisishia

kazi wao na waandishi wa habari.

Mwongozo huu wa Waangalizi, unaendana na maudhui ya Sheria ya Uchaguzi

Namba 11 ya 1984 na Kanuni zake, Miongozo ya kimataifa ya uangalizi wa uchaguzi,

Page 3: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

2

pamoja na Sera ya Tume ya Jinsia na Ushirikishwaji Jamii ya Mwaka 2015 na

Mpango Mkakati wa Miaka Mitano wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar.

Nawashauri Waangalizi wote watekeleze majukumu yao kwa umakini na weledi na

vile vile kutoa taarifa juu ya mazuri na mabaya yote yanayohusiana na uchaguzi.

Kwa mara nyengine tena nawakaribisha nyote kufanya uangalizi wa uchaguzi wa

mwaka 2015.

Bw. Salum Kasim Ali

Mkurugenzi wa Uchaguzi

Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar

Page 4: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

3

1.0 UTANGULIZI

Mwongozo huu umekusudiwa kuwasaidia Waangalizi wa Ndani na wa Nje kujua

nidhamu inayotarajiwa kwao watapokuwa Zanzibar, na kuwaongoza katika

utekelezaji wa majukumu yao ya uangalizi wa uchaguzi. Kutokana na sababu

hiyo, Mwongozo huu umejumuisha Maadili ya Waangalizi wa Uchaguzi

wanaoangalia chaguzi za Zanzibar.

Mwongozo pia, una lengo la kusaidia zoezi la uangalizi wa uchaguzi lifanyike bila

ya bughudha kwa mtu ye yote, awe mpiga kura, mtendaji wa uchaguzi,

waangalizi wengine au mdau mwingine yeyote wa uchaguzi.

Uangalizi wa uchaguzi una umuhimu mkubwa kwa vile unasaidia katika kujenga

ukweli, uaminifu na uhalali wa uchaguzi kwa vile unasaidia kujenga mazingira

kwa uchaguzi kuendeshwa kwa uwazi, uhuru na kwa mujibu wa sheria.

Mahususi, uangalizi wa uchaguzi unasaidia kuwaweka watendaji wa uchaguzi

katika hali ya umakini wa kuzingatia sheria na kanuni za uchaguzi na katika

utekelezaji wa majukumu yao ya kuendesha uchaguzi.

Katika kufanikisha hili, Waangalizi wa uchaguzi wanatakiwa watekeleze wajibu

wao kwa weledi ili kujijengea imani ndani ya mchakato wa uchaguzi na kutoka

kwa wadau wengine.

2.0 UHALALI WA KISHERIA

Mwongozo huu pamoja na Maadili ya Waangalizi wa Uchaguzi kwa ajili ya

Waangalizi wataoangalia chaguzi za Zanzibar, umetolewa chini ya kifungu cha

130 cha Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar ya 1984, na utawahusu Waangalizi wote

wataoruhusiwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar.

3.0 TAFSIRI

Katika Mwongozo huu, isipokuwa itavyoelezwa vyenginevyo maneno:

a) “Uangalizi wa Ndani” maana yake ni uangalizi wa hatua yoyote ya uchaguzi,

moja au zote zilizomo katika mzunguko wa uchaguzi, unaofanywa na asasi za

ndani na/au mtu ambaye ameruhusiwa na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar

kufanya uangalizi.

b) Uangalizi wa Kimataifa” maana yake ni uangalizi wa hatua yoyote ya

uchaguzi, moja au zote zilizomo katika mzunguko wa uchaguzi zikiwemo

tathmini za hali za kabla na baada ya uchaguzi, unaofanywa na asasi za

Page 5: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

4

kimataifa na wawakilishi wa serikali za nje walioruhusiwa na Tume ya

Uchaguzi ya Zanzibar kufanya uangalizi.

c) “Waangalizi” maana yake ni waangalizi wa Ndani na wa Nje ya Tanzania, na

inajumuisha wale wanaokuja kutoka nje ya Tanzania kwa ajili ya kutathmini

hali kabla na baada ya uchaguzi.

d) “Kundi la Waangalizi” maana yake ni kundi la Waangalizi walioletwa au

kudhaminiwa na asasi.

e) “Maadili” maana yake ni masharti yaliyomo katika kifungu cha 13 cha

Mwongozo huu.

f) “Tume” maana yake ni Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar.

g) “mzunguko wa uchaguzi” maana yake ni mfuatano wa hatua mbali za

uchaguzi toka maandalizi kabla ya uchaguzi, kufanyika kwa uchaguzi

wenyewe hadi tathmini za baada ya kukamilika kwa uchaguzi.

4.0 MUDA WA UANGALIZI:

Muda wa uangalizi wa uchaguzi kuhusiana na Mwangalizi utaanzia tarehe

atayopata ruhusa hadi

a) tarehe iliyowekwa ya kuwasilisha ripoti ya mwisho ya uangalizi, au

b) kufutwa kwa ruhusa ya uangalizi kutokana na kuvunja Maadili, au

c) baada ya kukamilika kipindi cha miezi mitatu baada ya kutangazwa kwa

matokeo ya uchaguzi;

lolote kati ya hayo litalotokea mwanzo.

5.0 AINA ZA WAANGALIZI

Kutakuwa na Waangalizi wa aina zifuatazo:-

a) Waangalizi wa Ndani ambao wanaweza kutoka katika:

i) Asasi za umma zinazofanyakazi Zanzibar ambazo miongoni mwa

majukumu yake yanahusiana na masuala ya uchaguzi na utawala

bora.

ii) Asasi za kijamii kama vile zisizo za kiserikali (NGO’s) na za wananchi

(CBOs) ambazo zimesajiliwa Zanzibar.

Page 6: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

5

iii) Asasi za kidini zilizosajiliwa katika Jamuhuri ya Muungano wa

Tanzania

iv) Wawakilishi wa wagombea na wa vyama vya siasa, vyombo vya

habari na waandishi wa habari wenye vibali vilivyotolewa na

Mamlaka zinazohusika za Zanzibar.

b) Waangalizi wa Nje wanaoweza kutoka katika :-

i) Mashirika au Taasisi za Kimataifa ambazo Tanzania ni mwanachama

au ina uhusiano wa kidiplomasia nazo.

ii) Mashirika au Taasisi za kikanda ambazo Tanzania ni mwanachama au

zina uwakilishi Tanzania.

iii) Ofisi za kibalozi za nchi za nje zinazowakilisha nchi zao Tanzania.

iv) Tume za Uchaguzi kutoka nchi nyengine za Dunia.

v) Asasasi zisizo za kiserikali za kimataifa zinazofanya kazi Tanzania au

iwapo hazifanyi kazi Tanzania, zimepata kibali maalumu cha mamlaka

husika za Zanzibar.

c) Waangalizi wa muda mfupi ambao ni Waangalizi wa Nje wanaokuja

nchini kwa ajili ya kutathmini hali kabla au baada ya uchaguzi na kukaa

kwa muda usiozidi ziku 15.

d) Waangalizi wa muda mrefu ni Waangalizi wa Nje wanaokuja kwa

uangalizi wa hatua zaidi ya moja za uchaguzi na kukaa kwa muda

unaozidi siku 60.

6.0 RUHUSA YA UANGALIZI WA UCHAGUZI:

Kabla ya kuanza majukumu ya uangalizi, Waangalizi lazima wawe wameshapata

ruhusa ya uangalizi ili kuwatofautisha na wadau wengine wa mchakato wa

uchaguzi. Utoaji wa ruhusa kwa Waangalizi ni jukumu la Tume pekee. Ili

Waangalizi waweze kupatiwa ruhusa, utaratibu ufuatao lazima ufuatwe:-

a) Mialiko ya jumla kwa Waangalizi wa Nje hutolewa na Serikali ya Jamhuri ya

Muungano wa Tanzania.

b) Asasi na serikali zinazodhamini Waangalizi zitaijuilisha Tume juu ya dhamira

na mipango yao ya kuleta Vikundi vya Waangalizi, kabla ya siku ya mwisho

itayokuwa imewekwa na Tume.

Page 7: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

6

c) Ili mtu atambulike kama Mwangalizi, anatakiwa awe amethibitishwa

kimaandishi na asasi husika au Serikali ya nje kwa Tume kupitia barua

itayotoa taarifa mbali mbali zinazomhusu pamoja na wasifu wake.

d) Japokuwa Waangalizi huweza kuletwa na asasi, ruhusa ya uangalizi

hutolewa kwa Mwangalizi binafsi; kwa hivyo wanawajibika pia kuomba

ruhusa kila mmoja binafsi.

e) Katika maombi yake, kila Mwangalizi atatakiwa kuwasilisha wasifu na taarifa

zake rasmi za utambulisho kwa Tume.

f) Zaidi ya nyaraka za utambulisho wa Mwangalizi zilizowasilishwa na asasi

iliyomdhamini au Serikali yake, kila Mwangalizi atapatiwa na Tume, hati ya

ruhusa pamoja na kitambulisho au vitambulisho vitavyomwezesha

kutambulika kwa urahisi.

g) Mwangalizi atatakiwa muda wote atapokuwa anatekeleza jukumu lake la

uangalizi, kuvaa kwa uwazi kitambulisho atachokuwa amepatiwa na Tume;

atachukua pia nyaraka zake za ruhusa ya uangalizi; na kwa Mwangalizi wa

nje atachukua pamoja na nyaraka hizo, nyaraka zake halali za kusafiria.

7.0 VIDOKEZO VYA USHAURI KWA AJILI YA UANGALIZI WENYE UFANISI

Itapendeza kwa Mwangalizi:-

a) Kuwa na kiasi fulani cha uzoefu, sifa ya kutopendelea upande wowote, na

kuonyesha uhuru wa mawazo ili asiburuzwe na vyama vya siasa.

b) Kuweza kuzungumza Kiswahili na/au Kingereza kwa ajili ya mawasiiliano

na wenyeji;

c) Kuwa na uelewa wa Sheria za Uchaguzi za Zanzibar;

d) Kuwa na uelewa na ufahamu wa viwango vya kimataifa vya kuweza

kupambanua hali za mchakato uchaguzi kuwa huru na wa haki ;

e) Kuwa na uwelewa wa historia, jiografia, utamaduni na hali halisi ya

kisiasa ya Zanzibar na;

f) Kuzipa uzito taarifa na ripoti zake za uangalizi kwa kubainisha rejea za

sheria,kanuni, mpango mkakati, na sera zinazoongoza uchaguzi na

kuzioanisha na viwango vya kimataifa vilivyo ridhiwa na Serikali ya

Tanzania juu ya upigaji kura katika vituo vya upigaji kura.

Page 8: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

7

8.0 MIONGOZO MAALUMU KWA WAANGALIZI WA NJE

Waangalizi wa Nje zaidi ya masharti ya jumla watawajibika:-

a) Kuwa na hati halali za kusafiria ikiwemo viza pale inapohitajika.

b) Kufuata maelekezo ya kiafya.

c) Kuzingatia vidokezo vya afya vitavyotolewa na Tume na

d) Kufuata tahadhari za kiusalama zitazotolewa na Tume.

9.0 NYARAKA NA TAARIFA ZA MAELEZO YA AWALI

Tume itatoa kwa Waangalizi nyaraka na taarifa juu ya masuala mbali mbali

yanayohusu Zanzibar.

Nyaraka na taarifa hizo zitajumuisha yafuatayo:-

a) Taarifa zinazohusiana na historia (ikiwemo ya uchaguzi), jiografia na hali

halisi ya kisiasa ya Zanzibar.

b) Taarifa kuhusu mchakato wa uchaguzi zikiwemo sheria na kanuni za

uchaguzi.

c) Orodha ya vituo vya kupigia kura anavyotaka kuvifanyia kazi mwangalizi.

d) Orodha ya vyama vya siasa vyenye usajili kamili.

e) Orodha ya wagombea na vyama vyao katika jimbo.

f) Ratiba ya Mikutano ya kampeni za Uchaguzi.

g) Sera ya Tume ya Jinsia na Ushirikishwaji wa Jamii ya mwaka 2015.

h) Nyaraka nyingine zozote ambazo Tume itaona zitafaa kupatiwa

Waangalizi.

10.0 UPEO WA UANGALIZI :

Upeo wa uangalizi utajumuisha vipindi vyote vya mzunguko wa uchaguzi na

hususan utajumuisha tathmini ya mambo yafuatayo miongoni mwa mengine:-

a) Tume kutopendelea na kufanya kazi kwa uadilifu.

b) Haki na uhalali wa kisheria wa maamuzi yanayofanywa na Tume kuhusiana

na migogoro ya kiuchaguzi.

c) Kutosheleza kwa mfumo wa kisheria unaoongoza masuala ya uchaguzi.

d) Haki katika ukataji wa majimbo ya uchaguzi.

e) Utaratibu wa uandikishaji wa wapiga kura.

f) Mchakato wa uteuzi wa wagombea kuanzia ndani ya vyama vya siasa.

g) Utaratibu wa kuendesha na kusimamia kampeni za uchaguzi.

h) Utaratibu wa kupiga kura na kutangaza matokeo.

Page 9: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

8

i) Ujumuishaji wa kura katika hatua zote na kutangaza matokeo ya uchaguzi.

j) Hali ya kisiasa baada ya kukamilika kwa uchaguzi.

k) Katika tathmini yake ya kila moja ya hatua hizi na masuala mengine ya

mzunguko wa uchaguzi, Mwangalizi atatarajiwa kukusanya taarifa sahihi

kwa kuzingatia yafuatayo:-

i) Uelewa wa kutosha wa Sheria, Kanuni, Mpango Mkakati na Sera

zinazoongoza chaguzi na taratibu za utendaji kazi wa Tume.

ii) Hali halisi ya kisiasa ya nchi, kabla, wakati na baada ya uchaguzi,

hususan taswira za wananchi kuhusiana na maisha yao ya kawaida,

usawa wa kijinsia na ushiriki wa makundi mbalimbali ya kijamii,

harakati za vyama vya siasa, wagombea, wapambe na wengineo.

iii) Ushiriki wa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu hususan

mazingatio maalumu watakayokuwa wamewekewa kurahisisha

ushiriki wao katika uchaguzi.

iv) Mchanganuo wa takwimu kijinsia.

v) Hali ya utayari wa uchaguzi kama vile uandikishaji wa wapiga kura,

utoaji wa elimu ya uraia na ya wapiga kura, uteuzi wa wagombea,

ukataji wa majimbo ya uchaguzi, kampeni za uchaguzi n.k.

vi) Uelewa juu ya wajibu wa kila mdau wa uchaguzi na wananchi kwa

jumla katika shughuli za uchaguzi.

vii) Namna haki za msingi za watu zinavyoheshimiwa kwa mnasaba wa

uchaguzi.

viii) Kama vyombo vya habari vya umma vinatumiwa kwa usawa na

vyama vya siasa wakati wa kampeni.

ix) Kama fursa ya matumizi ya vyombo vya habari vya binafsi

inatolewa kwa usawa kwa vyama vya siasa pamoja na kuzingatia

maslahi yaliyotangazwa navyo.

x) Uheshimu wa jumla wa Maadili ya Vyama vya Siasa na wadau

wengine.

xi) Uwakilishi wa vyama vya siasa na/au wagombea katika maeneo na

vituo vya uandikishaji na kupigia kura.

Page 10: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

9

xii) Ushirikishwaji wa vyama vya siasa na wadau wengine wa uchaguzi

katika harakati za Tume ya uchaguzi.

xiii) Uzowefu na uwezo wa watendaji wa uchaguzi katika kupanga na

kuendesha uchaguzi.

xiv) Maoni ya jumla juu ya uchaguzi ulivyokwenda hususan kuhusu

kujitokeza kwa wapiga kura; urahisi wa mchakato wa upigaji kura,

uhesabuji wa kura, ujumuishaji wa kura na utangazaji wa matokeo.

xv) Aina ya migogoro iliyojitokeza na namna ilivyoshughulikiwa na

wahusika wa shughuli za uchaguzi.

xvi) Kutathmini taarifa zote bila ya jazba za aina yoyote, wala upendeleo

kwa mwelekeo wa kuweka wazi mambo yaliyokwenda vyema;

mambo yaliyokwenda kombo kutokana na kuvunjwa kwa sheria na

kanuni na kupuuzwa kwa viwango vya kimataifa vya uendeshaji wa

uchaguzi; na hatimaye masuala yatayopaswa kushughulikiwa katika

chaguzi za siku za mbele.

xvii) Kuwasilisha ripoti za uangalizi wa uchaguzi kwa Tume na wadau

wengine wanaohusika.

11.0 UTARATIBU WA KURIPOTI:

Ni matarajio ya kawaida kwamba Kundi la Waangalizi litabainisha miongozo yake

kwa Waangalizi wake kabla ya kuanza majukumu yake. Hata hivyo, Waangalizi

Zanzibar wanatarajiwa kutoa taarifa/ripoti za wanayoyaona katika hatua tatu

kama ifuatavyo:-

a) Wakati wa Uangalizi Wenyewe:

Mwangalizi ataripoti bila ya kuingilia kati kwa aina yoyote mchakato wa

uchaguzi unaoendelea, changamoto yoyote ya kiutekelezaji wa sheria

atayoibaini wakati wowote wa uandikishaji wapiga kura au upigaji kura, kwa

Tume au Msimamizi wa Uchaguzi au Msaidizi wake ambaye ataifanyia kazi

kasoro hiyo na kuirekebisha ipasavyo.

b) Mara Baada ya Uchaguzi:

Mwangalizi au Kundi la Waangalizi, kwa kadiri itavyokuwa, litawajibika

kutoa taarifa ya awali ya uangalizi itayoelezea tathmini yake ya ujumla juu

ya uchaguzi ulivyoendeshwa.

Page 11: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

10

c) Katika kipindi cha siku 90 baada ya kutangazwa kwa matokeo

Waangalizi au makundi ya Waangalizi, kwa kadiri itavyokuwa, watawajibika

kuwasilisha ripoti zao za mwisho za uangalizi kwa Tume.

Katika utayarishaji wa ripoti zao, Waangalizi au makundi ya Waangalizi

watapaswa kuzingatia yafuatayo:-

i) Upekee na uhalisia wa Zanzibar, kuhusiana na historia yake,

maendeleo ya kikatiba, shughuli za kisiasa, utamaduni na mfumo wa

uchaguzi.

ii) Kila uchaguzi una mambo yanayoutofautisha na mwingine kulingana

na sehemu unapofanyika na sheria zinazouongoza.

iii) Uchambuzi wenye kuheshimika wa mambo yaliyoonekana katika

uangalizi wa uchaguzi hutokana na taarifa za kweli, zilizo sahihi na

zenye kuthibitika. Uchambuzi unaotokana na hisia, utashi, uvumi au

mtazamo aliokuja nao Mwangalizi hupelekea ripoti zisiso sahihi.

iv) Kutumia lugha ambayo haitokuwa chanzo cha mtafaruku na mgogoro

usiokuwa wa lazima.

v) Ripoti zisielezee tu mambo yaliyokwenda kombo, bali pia mambo

yaliyokwenda vyema na kutoa mapendekezo juu ya mambo ya

kufanya yatayosaidia kufanya chaguzi za siku za mbele kuwa bora

zaidi.

vi) Katika ripoti zao, Waangalizi wanapaswa kujiepusha kuingiza maneno

ya uvumi kutoka watu wengine, bali wajikite katika mambo

waliyoyaona wenyewe, wakizingatia vidokezo mbalimbali vya ushauri

vilivyomo katika Mwongozo huu.

12.0 HAKI ZA WAANGALIZI:

Waangalizi Zanzibar watakuwa na haki zifuatazo:-

a) Kuomba na kupatiwa kwa wakati muafaka taarifa stahiki juu ya kila hatua

ya mchakato wa uchaguzi.

b) Kupata wepesi wa kuingia katika maeneo ya uchaguzi kama vile vituo vya

uandikishaji au vya kupigia kura wakati na baada ya shughuli husika; na

kuomba na kupatiwa taarifa kutoka kwa wahusika walioruhusika wa

Page 12: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

11

uendeshaji wa uchaguzi, watendaji wa vyombo vya kutunga sheria,

maofisa husika wa serikali, waandishi wa habari, asasi nyengine yoyote

husika na wadau wataofikiriwa kuwa na taarifa zitazoweza kusaidia

uangalizi.

c) Kuwa na uhuru wa kutembea Zanzibar yote isipokuwa maeneo ya kijeshi

na maeneo mengine yaliyokatazwa kisheria.

d) Bila ya kuathiri Maadili yaliyotajwa katika kifungu cha 13 cha Mwongozo

huu, kuwasiliana kwa uhuru na wawakilishi wa vyama vya siasa.

e) Kuhakikisha usalama wao pahali popote wanapokwenda wakitekeleza

majukumu yao.

13.0 MAADILI YA WAANGALIZI :

Ingawa Waangalizi hutekeleza majukumu yao kwa uhuru, kuna sheria, kanuni na

maadili wanayotarajiwa kama sharti la msingi na wajibu, kuyaheshimu na

kuyafuata ili wadhihirike kuwa ni watu wenye hadhi stahiki ya kuaminika na

kuheshimika; na vitendo vyao vyenye faida katika kukuza demokrasia ya

uchaguzi

Kwa kuzingatia misingi ya sheria za uchaguzi, kanuni na viwango vya kimataifa

vya uendeshaji uchaguzi, Waangalizi watawajibika kutekeleza masharti yafuatayo

ambayo kwa pamoja yanafanya Maadili ya Waangalizi:-

a) Kuruhusiwa kwa ukamilifu na Tume kabla ya kuanza harakati za uangalizi.

b) Kuzielewa na kuziheshimu sheria za Tanzania kwa jumla na hususan za

Zanzibar.

c) Kutopendelea kabisa kwa namna yoyote vyama vya siasa, wagombea na

mchakato wote wa uchaguzi kwa jumla.

d) Kuwa watu wenye tabia za kujiheshimu na kuheshimu wengine.

e) Kuheshimu majukumu, hadhi na madaraka ya maafisa wa uchaguzi.

f) Kutoingilia kwa namna yoyote, kazi za maofisa wa uchaguzi wala uendeshaji

wa uchaguzi kwa ujumla.

Page 13: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

12

g) Kuepuka malumbano na maofisa wa uchaguzi, mawakala wa vyama vya

siasa na wa wagombea, Waangalizi wengine, wadau wengine ndani ya

vituo vya kuandikishia wapiga kura na vya kupigia kura ambayo yanaweza

kusitisha mwenendo wa uandikishaji, upigaji kura na kuhesabu kura.

h) Asifanye kazi za utendaji (kama vile kutoa maagizo au amri kwa watendaji

wa shughuli za uchaguzi), wala asifanye kazi za tume ya uchunguzi au za

ushauri elekezi.

i) Kujizuia kutoa taarifa kwa umma ambazo zinaweza kusababisha mtafaruku

au migongano wakati wa mchakato wa uchaguzi.

j) Kujiepusha kutoa maelezo na taarifa zisizo sahihi.

k) Kujiepusha na matumizi ya lugha au vitendo vinavyoweza kusababisha

uvunjifu wa amani wakati mchakato wa uchaguzi ukiendelea.

l) Kutowatumia kisiasa wasaidizi wao kama vile wakalimani na madereva.

m) Kuheshimu utamaduni wa nchi.

n) Kutotangaza au kutochapisha kabisa matokeo ya uchaguzi kabla

hayajatangazwa na Tume.

o) Kurudisha kitu chochote ambacho ametakiwa na tume kurejesha baada ya

matumizi yake.

p) Kuwasilisha ripoti kamili ya uangalizi kwa Tume katika kipindi kisichozidi siku

90 baada ya kutangazwa kwa matokeo kwa kuzingatia maelekezo ya

kifungu cha 11(c) cha Mwongozo huu.

14.0 KUONDOLEWA HADHI YA UANGALIZI

Mwangalizi yeyote anaweza kuzuiliwa uangalizi wake katika mazingira

yafuatayo:-

a) Ikiwa atakiuka kipengele chochote cha Maadili, ruhusa yake ya uangalizi

itaweza kufutwa (baada ya mashauriano na uongozi wa Kundi lake la

Waangalizi au asasi iliyomdhamini); hivyo kusababisha kuzuiliwa kwa

harakati zake za uangalizi.

b) Ikiwa atamfanyia kampeni mgombea au chama cha siasa au kuonesha

upendeleo kwao, siyo tu ruhusa yake ya uangalizi itafutwa, bali pia atakuwa

Page 14: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

13

ameathiri uwezekano wa kuruhusiwa tena kushiriki uangalizi wa chaguzi za

siku za mbele za Zanzibar.

c) Ikiwa Mwangalizi au Kundi la Waangalizi limekiuka matakwa ya kifungu cha

13(p) cha Mwongozo huu watakuwa wameathiri sana uwezekano wa

kuruhusiwa tena kushiriki uangalizi wa chaguzi za siku za mbele za Zanzibar.

15.0 KUTUMIKA NA KUMALIZIKA MATUMIZI YA MWONGOZO HUU:

Mwongozo huu utaanza kutumika pale Mwangalizi au Kundi la Waangalizi

watapokubali mwaliko waliopewa na Tume, na utakoma pale Mwangalizi au

Kundi hilo litapowasilisha ripoti yake ya mwisho, au vinginevyo

atapokuwa/litapokuwa limeondolewa hadhi ya uangalizi.

Jecha S. Jecha

Mwenyekiti

Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar

Zanzibar, 2015

Page 15: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

14

TUME YA UCHAGUZI YA ZANZIBAR

Ahadi ya Waangalizi wa Uchaguzi Kutekeleza Mwongozo na Maadili

Nathibitisha kuwa, nimeusoma na kuuelewa Mwongozo huu na Maadili ya Wangalizi

wa Uchaguzi kwa Waangalizi wa Ndani na wa Nje.

Sasa naahidi kuwa nitautekeleza na kuufuata Mwongozo huu na kwamba utekelezaji

wa majukumu yangu utafuata Mwongozo huu. Sina mgongano wa maslahi ya

kisiasa, kiuchumi au mengineyo yoyote, ambao unaweza kuathiri uwezo wangu wa

utendaji kazi wa kuwa Mwangalizi asiyekuwa na upande fulani na kufuata kikamilifu

Maadili ya uangalizi yaliyomo katika Mwongozo huu.

Naahidi kuwa nitahakikisha kuwa nitafanya kazi zangu bila ya kuwa na upendeleo wa

kisiasa. Nitatoa maamuzi kufuatana na taarifa sahihi na kufanya uchambuzi

usioegemea popote wakati wote. Nitatoa uamuzi kufuatana na ushahidi ulio wazi na

uliofanyiwa utafiti.

Kwa hali na namna yoyote ile sitoingilia kati wala kuzuwia mchakato wa uchaguzi.

Nitaheshimu sheria za Zanzibar na Tanzania na mamlaka ya watendaji wa uchaguzi

na kuendeleza heshima juu ya mamlaka za uchaguzi na nyenginezo. Nitaheshimu

haki za msingi na uhuru wa watu wa Zanzibar. Nitadumisha tabia njema na heshima

kwa wengine, nitaheshimu tamaduni, mila na silka za Zanzibar na nitafanya

maamuzi muafaka katika kujitathmini na kuhakikisha nafanya kazi zangu kwa weledi

wa hali ya juu wakati wote, ikiwemo wakati wa faragha.

Naahidi kulinda heshima ya asasi za uangalizi za ndani, Makundi ya Waangalizi wa

Nje ambayo ninayafanyia kazi na kufuata maelekezo yao. Nitahudhuria mikutano ya

kupata taarifa, mafunzo na kutoa taarifa inayotakiwa. Nitashirikiana katika kuandaa

maelezo au taarifa kadiri itavyohitajika kwangu. Sitatoa taarifa, maelezo au

majumuisho yangu binafsi kwa vyombo vya habari au kwa umma kabla ya asasi

yangu ya uangalizi ya ndani au Kundi langu la Waangalizi wa Nje kutoa taarifa yake,

isipokuwa kama nitaruhusiwa au nitaelekezwa hivyo.

Page 16: Mwongozo Wa Waangalizi Wa Uchaguzi Zanzibar

15

Jina : ______________________Wadhifa : ____________________

Taasisi ya Uangalizi : ______________________________________

Uraia: __________________________________________________

Saini: ________________________

Tarehe:_____________________