41
1 RIPOTI YA KAMATI YA BAJETI YA BARAZA LAWAWAKILISHI ZANZIBAR KWA MWAKA WA FEDHA 2018/2019 SEHEMU YA KWANZA UTANGULIZI Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi ni miongoni mwa Kamati nane (8) za Kudumu za Baraza, imeundwa chini ya Kanuni ya 106 ya Kanuni za Baraza, Toleo la mwaka 2016. Aidha, majukumu yake yametajwa katika Jadweli la kwanza la Kanuni hizo. MAJUKUMU YA KAMATI YA BAJETI YA BARAZA LA WAWAKILISHI i. Kujadili na kutoa maoni na ushauri kuhusu uandaaji wa mwongozo wa kutayarisha Mpango na Bajeti ya Serikali kwa kila mwaka. ii. Kufuatilia na kusimamia utekelezaji wa Bajeti ya Serikali. iii. Kufanya utafiti na uchambuzi kuhusu sera za kodi, sera za fedha na sera za kiuhasibu zilizopendekezwa na Serikali. iv. Kujadili na kutoa maoni na ushauri kuhusu vyanzo vya mapato ya Serikali, na mapendekezo ya hatua za kupunguza utegemezi wa kibajeti. v. Kutoa ushauri wa jumla kuhusu Bajeti ya Serikali kwa Baraza na Kamati za Kudumu za Baraza. vi. Kuchambua na kutoa maoni na ushauri kuhusu Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaopendekezwa na Serikali. vii. Kuchambua hoja zitakazojitokeza kwenye Kamati za Kudumu za Baraza wakati wa kujadili Bajeti za Wizara kwa ajili ya kuishauri Serikali. viii. Kuchambua Mapendekezo ya Jumla ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi. ix. Kufikiria na kuchunguza Mswada wa Makadirio ya Mapato na matumizi ya mwaka.

RIPOTI YA KAMATI YA BAJETI YA BARAZA LAWAWAKILISHI ... · Kuhusiana na deni la taifa, hadi kufikia Febuari, 2019 deni lilifikia TZS 444.480 bilioni lilojumuisha deni la ndani TZS

  • Upload
    others

  • View
    15

  • Download
    0

Embed Size (px)

Citation preview

1

RIPOTI YA KAMATI YA BAJETI

YA BARAZA LAWAWAKILISHI ZANZIBAR

KWA MWAKA WA FEDHA 2018/2019

SEHEMU YA KWANZA

UTANGULIZI

Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi ni miongoni mwa Kamati nane (8) za Kudumu za

Baraza, imeundwa chini ya Kanuni ya 106 ya Kanuni za Baraza, Toleo la mwaka 2016.

Aidha, majukumu yake yametajwa katika Jadweli la kwanza la Kanuni hizo.

MAJUKUMU YA KAMATI YA BAJETI YA BARAZA LA WAWAKILISHI

i. Kujadili na kutoa maoni na ushauri kuhusu uandaaji wa mwongozo wa kutayarisha

Mpango na Bajeti ya Serikali kwa kila mwaka.

ii. Kufuatilia na kusimamia utekelezaji wa Bajeti ya Serikali.

iii. Kufanya utafiti na uchambuzi kuhusu sera za kodi, sera za fedha na sera za kiuhasibu

zilizopendekezwa na Serikali.

iv. Kujadili na kutoa maoni na ushauri kuhusu vyanzo vya mapato ya Serikali, na

mapendekezo ya hatua za kupunguza utegemezi wa kibajeti.

v. Kutoa ushauri wa jumla kuhusu Bajeti ya Serikali kwa Baraza na Kamati za Kudumu

za Baraza.

vi. Kuchambua na kutoa maoni na ushauri kuhusu Mpango wa Maendeleo wa Taifa

unaopendekezwa na Serikali.

vii. Kuchambua hoja zitakazojitokeza kwenye Kamati za Kudumu za Baraza wakati wa

kujadili Bajeti za Wizara kwa ajili ya kuishauri Serikali.

viii. Kuchambua Mapendekezo ya Jumla ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na

Matumizi.

ix. Kufikiria na kuchunguza Mswada wa Makadirio ya Mapato na matumizi ya mwaka.

2

x. Kuchambua mapendekezo ya Serikali endapo itataka kuwasilisha katika Baraza

Mswada wa Matumizi ya Nyongeza kwa mujibu wa Kanuni ya 101 ya Kanuni za

Baraza.

xi. Kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Kamati yaliyotolewa kwenye Ripoti ya Kamati

ya mwaka uliotangulia na kutathmini taarifa ya Wizara juu ya utekelezaji wa maagizo

hayo na kuwasilisha Barazani maoni ya Kamati kuhusu taarifa hiyo.

MUUNDO WA KAMATI:

Kamati ya Bajeti imeundwa na Wajumbe saba na Makatibu wanne (4) kama ifuatavyo:

1. Mhe. Mohamed Said Mohammed Mwenyekiti

2. Mhe. Bahati Khamis Kombo M/Mwenyekiti

3. Mhe. Mohammedraza Hassanali Mjumbe

4. Mhe. Salha Mohamed Mwinjuma Mjumbe

5. Mhe. Abdalla Ali Kombo Mjumbe

6. Mhe. Asha Abdalla Mussa Mjumbe

7. Mhe. Simai Mohammed Said Mjumbe

8. Ndg. Abdalla Ali Shauri Katibu

9. Ndg. Asha Said Mohamed Katibu

10. Ndg. Kassim Tafana Kassim Katibu

11. Ndg. Shaib Fadhil Shaib Katibu

3

SEHEMU YA PILI

UTEKELEZAJI WA KAZI ZA KAMATI

Kwa mwaka wa Fedha 2018/2019, Kamati ya Bajeti imefanya kazi mizunguko mitatu,

mzunguko wa kwanza ulianzia tarehe 20/08/2018 hadi tarehe 31/08/2018 ambapo Kamati

ilifanya kazi Unguja na katika mzunguko wa pili, pia Kamati ilifanya kazi Unguja kuanzia

tarehe 05/11/2018 hadi tarehe 13/11/2018 na kwa Dar es Salaam ilifanya kazi kuanzia tarehe

14/11/2018 hadi tarehe 16/11/2018. Aidha, katika mzunguko wa tatu Kamati ilifanya kazi

Unguja kuanzia tarehe 14/01/2019 hadi tarehe 25/01/2019.

Kamati katika kutekeleza majukumu yake ilikutana na Wizara na Taasisi mbali mbali za

Serikali, Wadau na kufanya vikao na Wawekezaji wa Sekta ya Utalii na Hoteli, wazalishaji

wa vinywaji visivyo na kilevi na baadhi ya wafanyabiashara. Lengo la vikao hivyo ni kujadili

mambo yanayohusiana na uwekezaji, biashara, mfumo wa kodi na kupata maoni yao katika

kuimarisha maeneo hayo na hata kusaidia kutatua changamoto mbali mbali zinazowakabili.

Afisi kwa kushirikiana na Kamati, ilizingatia suala la kuwapatia mafunzo wajumbe kwa

lengo la kuwajengea uwezo na kukuza uelewa mpana wa mambo mbali mbali. Hivyo, Kamati

pamoja na mambo mengine, ilipata fursa ya mafunzo yanayohusiana na uchambuzi wa Deni

la Taifa, uchambuzi wa mswada wa fedha na kodi na Mafunzo kuhusiana na Uandaaji,

Uchambuzi na Usimamizi wa Bajeti kwa Mfumo wa Programu (PBB).

MAENEO YALIYOFANYIWA KAZI NA KAMATI YA BAJETI

1. Kupokea taarifa ya utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kwa kipindi cha Januari –

Februari 2017/2018, Aprili – Juni 2017/2018, Julai – Septemba, 2018/2019 na

Octoba – Disemba, 2018/2019.

2. Mamlaka ya Kuendeleza Viwanda vidogo vidogo na vya kati (Small and Medium

Industrial Development Authority – SMIDA)

3. Mradi wa Uwanja wa Ndege wa Abeid Amaan Karume ( Terminal III)

4. Kiwanda cha Sukari – Mahonda

5. Mamlaka ya Udhibiti wa Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar

(ZPRA)

6. Mahkama Kuu – Zanzibar

4

7. Mradi wa Mahkama Kuu - Tunguu

8. Eneo la Kuhifadhia Mafuta na Gesi na Ujenzi wa Bandari ukanda wa Mangapwani –

Bumbwini

9. Mradi wa Ujenzi wa Bandari ya Mpiga Duri

10. Mradi wa Kiwanda cha Kuzalisha Maziwa – Fumba

11. Ziara ya Kamati ya Bajeti Tanzania bara

12. Shirika la Bima - Zanzibar

13. Shirika la Umeme - Zanzibar

14. Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF)

15. Kikao cha Pamoja Baina ya Kamati na Wafanyabiashara

16. Kikao cha Pamoja Baina ya Kamati na Wawekezaji wa Sekta ya Utalii na Mahoteli

17. Kikao cha Pamoja Baina ya Kamati na Wawekezaji wa Viwanda vya Vinywaji

Visivyo na Kilevi.

TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA SERIKALI ROBO YA TATU

(JANUARI – FEBRUARI 2017/2018)

Mapato

Kwa kipindi cha Januari - Februari, 2017/2018, Serikali ilipanga kukusanya jumla ya TZS

122.351 bilioni kutokana na vianzio vya ndani ambapo ZRB ilikadiriwa kukusanya TZS

64.980 bilioni, TRA TZS 42.803 bilioni, mapato yasiyo ya kodi TZS 11.068 bilioni na PAYE

TZS 3.3 bilioni. Aidha, Serikali ilikadiria kupokea jumla ya TZS 13.005 bilioni kutoka kwa

Washirika wa Maendeleo.

Katika kipindi hichi, utekelezaji halisi kwa Januari – Febuari, 2017/2018, kwa upande wa

mapato ya ndani yalifikia TZS 125.930 bilioni ambazo ni sawa na asilimia 103 ya makadirio

yaliyopangwa. Jumla ya TZS 30.121 bilioni zilipokelewa kutoka kwa washirika wa

maendeleo.

Matumizi

Kwa upande wa matumizi katika kipindi cha Januari - Febuari, 2017/2018, Serikali ilikadiria

TZS 133.328 bilioni, ambapo TZS 117.114 bilioni ni matumizi ya kawaida na TZS 16.214

bilioni ni matumizi kwa kazi za maendeleo. Aidha, fedha kwa miradi iliyochangiwa na

washirika wa maendeleo ilikadiriwa kuwa TZS 28.208 bilioni.

Utekelezaji halisi kwa upande wa matumizi kwa kipindi Januari – Febuari, 2017/2018 ulifikia

TZS 141.685 bilioni ya makadirio yaliyopangwa.

5

Deni la Taifa

Kuhusiana na deni la taifa, hadi kufikia Febuari, 2019 deni lilifikia TZS 444.480 bilioni

lilojumuisha deni la ndani TZS 162.870 bilioni na deni la nje ni TZS 281.610 bilioni. Sababu

za kuongezeka kwa deni la ndani ni pamoja na kuongezeka kwa madeni ya wazabuni, mkopo

wa hati fungani na kuongezeka kwa madeni ya kiinua mgongo. Kwa upande wa deni la nje,

miongoni mwa sababu za kuongezeka kwake ni kutokana na kushuka kwa thamani ya

shilingi ya Tanzania.

TATHMINI YA KAMATI JUU YA TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA

SERIKALI KWA KIPINDI CHA (JANUARI-FEBRUARI) 2017/2018)

1. Kwa kipindi cha Januari – Febuari 2017/2018, mapato ya Serikali yameongezeka na

kupindukia lengo la makadirio na kufikia TZS 125.930 bilioni ambazo ni sawa na

asilimia 103 ya makadirio yaliyopangwa. Hali hii inaonesha ishara nzuri katika

jitihada za kukuza mapato ya Serikali na kupunguza utegemezi wa Bajeti kutoka kwa

washirika wa maendeleo.

2. Deni la taifa limeendelea kukua siku hadi siku licha ya Kamati kuarifiwa kuwa Deni

hilo ni himilivu. Hadi kufikia mwishoni mwa mwezi wa Febuari 2018 deni

liliongezeka hadi kufikia jumla ya TZS 444.5 bilioni ikilinganishwa na deni la TZS

374.6 bilioni la mwezi wa Februari mwaka 2017 sawa na ongezeko la asilimia 18.

3. Kwa kipindi cha miezi miwili Januari – Febuari, 2017/2018, jumla ya TZS 141.68

zimetumika. Matumizi haya ni makubwa ukilinganisha na mapato halisi

yaliyokusanywa katika kipindi hicho ambayo ni TZS 125.93 bilioni.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kwa kuwa Serikali ina vyanzo mbali mbali vya mapato na ina uwezo wa kufanya

matumizi kwa mujibu wa programu na miradi iliyojipangia kwa kipindi husika cha

mwaka wa fedha, Kamati inaishauri Serikali iweke mkazo zaidi katika kudhibiti

uvujaji wa mapato kwa kuzingatia kuwa, matumizi yanayofanyika ni kwa mujibu wa

malengo na mapato yaliyopo.

2. Pamoja na uhimilivu wa Deni la Taifa kama Kamati ilivyoelezwa, Kamati inaishauri

Serikali ihakikishe deni hilo haliongezeki kwa kasi na kuathiri mwenendo wa uchumi.

Aidha, taarifa za deni la taifa zipatikane kwa wakati kwa vyombo husika ikiwemo

Benki Kuu ya Tanzania tawi Zanzibar ili vyombo hivyo viwe na taarifa sawa.

6

TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA SERIKALI ROBO YA NNE

(APRILI – JUNI 2017/2018)

Kamati ya Bajeti ilipokea taarifa ya utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kwa kipindi cha Aprili –

Juni 2017/2018, ambapo kwa kipindi hicho Kamati iliarifiwa kwamba Serikali ilikadiria

kukusanya jumla ya TZS 183.9 bilioni ikijumuisha TZS 160.8 bilioni kutoka vyanzo vya

ndani, TZS 9.6 bilioni mapato kutoka nje na 13.5 bilioni ni gawio la faida kutoka Benki Kuu

ya Tanzania. Makusanyo halisi kwa kipindi cha miezi mitatu (Aprili – Juni ) ni TZS 224.5

bilioni ambazo ni sawa na asilimia 122 ya matarajio, ikijumuisha makusanyo ya ndani

yaliyofikia Tsh 167.6 bilioni na mapato mengineyo TZS 56.9 bilioni ikiwemo gawio la faida

kutoka Benki Kuu TZS 13.5 bilioni na mapato kutoka nje Tsh 43.4 bilioni.

Kwa kipindi cha robo ya nne ya mwaka wa fedha 2017/18, matumizi halisi yalifikia jumla ya

TZS 222.6 bilioni, yakijumuisha matumizi ya vyanzo vya ndani ya jumla ya TZS 186.8

bilioni na TZS 35.8 bilioni kutoka kwa washirika wa maendeleo. Ikilinganishwa na kipindi

kama hicho mwaka 2016/17 kumejitokeza ongezeko la matumizi la asilimia 36 kutoka TZS

164.3 bilioni. Kati ya matumizi hayo, TZS 153.2 bilioni zimetumika kwa matumizi ya

kawaida sawa na asilimia 93 ya lengo.

Deni la taifa limeongezeka kwa asilimia 26 kutoka TZS 405.5 bilioni kwa kipindi cha Aprili

Juni 2016/2017 hadi kufikia TZS 512.5 Aprili –Juni 2017/2018.

Mfumko wa Bei kwa nchi za Afrika Mashariki.

Kasi ya mfumko wa bei kwa nchi za kwa nchi za Afrika Mashariki ulipungua na kufikia

wastani wa asilimia 2.2 kwa kipindi cha Aprili – Juni, 2018 ikilinganishwa na kipindi kama

hicho kwa mwaka 2017 ambapo kasi ya mfumko wa bei ilikuwa 9.1. Kwa mujibu wa

takwimu, nchi iliyoripotiwa kuwa na kasi ndogo ya mfumko wa bei ni Rwanda ambapo

ulifikia wastani wa asilimia 1.4 mwaka 2018 ikilinganishwa na wastani wa 9.4 kwa kipindi

2017.

Utalii

Katika kipindi cha robo ya nne ya mwaka 2018, idadi ya watalii imeongezeka kwa wastani

wa asilimia 26.8 na kufikia watalii 76,304 ikilinganishwa na watalii 60,158 kwa kipindi cha

April – Juni, 2017.

7

TATHMINI YA KAMATI JUU YA TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA

SERIKALI ROBO YA NNE (APRIL – JUNI 2017/2018)

Kamati ilichambua na kutathmini taarifa ya Bajeti kwa kipindi cha Aprili – Juni 2017/2018

na miongoni mwa mambo ya msingi ambayo Kamati imeyabaini katika taarifa hiyo ni kama

ifuatavyo:

1. Katika robo ya nne ya utekelezaji wa Bajeti ya Serikali, upatikanaji wa fedha za

misaada ya kibajeti pamoja na mikopo kutoka kwa wafadhili uliridhisha na hivyo

kusaidia sana utekelezaji wa shughuli za maendeleo ambazo ni msingi muhimu katika

ukuaji wa Uchumi.

2. Baadhi ya nchi za Afrika Mashariki ikiwemo Rwanda zimeweza kudhibiti kwa kiasi

kikubwa mfumko wa bei kutokana na kuimarisha uzalishaji wake wa ndani.

3. Kamati imepata changamoto ya kutojua taarifa za fedha halisi zinazotokana na

shughuli za Utalii, ambapo licha ya idadi ya watalii kuongezeka, Kamati hukosa

taarifa za fedha zinazoongezeka katika sekta ya utalii kutokana na ongezeko la idadi

ya watalii hao.

4. Deni la Taifa limeendelea kuongezeka kwa kasi licha ya Kamati kuarifiwa kwamba

deni hilo ni himilivu. Kamati imegundua ongezeko la deni la taifa haliendi sambamba

na ufanisi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Ili kukabiliana na tatizo la kupanda kwa mfumko wa bei hususan wa bidhaa za

chakula na athari zake kiuchumi, Kamati inaishauri Serikali kuongeza juhudi katika

kuimarisha uzalishaji wa ndani ili kudhibiti kasi ya mfumko huo.

2. Kutokana na kutofahamika thamani halisi ya fedha zinazotokana na ongezeko la

watalii, Kamati inaishauri Serikali kutafuta mfumo utakaowezesha kujua thamani

halisi ya fedha inayotokana na sekta ya utalii ili kusaidia katika kutathmini na kuweka

mikakati ya kuikuza zaidi sekta hiyo pamoja na kutoa taswira halisi ya mchango wa

sekta hiyo katika uchumi wa Zanzibar.

3. Kutokana na kasi kubwa ya kuongezeka deni la taifa, Kamati inaishauri Serikali

iweke mikakati ya kupunguza kasi ya ukuaji wa deni hilo kwa kuimarisha mapato ya

8

ndani na kuhakikisha kuwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo uliotokana na fedha

za mikopo unakwenda kwa mujibu wa malengo na muda uliokusudiwa.

TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA SERIKALI KWA KIPINDI CHA

ROBO YA KWANZA (JULAI –SEPTEMBA 2018/2019)

Kamati ya Bajeti ilipokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kwa kipindi

cha robo ya kwanza (Julai – Septemba 2018/2019) ambayo ilijumuisha taarifa ya mwenendo

wa Uchumi wa Zanzibar, mwenendo wa uchumi wa dunia na kanda, ukusanyaji wa mapato

ya Serikali na matumizi pamoja na taarifa kuhusu deni la taifa.

Mapato

Serikali ilipanga kukusanya jumla ya TZS 222.5 bilioni, TZS 189.5 bilioni kutokana na

mapato ya ndani na TZS 33.0 bilioni kutokana na mapato ya nje. Aidha katika ukusanyaji

halisi Serikali ilifanikiwa kukusanya jumla ya TZS 196.1 bilioni sawa na asilimia 88 ya

matarajio ya kukusanya TZS 222.5 bilioni. Makusanyo hayo yalijumuisha fedha kutoka

makusanyo ya ndani ya TZS 176.6 bilioni, mapato mengineyo ya TZS 19.5 bilioni na

mapato kutoka nje TZS 19.5 bilioni. Kwa ujumla mapato yameonekana kukuwa kwa asilimia

13 kwa kulinganisha na TZS 173 bilioni zilizokusanywa kwa kipindi kama hicho kwa mwaka

2017/2018.

Matumizi

Serikali ilitumia jumla ya TZS 222.5 bilioni zilizojumuisha matumizi ya vianzio vya ndani

yaliyofikia TZS 199.6 bilioni na TZS 22.8 bilioni kutoka kwa washirika wa maendeleo.

Matumizi hayo yote ni sawa na ongezeko la asilimia 25 ya matumizi halisi ya TZS 177.5

bilioni katika kipindi kama hicho kwa mwaka 2017/2018.

Mfumko wa Bei

Mfumko wa bei kwa nchi washirika wa biashara na Zanzibar kama China, India na UAE

katika kipindi cha Julai – Septemba, 2017 umepanda kutoka asilimia 2 hadi kufikia wastani

wa asilimia 3.3 kwa kipindi kama hicho kwa mwaka 2018. Kwa upande wa Zanzibar

mfumko wa bei za chakula ulishuka hadi kufikia asilimia 3.5 kulinganisha na mfumko wa bei

wa asilimia 5.9 kwa mwezi Septemba kwa mwaka 2017. Hali hii ilitokana na kushuka kwa

bidhaa za chakula kama vile unga wa mahindi, samaki, ndizi mbichi na sukari. Aidha kwa

upande wa bidhaa zisizo za chakula mfumko wa bei umepanda hadi kufikia asilimia 6.1

kulikotokana na kuongezeka kwa bei za bidhaa za nishati ya mafuta na saruji.

9

Deni la Taifa

Deni la taifa hadi kufikia mwishoni mwa robo ya kwanza ya mwaka 2018/2019 limerikodiwa

kuwa ni TZS 469.6 bilioni ambazo ni sawa na ongezeo la asilimia 17 ikilinganishwa na deni

la TZS 401.6 bilioni lililoripotiwa katika kipindi kama hicho katika mwaka 2017/18.

TATHMINI YA KAMATI JUU YA TAARIFA YA UTEKELZAJI WA BAJETI YA

SERIKALI KWA KIPINDI CHA ROBO YA KWANZA (JULAI –SEPTEMBA

2018/2019)

1. Pamoja na kuimarika kwa uchumi wa dunia na Afrika ya Mashariki kwa sababu mbali

mbali ikiwa ni pamoja na ukuaji wa viwanda na usarifu wa mazao. Kwa upande wa

Zanzibar pamoja na kuripotiwa kuimarika kwa shughuli za uchumi na kupelekea

kuongezeka kwa kasi ya ukuaji wa uchumi kwa robo ya kwanza na ya pili

kulinganisha na ukuaji wa robo kama hiyo kwa mwaka 2017, wawekezaji wengi wa

sekta ya viwanda wanalalamikia mazingira magumu ya uwekezaji katika sekta hiyo

kutokana na kuzorota kwa uzalishaji na kukosekana soko la bidhaa za Zanzibar kwa

upande wa Tanzania Bara.

2. Kwa mujibu wa malengo ya Mkuza III mfumko wa bei Zanzibar unaonekana kuvuka

malengo ya mpango huo ambao umekadiria ifikapo mwaka 2020 kuwa na mfumko

wa bei wa asilimia 5%1.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kutokana na kupanda kwa kasi ya mfumko wa bei katika nchi washirika wa biashara

na Zanzibar kama China, UAE na India, Kamati inaishauri Serikali kupanua wigo wa

kibiashara kwa kufungua milango ya kibiashara kwa nchi nyengine, kwa lengo la

kupunguza athari za mfumko wa bei unaotokana na nchi washirika.

2. Kamati inaisisitiza Serikali kuendelea kuwa na nidhamu ya matumizi ya fedha za

umma katika miradi mikubwa ya kitaifa ambayo isiposimamiwa vyema itapelekea

kuzorota kwa uchumi wa nchi pamoja na kuongeza mzigo wa deni la taifa.

1 Zanzibar Strategy for Growth and Reduction of Poverty III, 2016-2020, pg. 79

10

TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA SERIKALI ROBO YA PILI

(OKTOBA – DISEMBA 2018/2019).

Kamati ya Bajeti katika kutekeleza majukumu yake ilipokea taarifa ya utekelezaji wa bajeti

kwa robo ya pili (Oktoba-Disemba) 2018/19, iliyohusisha mwenendo wa hali ya uchumi,

utekelezaji wa mpango wa maendeleo na utekelezaji wa Bajeti.

Mapato

Kwa kipindi cha Oktoba - Disemba, 2018/19, Serikali ilipanga kukusanya jumla ya TZS

241.8 bilioni. Kati ya fedha hizo, TZS 198.7 bilioni mapato ya ndani na TZS 43.1 bilioni

mapato ya nje. Ukusanyaji halisi wa mapato ulifikia TZS 281.8 bilioni sawa na asilimia 117

ya matarajio ya makusanyo ambapo makusanyo ya ndani yalifikia TZS 190.1 bilioni na TZS

91.7 bilioni mapato ya nje.

Matumizi

Kwa kipindi cha Oktoba – Disemba, 2018 Serikali ilikadiria kufanya matumizi jumla ya TZS

188.7 bilioni kwa kazi za kawaida na TZS 82.6 bilioni kwa kazi za maendeleo. Matumizi

halisi yalifikia jumla ya TZS 290 bilioni ambapo jumla ya TZS 207.6 bilioni kutoka vianzio

vya ndani na TZS 82.4 bilioni kutoka kwa Washirika wa Maendeleo.

Utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo

Kupitia Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2018/19, jumla ya programu 27 na miradi 55

ilitegemewa kutekelezwa. Kwa kipindi cha Oktoba – Disemba, 2018 jumla ya TZS 155.5

bilioni zilipangwa kugharamia programu na miradi ya maendeleo. Kati ya fedha hizo TZS

39.5 bilioni zilipangwa kutoka Serikalini na TZS 116.02 bilioni zilipangwa kutoka kwa

washirika wa maendeleo. Hadi kufikia Disemba 2018, jumla ya TZS 97.6 bilioni sawa na

asilimia 63 zilipatikana kugharamia programu na miradi ya maendeleo.

Ukuaji wa Pato la Taifa

Kamati ilielezwa kuwa uchumi wa Zanzibar umeendelea kuwa imara ambapo kwa mwaka

2017 ulifikia wastani wa asilimia 7.7 ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 5.8 kwa mwaka

2016. Ukuaji huo ulitokana na kuongezeka kwa uzalishaji wa ndani ya nchi wa bidhaa na

huduma. Sekta zilizochangia katika ukuaji huo ni Sekta ya Kilimo, Viwanda na Huduma.

11

Mfumko wa Bei

Kwa mwaka wa 2018, kasi ya mfumko wa bei za bidhaa na huduma ulishuka na kufikia

wastani wa asilimia 3.9 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 5.6 mwaka 2017. Hali hii

ilitokana na kushuka kwa mfumko wa bei za bidhaa za chakula ambapo kwa mwaka 2018

ulifikia asilimia 1.4 ikinganishwa na asilimia 5.5 kwa mwaka 2017.

Kwa upande wa bidhaa zisizo za chakula nazo ziliendelea kushuka kidogo. Takwimu

zinaonesha kuwa, kwa mwaka 2018 mfumko wa bei zisizo za chakula zilifikia asilimia 5.7

ikilinganishwa na asilimia 5.8 mwaka 2017.

Utalii

Katika kipindi cha Oktoba – Disemba 2018, Sekta ya Utalii iliendelea kufanya vizuri na

kupelekea kuongezeka kwa idadi ya watalii wanaoingia nchini kutoka watalii 130,945 katika

kipindi cha mwaka 2017 na kufikia watalii 142,337 kwa mwaka 2018. Kamati iliarifiwa

kuwa, miongoni mwa sababu zilizopelekea ongezeko hilo ni pamoja na kuwepo kwa vivutio

vya watalii kama vile matamasha ya sanaa na utamaduni na kuwepo kwa ndege za moja kwa

moja za kuwaleta watalii nchini.

Thamani ya Shilingi

Kwa kipindi cha mwaka 2018 Shilingi ya Tanzania ilibadilishwa na dola ya kimarekani kwa

wastani wa TZS 2,264 ikilinganishwa na wastani wa TZS 2,229 katika kipindi kama hicho

kwa mwaka 2017. Takwimu hizo zinaonesha kuwa Shilingi ya Tanzania ilishuka thamani

kidogo dhidi ya dola ya Kimarekani.

Mwenendo wa Sekta za Kibenki

Kamati ilielezwa kuwa, kwa kipindi cha Oktoba - Disemba 2018, sekta za kibenki

zimeendelea kufanya vizuri na kumekuwa na ongezeko la kuweka akiba kutoka kwa wateja

uliofikia TZS 847.8 bilioni ikilinganishwa na TZS 737.6 bilioni kwa kipindi kama hicho kwa

mwaka 2017, na pia ongezeko la mikopo kwenda kwa wateja wake binafsi na

wafanyabiashara. Kufanya vizuri kwa sekta za kibenki kumetokana na kuongezeka na

kukuwa kwa shughuli za kiuchumi.

Sekta za Nje

Katika kipindi cha Oktoba – Disemba 2018, Kamati iliarifiwa juu ya kuongezeka kwa

uagiziaji wa bidhaa na huduma nje ya nchi na kupelekea nakisi kufikia jumla ya TZS 20.6

12

bilioni (Januari – Juni) 2018 ikilinganishwa na nakisi ya TZS 11 bilioni mwaka 2017.

Ongezeko la nakisi hiyo limetokana na usafirishaji mdogo wa karafuu ambapo ununuzi wa

zao hilo umepungua na kufikia tani 54.6 zenye thamani ya TZS 262.8 milioni mwaka 2018

kutoka tani 5790.7 zenye thamani ya TZS 80,697.6 milioni katika kipindi cha mwaka 2017.

Deni la Taifa

Kwa kipindi cha Oktoba – Disemba 2018/19, Deni la taifa limeripotiwa kufikia TZS 779.0

bilioni sawa na ongezeko la asilimia 99 ukilinganisha na deni la TZS 391.8 bilioni

lililoripotiwa kwa kipindi kama hicho kwa mwaka 2017/18.

TATHMINI YA KAMATI JUU YA TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA

SERIKALI KWA ROBO YA PILI (OKTOBA – DISEMBA 2018/2019)

1. Kwa kipindi cha Januari – Juni, 2018 uchumi wa Zanzibar uliendelea kuimarika

ambapo sekta zilizochangia katika ukuaji huo ni pamoja sekta ya viwanda asilimia

(16.9), mawasiliano (10.4), fedha na bima (9.1), ujenzi (49.8) na sekta ya uchimbaji

mawe na mchanga (16.7).

2. Kamati imebaini kushuka kwa kasi ya mfumko wa bei za bidhaa na huduma kwa

mwaka 2018 sambamba na kushuka kidogo kwa bidhaa zisizo za chakula.

3. Kamati imebaini kuongezeka kwa miradi mipya (14) kwa kipindi cha 2018/19 licha

ya kuwa na idadi kubwa ya miradi (41) ya zamani ambayo Serikali inatakiwa

kuendeleza utekelezaji wake.

4. Kamati imebaini ongezeko kubwa la Deni la Taifa ambapo limefikia TZS 779.0

bilioni sawa na ongezeko la asilimia 99 ikilinganishwa na deni la TZS 391.8 bilioni

liloripotiwa kwa kipindi kama hicho kwa mwaka 2017/18.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kwa kuwa takwimu zinaonesha uchumi wa Zanzibar uliendelea kuimarika ambapo

kwa mwaka 2017 ukauaji wa pato la taifa ulifikia wastani wa asilimia 7.7

ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 5.8 kwa mwaka 2016, katika kuhakikisha kuwa

ukuaji huu unamnufaisha mwananchi moja kwa moja , Kamati inaishauri Serikali,

pamoja na kutumia pato la taifa kuwa ni kipimo cha maendeleo, ihakikishe inapanga

sera za uchumi na kijamii zinazoweza kupima maendeleo na ustawi wa watu wengi

katika jamii kwa kuangalia mabadiliko yaliyopo katika jamii.

13

2. Kwa kipindi cha Januari - Juni 2018, Kamati imebaini mafanikio ya kiuchumi

yaliyochangiwa na sekta ya viwanda (16.9), mawasiliano (10.4), fedha na bima (9.1),

ujenzi (49.8) na sekta ya uchimbaji mawe na mchanga (16.7). Licha ya mafanikio ya

kiuchumi yaliyofikiwa kupitia sekta mbali mbali, Kamati inaishauri Serikali

kuishirikisha ipasavyo sekta binafsi na kuwa na takwimu za mchango wao katika

uchumi kwani sekta binafsi ina mchango mkubwa na muhimu katika kuinua uchumi

wa nchi.

3. Kamati inaishauri Serikali kuandaa mikakati madhubuti katika kudhibiti bei za bidhaa

na huduma ambazo zitazingatia maslahi ya mfanyabiashara pamoja na mtumiaji bila

ya kumkandamiza yeyote.

4. Kwa kipindi cha Oktoba – Disemba, 2018, Kamati imebaini ongezeko la mapato,

matumizi na deni la taifa. Katika kuhakikisha kuwa ongezeko la mapato, matumizi na

deni la taifa vinakuwa na tija katika ustawi wa nchi, Kamati inaishauri Serikali

kuhakikisha kuwa, matumizi yanayofanywa yanakwenda sambamba na malengo ya

bajeti kama yalivyoidhinishwa na kuhakikisha kuwa fedha zinazotokana na mikopo

zinatumika vyema ili kuondokana na mzigo wa madeni kwa vizazi vya sasa na

vijavyo.

MAMLAKA YA KUENDELEZA VIWANDA VIDOGO VIDOGO NA VYA KATI

(SMALL AND MEDIUM INDUSTRIAL DEVELOPMENT AUTHORITY – SMIDA)

Kuwepo kwa viwanda vya aina mbali mbali katika nchi ni moja wapo ya njia muhimu za

kuchochea uchumi wa nchi. Uzoefu unaonesha kuwa nchi nyingi ambazo zimejiimarisha

katika viwanda zimepiga hatua kubwa za maendeleo. Umuhimu wa viwanda unadhihirika

kwa wananchi kutokana na faida zinazotokana na viwanda hivyo, ikiwa ni pamoja na

upatikanaji wa bidhaa muhimu kwa bei nafuu zaidi badala ya kuagiza bidhaa hizo kutoka

nchi za nje. Aidha, viwanda ni kichocheo muhimu katika upatikanaji wa ajira kwa wananchi.

Serikali katika kuhakikisha kuwa inaendeleza viwanda ikiwa ni moja wapo ya hatua ya

utekelezaji wa malengo ya Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya 2020 (vision 2020) ya

kuwawekea mazingira mazuri ya uwekezaji na kuwasaidia wajasiriamali wadogo wadogo na

wa kati (Micro, Small and Medium Enterprises – MSMEs) imeanzisha Mamlaka ya

Kuendeleza Viwanda Vidogo Vidogo na vya Kati (SMIDA).

14

Miradi midogo midogo ya wajasiriamali inachukuwa nafasi kubwa katika kukuza uchumi wa

Zanzibar. Katika kufanikisha maendeleo ya miradi ya wajasiriamali wadogo wadogo, uzoefu

unaonesha kuwa, sekta ya viwanda inahitaji uratibu na usimamizi mzuri kwa ajili ya kusaidia

ukuajia endelevu wa sekta hiyo pamoja na kutoa nafasi za ajira ambazo zitachangia katika

ukuaji wa uchumi.

CHANGAMOTO ZA MAMLAKA YA KUENDELEZA VIWANDA VIDOGO

VIDOGO NA VYA KATI

1. Fedha ni changamoto kubwa ya Mamlaka katika kufikia malengo ya utekelezaji wa

majukumu yake kutokana na ukweli kwamba Sheria ya kuanzisha Mamlaka,

haikuweka vianzio vya mapato na hivyo kupelekea Mamlaka kuitegemea Serikali

moja kwa moja kama chanzo kikuu cha fedha.

2. Kamati imebaini Mamlaka ina upungufu wa wafanyakazi katika nyanja za ufundi,

utawala, masoko, fedha na biashara.

3. Miongoni mwa malengo ya Mamlaka ni kuwa na eneo lisilopungua hekta nne kwa

ajili ya shughuli za viwanda vidogo vidogo na vya kati katika kila Wilaya ya

Zanzibar, katika kulifikia lengo hilo, Mamlaka inahitaji kutafuta na kubainisha

maeneo kwa Wilaya zote, hata hivyo hadi Kamati ilipotembelea Mamlaka hiyo,

maeneo hayo bado hayajapatikana.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Katika kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wa fedha kwa lengo la kutekeleza

majukumu yake kama yalivyokusudiwa, Mamlaka Viwanda Vidogo vidogo inatakiwa

kubuni na kufikiria vianzio vyengine vya mapato ikiwa ni pamoja na kuanzisha

mahusiano na taasisi za nje ya nchi ambazo zitakuwa na majukumu yanayofanana na

Mamlaka, ambapo kupitia mahusiano hayo Mamlaka inaweza kupata fursa za ufadhili

pamoja na kupata uzowefu wa kazi.

2. Kamati inaisisitiza Mamlaka kwa kushirikiana na Wizara ya Biashara na Viwanda juu

ya upatikanaji wa wafanya kazi katika nyaja mbali mbali ili ujuzi wa wafanyakazi hao

utumike katika kutekeleza kazi za Mamlaka.

3. Kwa kuwa hatua za awali zinasisitiza upatikaji wa ardhi kwa eneo lisilopungua hekta

nne kwa ajili ya shughuli za viwanda vidogo vidogo katika kila Wilaya za Zanzibar,

15

Kamati inaisisitiza, Mamlaka itatafute maeneo yenye uhakika na yasiyo na migogoro

ili shughuli za viwanda vidogo vidogo ziweze kufanyika kwa ufanisi.

MRADI WA UJENZI WA UWANJA WA NDEGE WA ABEID AMAAN KARUME

(TERMINAL III)

Kamati katika utekelezaji wa majukumu yake, ilitembelea mradi wa ujenzi wa uwanja wa

ndege wa Abeid Amaan Karume (terminal III) ulioanza utekelezaji wake tokea Julai, 2010

ambapo Mkataba wa Ujenzi huo ulikuwa Baina ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia

Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji na Kampuni ya Beijing Construction

Engineering Group (BCEG) ya China uliotiwa saini mwaka 2009 ukigharimu jumla ya USD

70.4 milioni zilizotolewa na Benki ya Exim ya China kwa ajili ya ujenzi wa uwanja huo.

Mradi huo unakabiliwa na changamoto mbali mbali na lengo la Kamati kufanya ziara ya

mradi ni kuzifahamu changamoto hizo na kuishauri Serikali ipasavyo katika kuzitafutia

ufumbuzi.

CHANGAMOTO ZA MRADI WA UWANJA WA NDEGE WA ABEID AMAAN

KARUME (TERMINAL III)

1. Kutokusainiwa kwa mkataba wa fedha (Financing Agreement) kwa ajili ya fedha za

ziada USD 58 milioni. Licha ya kuwa rasimu ya mkataba huo tayari

imeshawasilishwa Wizara ya Fedha na Mipango ya Tanzania lakini rasimu hiyo

haijasainiwa mpaka muda ambao Kamati ilikuwa inafanya kazi. Miongoni mwa

sababu zilizopelekea kutokusainiwa kwa rasimu hiyo ni Kamati ya Kitaifa ya

Uidhinishaji wa Mikopo kutokubali baadhi ya masharti, hali inayoweza kupelekea

kusimama tena kwa kazi za ujenzi.

2. Kamati inapata wasiwasi juu ya aina ya mikataba ambayo Serikali inaingia na

wakandarasi hasa panapotokea kasoro za utekelezaji wa mradi husika na kupelekea

kuongezeka kwa gharama au kukwama kwa mradi, kama ilivyotokea katika ujenzi wa

Terminal III ambapo Serikali iliamua kuendelea na kampuni hiyo hiyo bila ya

kufanya maamuzi ya kutoendelea na kampuni hiyo ambayo imesababisha kasoro

katika utekelezaji wa mradi huo.

16

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kwa kuwa mkataba wa fedha za ziada wa ujenzi wa Terminal III haujasainiwa na

kutosainiwa kwake kunaweza kuleta athari kubwa katika utekelezaji wa mradi,

Kamati inaishauri Serikali kupitia Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji wa Mikopo,

kuendelea kufuatilia na kuhakikisha kuwa mkataba huo unasainiwa kwa haraka ili

kazi za ujenzi ziendelee kama zilivyokusudiwa.

2. Kamati inaishauri Serikali kuwa na usimamizi madhubuti wa maeneo ya ardhi ikiwa

ni pamoja na kuyatambua mapema maeneo yanayotarajiwa kuekezwa miradi ili

kuepukana na gharama za kulipa fidia wananchi wanaojenga katika sehemu hizo.

3. Kamati inaishauri Serikali kuwa makini na mikataba wanayoingia na wakadarasi

pamoja na usimamizi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa kuzingatia kuwa

fedha za miradi hiyo ni za mikopo na kutokufanikisha utekelezaji wake ni hasara kwa

nchi.

KIWANDA CHA SUKARI MAHONDA

Mnamo mwaka 1965, Serikali kwa kuona umuhimu wa kuwa na mashirika, ilianzisha Shirika

la Sukari na Manukato kupitia Kiwanda cha Sukari - Mahonda kwa ajili ya uzalishaji wa

sukari, manukato na vinywaji vikali, kufuatia makubaliano ya kibiashara (The Trade

Agreement) baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya watu wa

China. Ujenzi wa kiwanda hichi na utayarishaji wa mashamba yaliyokuwa na ukubwa wa

ekari 6529.23 katika maeneo ya Kitope - Mahonda, Chechele, Panga Tupu na Upenja ulianza

rasmin mnamo mwaka 1971 na kiwanda kilianza uzalishaji mwaka 1973 chini ya Serikali ya

Mapinduzi ya Zanzibar kwa mkopo kutoka Jamhuri ya Watu wa China.

Kamati ilipata fursa ya kutembelea Kiwanda cha Sukari - Mahonda na kuona marekebisho

makubwa yaliyofanywa ikiwa ni pamoja na kufungwa mashine mpya inayotumia teknolojia

ya kisasa kwa lengo la kuongeza uzalishaji kutoka kukamua tani 400 za miwa kwa siku hadi

kufikia tani 800 mpaka tani 1250 kwa siku. Marekebisho hayo yamefanya uwekezaji katika

kiwanda hicho kufika dola za kimarekani milioni 35. Kwa ujumla mpaka Kamati ilipofanya

ziara, kiwanda kilikuwa katika hali nzuri kimiundo mbinu na vifaa.

17

CHANGAMOTO ZA KIWANDA CHA SUKARI MAHONDA

1. Ardhi iliyopo ni finyu kwa ajili ya upandaji wa miwa, Kamati iliarifiwa kiwanda kina

ekari 3,900 tu ambazo zinatumika na kuvunwa miwa kati ya ekari 10,000 ambazo ni

mahitaji halisi ya kiwanda hicho. Changamoto hii ni ya muda mrefu na imewahi

kutolewa agizo na Mhe. Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi

kuwa, kiwanda kipatiwe ekari 3,000 kama mkataba wa kiwanda hicho unavyoelekeza

na mahitaji kwa ujumla, lakini mpaka Kamati inafanya ziara katika kiwanda cha

Mahonda ni ekari 732 ndio zimekabidhiwa.

2. Kukosa kibali cha kuuza sukari inayozalishwa katika Kiwanda cha Sukari Mahonda

kwa upande wa Tanzania bara. Kutokana na ufinyu wa soko na bei ya sukari

inayozalishwa Mahonda, Kiwanda kinaendelea kuuza sukari Zanzibar pekee

kinakisababishia hasara ya shillingi 387,000 kwa kila tani moja ya sukari. Licha ya

jitihada mbali mbali bado kiwanda hakijafanikiwa kupata kibali cha kuingia katika

soko la Tanzania Bara ambako kuna bei nzuri itakayokiwezesha kiwanda kurudisha

gharama za uzalishaji.

3. Kuwepo kwa kodi kubwa ya ardhi ambapo kwa mwaka kiwanda cha sukari Mahonda

kinalipa TZS 670,000 (300 USD) kwa kila ekari moja, ambayo ni kubwa mno

ikilinganishwa na kodi ya ardhi kwa upande wa Tanzania bara ambayo ni TZS 5,000

tu kwa ekari kwa mwaka. Kimsingi kodi hii ya ardhi inaongeza gharama za uzalishaji

wa kiwanda.

4. Kutokuwepo kwa barabara zinazopitika wakati wote kuwafikia wakulima wengi zaidi

hasa wakati wa mavuno ya miwa hali inayopelekea gharama kubwa zaidi za

uendeshaji kuanzia uandaaji wa shamba mpaka uvunaji. Licha ya kiwanda kuwa na

mashamba yake, kimeanzisha mpango wa kuwatumia wakulima wa nje wa miwa

(out-growers scheme) kutoka maeneo mbali mbali kwa ajili ya kununua miwa kupitia

kilimo cha mkataba.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kamati inaishauri Serikali kuharakisha utaratibu wa upatikanaji wa eneo la ardhi

lenye ukubwa wa ekari 2268 kati ya ekari 3000 zilizoagizwa kupewa kiwanda na

Mhe. Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, kwa kuwa

18

kutopatikana kwa eneo hilo la ardhi kunapelekea kiwanda kuzalisha chini ya uwezo

kutokana na kukosekana miwa ya kutosha.

2. Kamati inaishauri Wizara ya Biashara na Viwanda, kwa kushirikiana na Uongozi wa

Kiwanda cha Sukari Mahonda kuifuatilia kwa ukaribu na kuitafutia ufumbuzi

changamoto ya Kiwanda cha Sukari - Mahonda ya kukosa kibali cha kuuza sukari

Tanzania bara.

3. Kwa kuwa Kamati imeelezwa kuwa kiwanda cha sukari Mahonda hakina unafuu wa

kodi wala ruzuku ya aina yoyote kutoka Serikalini, inayokiwezesha kuzalisha kwa

gharama nafuu, Kamati inaishauri Serikali kuandaa utaratibu maalum wa kuweka

unafuu wa kodi au ruzuku kwa lengo la kukisaidia Kiwanda cha Sukari na

kuwahamasisha wawekezaji wengine wa viwanda kuwekeza Zanzibar.

MAMLAKA YA UDHIBITI WA UTAFUTAJI NA UCHIMBAJI WA MAFUTA NA

GESI ASILIA ZANZIBAR (ZPRA)

Mamlaka ya Udhibiti wa Utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar

imeanzishwa chini ya Sheria namba ya 6 ya mwaka 2016 (Sheria ya Utafutaji na Uchimbaji

Mafuta na Gesi Asilia) ikiwa na majukumu ya msingi ya kufuatilia na kudhibiti utafutaji na

uchimbaji wa mafuta na gesi asilia, kuishauri Serikali juu ya mpango unaowasilishwa na

mkandarasi juu ya zoezi zima la uendelezaji wa eneo kwa ajili ya ujenzi wa miundo mbinu,

uzalishaji na ukomo wa shughuli za mafuta na gesi pamoja na kuhakikisha wadau wote

wanafuata Sheria za Zanzibar na mikataba ya mafuta na gesi asilia.

CHANGAMOTO ZA MAMLAKA YA UDHIBITI WA UTAFUTAJI NA UCHIMBAJI

WA MAFUTA NA GESI ASILIA ZANZIBAR (ZPRA)

1. Mamlaka inakabiliwa na uharibifu wa vifaa vya utafiti kwa ajili ya kupata taarifa za

mtetemo unaofanywa na baadhi ya wananchi na kuufanya utafiti huo kuwa wa

gharama zaidi.

2. Mamlaka inakabiliwa na ufinyu wa vifaa vya ofisini na vitendea kazi vyengine kama

gari kwa ajili ya ufuatiliaji wa shughuli zake za nje ya ofisi, ambapo mpaka Kamati

inapokea taarifa hii, iliarifiwa kuwa Mamlaka ina gari moja tu ambayo haikidhi haja

kwa shughuli zake.

19

3. Uhaba wa wafanyakazi hususan wataalam waliobobea katika sekta ya utafutaji na

uchimbaji wa mafuta na gesi asilia ambazo ni shughuli za msingi za Mamlaka.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kwa kuwa mkataba juu ya utafutaji na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi umeshatiwa

saini, Kamati inaisisitiza Mamlaka kuongeza umakini katika kusimamia mkataba huo

ili kuhakikisha zoezi la utafutaji na uchimbaji wa mafuta linafanyika kwa ufanisi.

2. Kwa kuwa Kamati imearifiwa kuwa, Bodi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Utafutaji na

Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar imeshaundwa na tayari imeshaanza

kazi, Kamati inaishauri Mamlaka iharakishe zoezi la uajiri wa wafanyakazi ili kukidhi

mahitaji ya Mamlaka.

MAHKAMA KUU - ZANZIBAR

Kamati ilifanya ziara katika ofisi za Mahkma Kuu ya Zanzibar - Vuga na kupokea taarifa ya

utekelezaji wa majukumu yake kwa mwaka wa fedha 2017/2018.

CHANGAMOTO ZA MAHKAMA KUU

1. Kamati imebaini kukosekana kwa hati miliki za baadhi ya majengo ya Mahkma

Zanzibar ikiwa ni pamoja na jengo la Mahkama Kuu - Vuga na Mahkama ya

Mfenesini hali ambayo inaweza ikasababisha matatizo iwapo majengo hayo yatahitaji

kufidiwa au iwapo kutajitokeza migogoro katika umiliki.

2. Kuchakaa kwa majengo mengi ya mahkama kwa upande wa Unguja na Pemba,

ambapo Kamati imeelezwa kuwa, kwa upande wa Pemba Mahkama ya Wete na

Chake Chake zipo katika hali mbaya. Aidha, kwa upande wa Unguja, majengo ya

Mahkama ya Mfenesini na Mkokotoni nayo yapo katika hali mbaya na yanahitaji

kufanyiwa ukarabati wa haraka.

3. Ufinyu wa bajeti ya Mahkama isiyokwenda sambamba na wingi wa taasisi za

mahkama katika ngazi za wilaya na mkoa.

4. Kukosekana kwa Ofisi ya Tume ya Mahkama na ukumbi kwa ajili ya uendeshaji wa

shughuli zake.

20

5. Kamati imeleezwa kuwa, Tume ya Mahkama haina watendaji ambao wangesaidia

katika utekelezaji wa shughuli zake. Hali hii imesababishwa na Tume hiyo kutokuwa

na fungu la fedha kwa ajili ya kuendeshea shughuli zake.

6. Upungufu wa vitendea kazi ikiwa ni pamoja na uchache wa vitabu vya kusomea na

kufanya rejea, vyombo vya usafiri na samani za ofisi kama viti na meza.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kwa kuwa majengo mengi ya Serikali hayana hati miliki, Kamati inaishauri Serikali

kuandaa mkakati maalum wa kuhakikisha majengo yote ya Serikali yanakuwa na hati

miliki kwa lengo la kuhakikisha majengo hayo yanaendelea kuwa chini ya umiliki wa

Serikali na kuepusha athari zinazoweza kujitokeza kutokana na kukosekana kwa hati

miliki hizo.

2. Kamati inaishauri Mahkama katika kukabiliana na changamoto ya uchache wa vitabu,

kuanza kutumia mfumo wa maktaba za kielectroniki (e - library ) ambao ni mfumo wa

kisasa na unanufaisha watu wengi.

3. Kwa bajeti ya mwaka 2019/2020, Kamati inaishauri Mahkama kuongeza fedha

zinazotengwa kwa ajili ya Tume ya Mahkama ili kutatua changamoto ya upungufu wa

wafanyakazi na ofisi.

4. Kamati inaishauri Wizara ya Fedha na Mipango, kwa kushirikiana na Mahkama,

kuangalia namna ya kutatua changamoto ya ufinyu wa bajeti kwa Mahkama ili

kuhakikisha shughuli zao zinafanyika kwa ufanisi zaidi.

MRADI WA MAHKAMA KUU - TUNGUU

Kamati ilitembelea eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa jengo jipya na la kisasa

la Mahkama Kuu Zanzibar unaotarajiwa kutekelezwa kupitia fedha za SMZ. Mradi huu

ulianza rasmini katika mwaka wa fedha 2016/17 chini ya Wizara ya Nchi, Afisi ya Raisi,

Katiba, Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Mnamo tarehe 19 Juni, 2017, Wizara hiyo

iliingia mkataba na Kampuni ya Landmark Consultant Ltd na kuanza kazi ya kushauri juu ya

ujenzi huo ambapo TZS 100 Milioni zilitengwa.

Katika mwaka wa fedha wa 2017/2018, Mradi huo ulihamishiwa Mahkama Kuu ambapo

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilitenga TZS 900 Milioni na katika mwaka huo wa fedha

21

jumla ya TZS 500 milioni zilipatikana kwa ajili ya maandalizi ya kuanza utekelezaji wa

mradi huo.

CHANGAMOTO ZA MRADI WA MAHKAMA KUU TUNGUU

1. Kusuasua kwa ujenzi wa Mahkama Kuu - Tunguu ambao awali ulitarajiwa

kukamilika mwaka 2020. Ujenzi huu unakabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa

hati ya eneo la mradi na uhamishwaji wa usimamizi wa mradi kutoka taasisi tofauti.

Kamati iliarifiwa kwamba, awali mradi huo ulikuwa ukisimamiwa na Wizara ya Nchi,

Afisi ya Rais, Katiba, Utumishi wa Umma na Utawala Bora na baadae ukahamishiwa

Mahkama Kuu, kwa mwaka wa fedha (2018/19) mradi huu fedha zake zimeingizwa

katika Wizara ya Fedha na Mipango kupitia fungu la Ujenzi wa Ofisi za Serikali.

2. Kutokuwepo kwa mawasiliano mazuri baina Mahkama Kuu, Wizara ya Nchi, Afisi ya

Rais, Katiba, Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Wizara ya Ardhi, Makaazi,

Maji na Nishati kulikopelekea mradi huo kukumbwa na changamoto ya kutopatikana

hati ya kiwanja kutokana na utanuzi wa barabara unaotarajiwa kufanywa na Idara ya

Barabara, hali iliyopelekea hati ya mwanzo kutofaa kwasababu ya kupungua eneo la

mradi kwa takribani mita 75.

3. Changamoto ya mkataba ambao awali ulifungwa baina ya Afisi ya Rais, Katiba,

Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Mshauri elekezi, kwa sasa mradi huo

unasimamiwa na Mahkama Kuu, hivyo kunakosekana nguvu ya moja kwa moja kwa

Mahkama kumuwajibisha mshauri elekezi iwapo kutatokea kasoro katika utekelezaji

wa mradi huo.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kamati haijaridhishwa na mwenendo wa mradi wa Mahkama Kuu Tunguu pamoja na

utaratibu wa uidhinishaji wa fedha za mradi huo ambazo zimekuwa zikihamishwa

katika mafungu (vote) tofauti, iliyopelekea kutokuwepo kwa ufanisi wa mradi.

Kamati inashauri fedha zilizotengwa za mradi ziingizwe katika fungu la Mahkama

kwa kuwa ndio wasimamizi wa mradi huo.

2. Kutokana changamoto ya utanuzi wa barabara uliopelekea eneo la mradi wa

Mahkama Kuu kupunguwa, Kamati inaishauri Serikali kuhakikisha kunakuwepo kwa

mawasiliano na mashirikiano wakati wa uandaaji na utekelezaji wa miradi, ili

22

kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa ufanisi na kuepuka gharama zisizo na

msingi.

3. Kamati inaishauri Serikali kuifanyia kazi changamoto ya kimkataba inayopelekea

usimamizi usio na ufanisi wa mradi wa ujenzi wa Mahkama Kuu ili kuondoa

changamoto hiyo na hatimae kuukamilisha mradi huo kwa ufanisi.

ENEO LA KUHIFADHIA MAFUTA NA GESI NA UJENZI WA BANDARI

UKANDA WA MANGAPWANI - BUMBWINI

Kutokana na umuhimu wa Nishati ya Mafuta na Gesi, Kamati ilitembelea Mamlaka ya

Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati (ZURA) yenye jukumu la kudhibiti huduma za maji

na nishati Zanzibar. Kamati ilipokea taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Mamlaka na

kufanya ziara katika eneo la kuhifadhia mafuta na gesi Mangapwani – Bumbwini.

Katika eneo hili lenye upana wa mita 400 kutoka ufukweni kuelekea nchi kavu limetengwa

kwa ajili ya kujengwa miundombinu itakayotumiwa na taasisi za Serikali zinazohusiana na

nishati ya mafuta na gesi na eneo jengine lenye upana wa mita 200 limepangwa kwa ajili

matumizi ya wawekezaji katika sekta ya mafuta na gesi.

CHANGAMOTO ZA ENEO LA KUHIFADHIA MAFUTA NA GESI

1. Kumekuwepo kwa baadhi ya wawekezaji wenye biashara za masuala ya mafuta na

gesi ambao wameonesha nia ya kutaka kupanua uwekezaji wao kwa kuanzisha

biashara nyengine katika eneo hilo ambazo hazina uhusiano na shughuli zilizopangwa

katika eneo hilo.

2. Kutokuwepo kwa udhibiti wa bei za gesi baina ya Zanzibar na Tanzania bara hali

inayopelekea wawekezaji wa Zanzibar kununua gesi Tanzania bara kwa bei ya juu

zaidi na kushindwa kuhimili ushindani wa kibiashara na kupanda kwa bei ya gesi

kwa wananchi.

3. Kusitishwa kwa zoezi la ulipaji fidia ya mazao (vipando) vya wananchi katika eneo la

mradi kutokana na viwango vidogo vya malipo ya fidia vilivyoelekezwa katika

Kanuni ya Mazao ya Mwaka 2013 ambayo inatokana na utekelezaji wa kifungu cha

100(1) (f) cha Sheria ya Usimamizi na Uhifadhi wa Rasilimali za Misitu Nam. 10 ya

mwaka 1996.

23

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kwa kuwa Serikali ina nia ya kuwahamisha wawekezaji katika eneo la Mangapwani,

Kamati inaishauri Serikali iharakishe kuwatafutia eneo jengine la kuendeleza

uwekezaji wao kwa lengo la kuunga mkono jitihada za wawekezaji wazalendo.

Aidha, kwa sasa Kamati inaishauri Serikali iwaruhusu wawekezaji hao kuendelea na

shughuli zao mpaka itakapokuwa tayari kulitumia eneo hilo.

2. Kamati inaishauri Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati ya Zanzibar

(ZURA) itafute namna ya kuwasaidia wafanya biashara wa gesi Zanzibar kwa

kufanya mashauriano na Mamlaka ya Udhibiti wa Maji na Nishati ya Tanzania bara

(EWURA) juu ya utaratibu mzuri zaidi wa kibiashara ambao utawadhibiti

wafanyabiashara hiyo katika upangaji wa bei kwa lengo la kuimarisha huduma ya

upatikanaji wa gesi baina ya Zanzibar na Tanzania bara na kuepusha upandaji wa bei

ya gesi kiholela.

3. Kamati inaishauri Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi

kufanya marekebisho ya Kanuni ya Mazao ya Mwaka 2013 ambayo inatokana na

utekelezaji wa kifungu cha 100(1) (f) cha Sheria ya Usimamizi na Uhifadhi wa

Rasilimali za Misitu Nam. 10 ya 1996, ili iendane na thamani halisi ya mazao

(vipando) na kuiwezesha Serikali kutoa fidia ili wananchi waondoke katika sehemu

ya utekelezaji wa mradi.

MRADI WA UJENZI WA BANDARI YA MPIGA DURI

Mradi wa Bandari ya Mpigaduri unatarajiwa kujengwa katika eneo la Maruhubi Mjini

Zanzibar kwa mfumo wa ubia kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Kampuni ya

“China Harbor Engineering Company LTD (CHEC)”. Mradi huo unatarajiwa kugharimu

jumla ya Dola za Kimarekani 231,400,000 kati ya fedha hizo Serikali ya Mapinduzi ya

Zanzibar itatoa jumla ya USD 200,000,000 kupitia mkopo wa Benki ya China – Exim Bank

na Kampuni ya China Harbor Engineering Company Ltd itatoa jumla ya Dola za Kimarekani

31,400,000. Mkataba wa ujenzi huo ulitiwa saini mwaka 2014 kati ya Serikali ya Mapinduzi

ya Zanzibar na Kampuni ya CHEC.

24

CHANGAMOTO ZA MRADI WA UJENZI WA BANDARI YA MPIGA DURI

1. Changamoto kubwa ya mradi huu ni kutokufanyiwa kazi kwa rasimu ya Mkataba

wa fedha (Drafting Finance Agreement) ambayo inapaswa kupitiwa na kupatiwa

maoni na Wizara ya Fedha ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ili Mkataba

halisi uweze kusainiwa. Kamati ilifuatilia suala hili Wizara ya Fedha ya Jamhuri ya

Muungano wa Tanzania kupitia Kamati ya Kitaifa ya uidhinishaji wa Mikopo na

iliarifiwa kuwa, suala hilo bado halijafanyiwa kazi na badala yake Serikali ya

Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) imetakiwa kupeleka tena upembuzi yakinifu

(Feasibility Study) ili mradi upitiwe kwa mara nyengine.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Ili kupata maelezo juu ya changamoto zinazokwamisha upatikanaji wa fedha za Mradi

wa Bandari ya Mpiga Duri, Kamati ilifanya ziara maalum ya kufuatilia suala hili

Wizara ya Fedha na Mipango ya Jamhuri ya Muungano ambapo Kamati ilipata taarifa

tofauti na taarifa ambazo ilizipata Zanzibar kupitia Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na

Usafirishaji. Hivyo, Kamati inaamini kuwa hakuna uwazi katika kutoa taarifa za

baadhi ya miradi ya Serikali.

MRADI WA KIWANDA CHA KUZALISHA MAZIWA FUMBA

Kiwanda kilianza kuzalisha bidhaa ya maziwa mwaka 2014. Uwezo wa kiwanda ni kuzalisha

maziwa lita 180,000 kwa siku, lakini kutokana na changamoto ya soko kiwanda kinazalisha

maziwa wastani wa lita 22,000 mpaka 25,000 kwa siku. Uzalishaji wa kiwanda kwa kiasi

kikubwa unategemea soko la Tanzania Bara kwani kwa upande wa Zanzibar mahitaji ya

maziwa kwa siku kwa mujibu wa takwimu za kiwanda hicho ni chini ya lita 5000.

Kiwanda kina jumla ya wafanyakazi 70 ikijumuisha wataalamu na wafanyakazi wengine wa

kawaida. Kamati ilifanya ziara katika kiwanda hicho ili kujua changamoto zinazokikabili na

kwa lengo la kuishauri Serikali namna bora ya kukisaidia, ili kiweze kuzalisha kwa faida na

kusaidia katika kujenga uchumi wa nchi.

CHANGAMOTO ZA KIWANDA CHA MAZIWA - FUMBA

1. Malighafi ya kutengenezea maziwa inaagizwa kutoka nje ya nchi kutokana na kuwa

maziwa yanayozalishwa Zanzibar hayako katika kiwango na ubora unaohitajika.

25

2. Kiwanda kinategemea soko la Tanzania bara lakini kutokana na kupanda kwa kodi ya

mifugo kupitia “The Animal Disease Act (CAP 156)”, Kiwanda kinalazimika kulipia

kodi ya TZS 2000/= kwa kila kilo moja ya unga wa maziwa unaoingizwa nchini. Kwa

Sheria hiyo Zanzibar inahesabika kama nchi ya kigeni. Hivyo, kiwanda kimeshindwa

kumudu gharama hizo na kulazimika kutoendelea kuzalisha bidhaa tokea Julai, 2018.

3. Wafanyakazi wa kiwanda hawana uhakika na ajira zao kutokana na hali ya kiwanda

kusuwa suwa katika uendeshaji wake. Kiwanda kimesitisha baadhi ya wafanyakazi

wake kuhudhuria kazini tokea mwezi wa Juni 2018, kutokana na changamoto ya

kupanda kwa kodi ya maziwa kwa bidhaa zinazopelekwa Tanzania bara. Licha ya

kuwepo kwa tatizo hilo, kiwanda bado kinaendelea kuwalipa wafanyakazi wake

gharama za mshahara kwa wafanyakazi wote ambao unafikia wastani wa TZS 30

milioni mpaka TZS 40 milioni kwa mwezi.

4. Kutokana na kuwepo kwa kodi ya mifugo inayochangia kuzidisha gharama za

uendeshaji, Kiwanda kimepunguza stahiki za wafanyakazi ikiwemo posho la usafiri,

chakula na malazi.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kwa kuwa soko kubwa la maziwa ya kiwanda cha Fumba lipo Tanzania bara na kwa

sasa soko hilo limeanguka kutokana na kupanda kwa bei ya maziwa kulikochangiwa

na kupandishwa kodi, Kamati inaishauri Serikali kuchukua juhudi ya kuweka sera

ambazo zitalinda bidhaa zinazozalishwa Zanzibar ili kuhimili hali ya ushindani wa

soko.

2. Kutokana na kusita kwa uzalishaji wa kiwanda, Serikali itakosa mapato mengi

yanayotokana na kodi inayolipwa na kiwanda hicho ambayo ni zaidi ya milioni mia

tatu kwa mwaka. Kamati inaishauri Serikali kuleta mipango madhubuti ya kukinusuru

kiwanda ili kiweze kuendelea na uzalishaji.

3. Changamoto za soko kwa wawekezaji wa viwanda Zanzibar ambayo inaathiri

uwekezaji nchini na kuwavunja moyo wawekezaji wapya, kwa kuwa miongoni mwa

vivutio vikubwa vya uwekezaji ni pamoja na soko la uhakika na sheria rafiki kwa

wawekezaji.

26

ZIARA YA KAMATI YA BAJETI TANZANIA BARA

Kamati ilifanya ziara ya kikazi Wizara ya Fedha na Mipango ya Jamhuri ya Muungano wa

Tanzania tarehe 15/11/2018 hadi tarehe 16/11/2018. Katika ziara hiyo, Kamati ilionana na

Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo (National Debt Management Committee) pamoja

na kutembelea Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA). Kamati iliambatana na

baadhi ya Maafisa wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wa Wizara ya Fedha na Mipango

Zanzibar, Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji Zanzibar pamoja na Mamlaka ya

Viwanja vya Ndege Zanzibar.

Lengo la ziara ilikuwa ni kujifunza namna Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo

(National Debt Management Committee) inavyofanya kazi na kupata maelezo juu ya

changamoto zinazokwamisha upatikanaji wa fedha za mikopo kwa ajili ya Miradi ya

Zanzibar ambayo fedha zake zina dhamana ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa

Tanzania .

Kamati pia ilijifunza mfumo wa uendeshaji na mgawanyo wa Mapato ya Mamlaka ya

Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) pamoja na kukagua Mradi wa ujenzi wa Uwanja wa

Ndege “Terminal III”, kuona namna Mamlaka hiyo ilivyofanikiwa katika usimamizi na

uendeshaji wa Mradi huo, hasa ikizingatiwa kwamba Mradi kama huo unatekelezwa Zanzibar

na ambao unakabiliwa na changamoto za ujenzi na upatikanaji wa fedha.

KAMATI YA KITAIFA YA UIDHINISHAJI MIKOPO

Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo imeundwa kwa Mujibu wa Sheria ya Mikopo,

Dhamana na Ruzuku za Serikali ya mwaka 1974. Ambapo Wajumbe wake ni pamoja na:-

1. Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango SMT Mwenyekiti

2. Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango SMZ Mjumbe

3. Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu SMT Mjumbe

4. Katibu Mkuu Afisi ya Makamo wa Rais SMT Mjumbe

5. Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje SMT Mjumbe

6. Katibu Mtendaji Tume ya Mipango SMT Mjumbe

7. Katibu Mtendaji Tume ya Mipango SMZ Mjumbe

8. Mwanasheria Mkuu SMT Mjumbe

9. Mwanasheria Mkuu SMZ Mjumbe

27

10. Gavana Benki Kuu Tanzania Mjumbe

11. Mhasibu Mkuu SMT Mjumbe

12. Mhasibu Mkuu SMZ Mjumbe

13. Mtendaji Mkuu wa Benki ya Maendeleo Tanzania Mjumbe

(TIB- Development Bank)

Mbali na Kamati hiyo pia kuna Watendaji “Secretariat” wa Kamati ya Wataalamu (Technical

Debt Managemenet Committee - TDMC) ambayo hufanya uchambuzi wa awali, kabla

kuwasilisha uchambuzi wao kwa Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo. Kamati ya

Wataalamu inaongozwa na Kamishna wa Sera na Madeni ambae ndie Mwenyekiti.

MAMBO YALIYOBAINIKA KATIKA KIKAO NA KAMATI YA KITAIFA YA

UIDHINISHAJI MIKOPO

1. Kamati iliarifiwa kwamba Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Zanzibar

mara nyingi huwa hahudhurii vikao vya Kamati hiyo yeye mwenyewe na mara nyingi

huwakilishwa na watendaji wengine.

2. Kwa mujibu wa Sheria iliyoanzisha Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo,

Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango wa Jamhuri ya Muungano hawezi

kuwakilishwa na mtu mwengine, hivyo asipokuwepo kikao hakiwezi kufanyika.

3. Kamati hufanya vikao vinne vya kawaida kwa mwaka, hata hivyo kwa mwaka

2017/2018 imefanya zaidi ya vikao 14 vya dharura.

4. Jukumu la msingi la Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo ni kumshauri Waziri

wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu kuukubali au kuukataa

mkopo na kusimamia utekelezaji wa mikakati ya mikopo iliyoidhinishwa.

5. Miongoni mwa sababu zinazochelewesha kupatikana kwa fedha za mikopo ya miradi

ni mchakato wa kina unaofanywa na Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo ili

kujiridhisha kwa kupata taarifa sahihi za wakopeshaji, masharti ya mkopo na ubora

wa mkopo husika.

6. Sababu zilizopelekea kuchelewa kwa fedha za Mkopo wa Mradi wa jengo la Abiria la

Uwanja wa Ndege Zanzibar ni Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo kutokubali

masharti ya kuchanganya mkataba wa mkopo na madai ya Kiwanda cha Urafiki

pamoja na kuwekwa dhamana ya mkopo kwa baadhi ya mali za Serikali. Hata hivyo,

28

Kamati ya Bajeti iliarifiwa kwamba Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya

Muungano wa Tanzania ameshatowa maoni yake kuhusu kuondolewa kwa vipengele

hivyo na tayari Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeshawaandikia

wakopeshaji.

7. Kwa upande wa Mradi wa Barabara ya Wete-Chake Chake sababu za msingi

zilizokwamisha ni Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo kutokubaliana na

masharti ya Mkataba wa Mkopo huo ambayo yanahusiana na uwekaji dhamana wa

mali za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Licha ya Serikali kutoridhika

na masharti,wakopeshaji hawajakubali kuyaondosha masharti hayo. Kwa sasa Serikali

ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania inajaribu kutumia njia mbadala za kidiplomasia

(Diplomacy negotiations) ili kufikia muwafaka wa jambo hilo.

8. Kuhusu Mradi wa Bandari ya Mpiga Duri, licha ya kuwa Mradi huo ni wa siku

nyingi, bado upo katika hatua za awali, kwani Kamati ya Bajeti imearifiwa kuwa

Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo ndio kwanza imeomba kupatiwa nyaraka

za Upembuzi yakinifu (Feasibility study) wa Mradi huo ili upitiwe tena upya, hali

ambayo inaweza kupelekea mradi huo kuchukua muda mrefu zaidi.

MAMLAKA YA VIWANJA VYA NDEGE TANZANIA

Mradi wa Ujenzi wa Jengo la Tatu la Abiria (TB III) ni mwendelezo wa upanuzi wa

Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) ambacho kilianzishwa

mwaka 1956. Mradi wa upanuzi ulianza mwaka 2013 ambapo hadi sasa umefikia asilimia

85 na unatarajiwa kukamilika mwezi Mei, 2019.

MAMBO YALIYOBAINIKA WAKATI WA ZIARA YA MAMLAKA YA VIWANJA

VYA NDEGE

1. Pamoja na ukweli kwamba Mradi wa uwanja wa ndege wa Tanzania Bara ni mkubwa

na umeanza mwisho ukilinganishwa na mradi kama huo kwa upande wa Zanzibar,

mradi huo uko katika hatua nzuri na unatarajiwa kukamilika hivi karibuni.

2. Sehemu ya Mapato ya Mamlaka ya Uwanja wa Ndege inayotokana na kodi ya Abiria

(Passengers Services Charge) inarejeshwa Mamlaka, tofauti na ilivyo kwa Mamlaka

ya Uwanja wa Ndege Zanzibar ambapo mapato hayo yote yanakwenda Serikalini.

29

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kamati ya Bajeti haikuridhishwa na Kitendo cha Katibu Mkuu Wizara ya

Fedha na Mipango Zanzibar, kutohudhuria mara kwa mara vikao vya Kamati

ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo (National Debt Management Committee),

hasa kwa kuzingatia uzito wa vikao hivyo na nafasi yake katika Serikali ya

Mapinduzi ya Zanzibar.

2. Kamati ya Bajeti imeshagazwa na taarifa kwamba wapo Wajumbe wa

Zanzibar wanaoshiriki vikao katika Kamati ya Kitaifa ya Uidhinishaji Mikopo,

ambao walipaswa kujua changamoto zinazokwamisha uidhinishwaji wa Fedha

za mikopo za miradi ya Zanzibar, ingawaje Kamati imekuwa inakosa taarifa

hizo kila mara wakati inapohoji sababu zinazopelekea kukwama kwa mikopo

ya Miradi hiyo.

3. Kamati ya Bajeti haijaridhishwa na hatua zinazochukuliwa na Serikali ya

Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu ufuatiliaji wa fedha za Mradi wa Bandari ya

Mpiga Duri, kutokana na kuarifiwa kwamba, Kamati ya Kitaifa ya

Uidhinishaji Mikopo ipo katika hatua ya kupitia upya upembuzi yakinifu wa

Mradi huo, licha ya taarifa ya Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji

Zanzibar kuonesha kuwa hatua za awali za mradi huo zimeshakamilika.

SHIRIKA LA BIMA LA ZANZIBAR

Shirika la Bima la Zanzibar ni miongoni mwa mashirika yanayomilikiwa na Serikali ya

Mapinduzi ya Zanzibar kwa asilimia100. Shirika lilianzishwa mwaka 1969 na linafanya kazi

chini ya Sheria ya Mitaji ya Umma Namb. 4 ya 2002. Malengo Makuu ya Shirika la Bima la

Zanzibar ni pamoja na kutoa huduma zote kwa wananchi na kuwekeza katika miradi mbali

mbali.

Kamati katika kutekeleza majukumu yake ilifanya ziara Afisi za Shirika la Bima na kupokea

taarifa ya Shirika hilo kuhusu mafanikio na changamoto tokea kuanzishwa kwake pamoja na

mchango wake katika Bajeti ya Serikali. Aidha, Kamati ilitaka kujua mkakati unaotumiwa na

Shirika hilo katika kukabiliana na ushindani wa soko la Bima. Kamati iliarifiwa kuwa,

miongoni mwa mafanikio ya msingi ya Shirika hilo ni pamoja na kulipa gawio Serikalini kwa

mujibu wa viwango ambavyo Shirika linapangiwa, kuongeza mtandao wa Afisi zake

30

Zanzibar na Tanzania bara, kuekeza katika benki ambazo zina viwango vizuri vya riba,

kukodisha majengo yake, kulipa madai halali na kwa haraka na kujenga imani kwa wateja.

Huduma zinazotolewa na Shirika la Bima la Zanzibar

Miongoni mwa huduma zinazotolewa na Shirika la Bima la Zanzibar ni pamoja na bima ya

magari, bima ya moto, bima ya ajali, bima ya wizi, bima kwa ajili ya wataalamu

(Professional Indemnity), bima ya vyombo vya usafiri wa anga na majini (Marine and

Aviation) pamoja na kukinga madhara yanayosababishwa na matumizi ya bidhaa au

matumizi ya huduma (Public liability)

Uwekezaji wa Shirika la Bima

Shirika limeendelea kufanya uwekezaji katika maeneo mbali mbali ikiwemo uwekezaji wa

fedha katika mabenki (Fixed deposit) pamoja na uwekezaji katika ofisi zake ambazo

zimekodishwa kwa watu mbali mbali. Aidha, baadhi ya fedha za Shirika huwekezwa katika

huduma za hawala za Serikali (Treasury bill) za Benki Kuu kupitia minada ya kila wiki.

CHANGAMOTO ZA SHIRIKA LA BIMA

1. Kuongezeka kwa ushindani wa biashara ya bima ambapo makampuni binafsi

yanatumia mbinu mbali mbali katika kukuza biashara, ikiwemo mbinu za kurahisisha

kufanya malipo ya fidia kwa haraka zaidi ikilinganishwa na kampuni ya Serikali

ambazo hufanya malipo baada ya uchunguzi wa kina ambao huchukua muda.

2. Kuongezeka kwa ajali za magari kunakopelekea Shirika kulipa madai mengi na

makubwa

3. Ukosefu wa umiliki wa majengo ya ofisi zote yanayotumiwa na Shirika la Bima

Tanzania bara ambapo Shirika hulazimika kutumia fedha nyingi kwa ajili ya kodi

ambazo zinaongezeka mwaka hadi mwaka.

4. Shirika linashindwa kuongeza maslahi ya wafanyakazi wake kutokana na kulazimika

kufuata muongozo wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wa viwango vya maslahi ya

watumishi. Licha ya kuwa Shirika linatoa huduma Tanzania nzima na pia lina ofisi

Tanzania bara, ambapo linakabiliwa na mazingira ya ushindani wa biashara kutoka

katika makampuni mengine, viwango vya mishahara ya Shirika hili ni vidogo

ikilinganishwa na mashirika mengine binafsi, jambo ambalo linapunguza ari kwa

watendaji na baadhi yao kufikiria kulihama Shirika.

31

5. Shirika linaongozwa na Sheria ya Utumishi wa Umma ya Zanzibar Sheria Nam. 2 ya

2011 ambapo kutokana na masharti yaliyomo kwenye sheria hiyo, kipaumbele cha

ajira kimewekwa kwa Wazanzibari. Hivyo inakuwa kikwazo kwa Shirika kufanya

uajiri wa kudumu wa wafanyakazi kwa upande wa Tanzania Bara ambapo Shirika

mara nyingi limekuwa likifanya uajiri wa muda.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kutokana na changamoto ya ushindani wa soko inayolikabili Shirika la Bima la

Zanzibar, Kamati inaishauri Serikali iweke mazingatio maalum katika muongozo

unaotolewa wa viwango vya mishahara kwa Taasisi za Serikali, kwa kuruhusu

kuongeza viwango vya maslahi ya wafanyakazi wa Shirika la Bima pamoja na

mashirika mengine ambayo yanatowa huduma kwa Tanzania nzima, ili mashirika

hayo yaweze kuhimili ushindani wa soko la ajira na kuhamasisha wafanyakazi wa

Shirika kufanya kazi kwa ari na ufanisi zaidi.

2. Kwa kuwa Sheria ya Utumishi wa Umma Nam. 2 ya 2011, imeweka kipaumbele

katika ajira kwa Wazanzibari, Kamati inaishauri Serikali kuifanyia mapitio na kuweka

mazingatio maalum ya uajiri kwa Mashirika ya Serikali yanayotoa huduma Tanzania

bara na kuyawezesha kuajiri wataalamu hususani kwa upande wa Tanzania bara

ambao watalisaidia Shirika katika kuendelea kutoa huduma bora.

3. Kamati imeridhishwa na mafanikio yaliyopatikana na Shirika la Bima la Zanzibar,

kutokana na Shirika hilo kujiendesha kwa faida na kuchangia vizuri gawio la Serikali

(dividend). Pamoja na mafanikio hayo, Kamati inalishauri Shirika kuendelea kuweka

mikakati imara zaidi itakayoliwezesha Shirika kukabiliana na ushindani wa soko

hususani upande wa Tanzania Bara ambako kuna kampuni nyingi zinazotoa huduma

za Bima.

4. Kamati inalishauri Shirika la Bima la Zanzibar kuendelea kutoa elimu kwa wananchi

juu ya taratibu na Sheria za Bima ili kuepusha migogoro na kukosa imani kwa

wananchi hao kutokana na kukosa elimu ya taratibu hizo, hususani pale mteja

anapokosa fidia ya madai yake kama alivyotarajia.

5. Kamati inaitaka Serikali ilitumie Shirika la Bima la Zanzibar, kwa kuhakikisha

inayakatia bima majengo ya Serikali pamoja na miradi yake yote. Aidha, katika

32

kutanua wigo wa soko, Kamati inalishauri Shirika kuzihamasisha Taasisi za Serikali

kutumia huduma za Shirika hilo.

6. Kamati inaishauri Serikali katika mikataba ya miradi ya ujenzi itakayoingia izingatie

kuweka kipengele cha Bima (Insurance Clause), ili kupata fidia endapo litatokea

tatizo katika utekezaji wa miradi hiyo.

SHIRIKA LA UMEME ZANZIBAR (ZECO)

Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) limeanzishwa kwa Sheria Nam. 3 ya mwaka 2006 na

linamilikiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) chini ya usimamizi wa Wizara ya

Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati. Shirika lina jumla ya wafanyakazi 758, kati ya wafanyakazi

hao, 582 kutoka Unguja na 176 kwa upande wa Pemba. Shirika katika utendaji wake wa kazi

linasimamiwa na Meneja Mkuu chini ya maelekezo ya Bodi ya Wakurugenzi.

Kazi kuu za Shirika ni kuzalisha na kusafirisha umeme, kusambaza na kuuza umeme katika

visiwa vya Unguja na Pemba. Katika kutekeleza kazi ya usambazaji umeme, Shirika

limeweza kusambaza huduma ya umeme vijiji 2,694 vya Unguja na Pemba sawa na asilimia

83 ya vijiji vya Zanzibar.

CHANGAMOTO ZA SHIRIKA LA UMEME LA ZANZIBAR (ZECO)

1. Ongezeko la madeni kwa Taasisi za Serikali ambapo Shirika linazidai Taasisi za

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar jumla ya TZS 26.556 Bilioni na TZS 2.219 bilioni

kwa Taasisi za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ongezeko la madeni

hayo, linaathiri sana mapato na gharama za uendeshaji wa Shirika.

2. Shirika linakabiliwa na deni linalodaiwa na TANESCO ambapo Shirika linaendelea

kufanya malipo ya deni hilo lililotokana na malimbikizo ya Ankara za ununuzi wa

umeme kutoka TANESCO.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kwa kuwa ongezeko la madeni kwa Shirika la Umeme la Zanzibar (ZECO) linaathiri

sana mapato na hata uendeshaji wa Shirika hilo, Kamati katika kukabiliana na hali hii

na kwa kuwa changamoto hii ni ya muda mrefu inalishauri Shirika kutoendelea

kuwapatia huduma ya umeme taasisi ambazo ni wadaiwa sugu.

2. Kutokana na Shirika kukabiliwa na deni la TANESCO, Kamati inalishauri Shirika

kuendelea na juhudi zake za kupunguza upotevu wa umeme na kuhakikisha kuwa

33

wateja wote wanaotumia umeme wanalipia huduma hiyo ili kukuza mapato ya

Shirika.

MFUKO WA HIFADHI YA JAMII ZANZIBAR -ZSSF

Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) umeanzishwa chini ya Sheria Nam. 2 ya 1998

ambayo ilifanyiwa mapitio makubwa na kutungwa upya Sheria Nam. 2 ya 2005. Aidha,

Sheria hiyo ilifanyiwa marekebisho katika Sheria Nam. 10 ya 2016.

ZSSF imekuwa na mafanikio katika kuongeza wigo wa wanachama na uwekezaji wa vitega

uchumi kama vile Dhamana za Serikali (SMZ Stock), Hati fungani (Treasury Bond), Hati

fungani PBZ (Corporate Bond), Hisa (Shares), Mabenki (Fixed Deposits), Majengo

(Investment Properties) na Mikopo (Institutional Loans).

CHANGAMOTO ZA MFUKO WA HIFADHI YA JAMII ZANZIBAR - ZSSF

1. Kutofautiana kwa taarifa za wanachama wakati wa kujisajili katika Mfuko na zile

zinazokuwepo katika Idara za Utumishi za taasisi husika zilizowaajiri wanachama

hao. Hali hii huleta ugumu katika kupiga hesabu ya kiasi cha mafao kinachostahiki

kulipwa kwa mwanachama.

2. Kutojisajili wanachama wapya katika Mfuko kwa baadhi ya Taasisi zenye makao

makuu yake Tanzania bara. Taasisi zinazoajiri Zanzibar zinapaswa kuwasajili

wafanyakazi wake Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar.

3. Ugumu wa kuwasajili wafanyabiashara wadogo wadogo ambao wengi wao wapo

katika sekta isiyo rasmi.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kamati inaishauri Mfuko wa Hifadhi wa Jamii Zanzibar (ZSSF) ishirikiane na taasisi

ambazo ni waajiri wa wanachama wa Mfuko kwa ajili ya kuchunguza taarifa zao na

kuzifanyia marekebisho ili kuondoa mkanganyiko wakati mwanachama anapostaafu.

2. Kamati inaushauri Mfuko uzingatie uwekezaji wa miradi ya ujenzi wa nyumba za

gharama nafuu kwa ajili ya wanachama wake, badala ya kuangalia uwekezaji wa

kibiashara pekee.

34

3. Kamati inaishauri Mfuko kutanua wigo wa uwekezaji kwa kujenga majengo na

miundombinu ambayo itatoa huduma za moja kwa moja kwa jamii kama vile vyoo

vya umma (public toilets), masoko ya samaki na mboga mboga

4. Kamati inaishauri Serikali kuitafutia ufumbuzi wa haraka changamoto ya

wafanyakazi wa Taasisi zenye Makao makuu yake Tanzania Bara zinazoajiri

Zanzibar ili wafanyakazi wote waliojariwa Zanzibar wasajiliwe katika Mfuko wa

Hifadhi ya Jamii Zanzibar kama ilivyo kwa baadhi ya mashirika.

5. Kamati inaishauri Serikali kutengeneza kanzi data (data base) ya wafanyabiashara

wadogo wadogo ili kurahisisha upatikanaji wa mapato ya Serikali na kutanua wigo wa

wanachama wapya kwa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF).

KIKAO CHA PAMOJA BAINA YA KAMATI YA BAJETI NA

WAFANYABIASHARA

Kamati ya Bajeti kutokana na umuhimu wa sekta ya biashara ilifanya majadiliano na

walipa kodi wakubwa (Strategic Tax Payer) kwa upande wa Zanzibar kwa lengo la kuona

namna wawekezaji hao wanaweza kuimarishiwa mazingira ya kufanya shughuli zao na

kuongeza mapato ya Serikali. Kwa lengo la kuhakikisha Kamati inagusa biashara mbali

mbali, ilikutana na wawakilishi wa kamapuni ya ndege Ethiopian Airline, Oman Air,

kampuni ya ujenzi ya Salem Construction, kampuni ya mawasiliano ya Zantel na ZAT.

Katika kikao hicho, Kamati ilizialika baadhi ya taasisi za Serikali zinazohusika na

masuala ya usimamizi na ukusanyaji wa kodi, ikiwemo Wizara ya Fedha na Mipango

Zanzibar, Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

MAMBO YALIYOJITOKEZA KATIKA KIKAO

1. Imebainika kuwa baadhi ya wafanyabishara hususani wafanyabishara wa

kampuni za ujenzi, wanaathirika kutokana na changamoto ya usafirishaji na

ushushaji mizigo, ambapo inachukua takribani mwezi mmoja na nusu kutoa

mzigo kutoka Mombasa hadi kushushwa katika Bandari ya Malindi -

Zanzibar. Hali hii kwa kiasi kikubwa inachangiwa na uwezo mdogo wa

Bandari kutokana na miundombinu hafifu ikiwemo changamoto ya kuharibika

kwa winch (crane) iliyokuwa ikitumika kwa kushushia mizigo.

35

2. Wafanyabishara wa Zanzibar wameendelea kulalamikia changamoto ya kulipa

kodi ya Ongezeko la thamani (VAT) mara mbili, ambapo wengi wa

wafanyabiashara hao hawawezi kununua bidhaa viwandani, hali hiyo

inaendelea kuathiri mazingira ya biashara – Zanzibar.

3. Wafanyabishara wa Zanzibar wanalazimika kukata vibali vya Shirika la

Viwango Tanzania (TBS) na Wakala wa Chakula, Dawa na Vipodozi

Tanzania (TFDA) vinavyotolewa na Mamlaka za Tanzania licha ya kuwa

vibali kama hivyo wameshapatiwa Zanzibar kupitia Mamlaka kama hizo

zilizopo Zanzibar yaani ZBS na ZFDA. Kamati iliarifiwa kwamba Serikali ya

Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ziliingia makubaliao

(MOU) kuhusu kuondosha vikwazo hivyo kwa kukubali vibali vinavyotolewa

na mamlaka za pande zote mbili, lakini utekelezaji wake umekuwa tofauti

kwani wafanyabiashara wa Zanzibar wanatakiwa kukata vibali hivyo tena

pindi wanapopeleka mizigo Tanzania bara.

4. Kwa upande wa wafanyabishara wa makampuni ya mashirika ya ndege,

Kamati iliarifiwa kuwa mashirika makubwa ya ndege yanalazimika kulipa

faini iwapo yatapindukia siku kumi na tano za mwezi kabla ya kulipa kodi

(safety and departure fee), jambo ambalo kwa mashirika ya kimataifa ambayo

kwa kawaida yanakuwa na vituo (destinations) vingi hulazimka kupitia hatua

nyingi mpaka kukamilika uidhinishaji malipo, hivyo muda uliowekwa wa siku

15 kutozwa faini iwapo malipo yatacheleweshwa ni mdogo sana hususani

kwa mashirika yanayotoa huduma Zanzibar ambapo makampuni hayo

yanalazimika kuripoti Afisi kuu ya Shirika - Dar es Salam na baadae makao

makuu ya Shirika .

5. Kamati imebaini kuna mvutano wa ukusanyaji kodi ya ongezeko la thamani

(VAT) baina ya Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya Mapato

Tanzania (TRA) kwa makampuni yanayotoa huduma za mawasiliano ya simu

Zanzibar na Tanzania bara, mvutano huo unatokana na maelekezo

yanayokinzana yanayotolewa na mamlaka hizo mbili juu ya mgawanyo halisi

wa kodi unaopaswa kulipwa na walipa kodi kwa Mamlaka hizo mbili, hali hii

inaathiri Makampuni ambayo ndio walipa kodi.

36

6. Kutokupewa kipaumbele kwa makampuni ya ndani wakati wa uendeshaji wa

zabuni za ujenzi za miradi ya Serikali, ambapo mara nyingi inaonekana ni

makampuni ya Kigeni yanayoshinda zabuni hizo na kuyaacha makampuni ya

wazawa yakiwa hayana kazi.

MAONI NA USHARI WA KAMATI

1. Kamati inaishauri Serikali kupitia Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya

Mapato Tanzania (TRA) kuongeza ushirikiano na wafanyabishara ikiwa ni pamoja na

kuandaa vikao vya mara kwa mara vya kusikiliza changamoto na maoni yao. Aidha,

kuwe na utaratibu wa kuwapatia elimu walipa kodi kuhusu mifumo ya kodi iliyopo

Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

2. Kamati inaishauri Serikali kupitia Bodi ya Mapato (ZRB) kukaaa pamoja na

Makampuni ya Ndege, kusilikiliza malalamiko yao kuhusu muda wa kulipia kodi

(Safety fee na Depature fee) na kuangalia uwezekano wa kuwaongezea muda wa

kulipia kodi hiyo ndani ya siku 30 badala ya siku 15 kama ilivyo sasa. Hatua hiyo

itasaidia kujenga uhusiano mzuri baina ya walipa kodi na mamlaka zinazosimamia

kodi na pia itasaidia kuhamasisha ulipaji kodi kwa hiari.

3. Ili kuvisaidia viwanda vya Zanzibar kutokana na changamoto ya mazingira magumu

ya soko na gharama kubwa za uzalishaji, Kamati inaishauri Serikali iweke sera ya

kuvilinda viwanda vya Zanzibar, kwani katika mfumo wa uchumi wa kiushindani

duniani, nchi nyingi zikiwemo nchi zilizoendelea zinatekeleza sera za kulinda

viwanda vyao vya ndani.

4. Ipo haja kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi

ya Zanzibar kukaa pamoja na kuzitatua changamoto zaa vikwazo vya kibiashara na

kodi ambavyo vinaathiri wafanyabiashara wa pande hizo mbili hususani

wafanyabiashara wa Zanzibar, ambako kuna soko dogo kutokana na idadi ndogo ya

watu wake. Hivyo, si busara kwa wafanyabiashara wa pande hizi mbili kuendelea

kulilia changamoto hizi ambazo zimekuwa za siku nyingi. Nchi nyingi duniani

zimekuwa zikianzisha mashirikiano ya kikanda (Regional Integration) ambayo

malengo yake makubwa ni kurahisisha biashara na uchumi wao. Hivyo ni vyema kwa

Serikali zetu mbili zikaondosha changamoto hizo na kuwa na Muungano imara

kiuchumi kama ambavyo Muungano huo umeimarika kisiasa.

37

5. Kamati inaishauri Serikali kuikarabati kwa haraka winch (crane) inayotumika

kupakua na kupakia makontena bandarini, ili winch (crane) hiyo ianze kufanya kazi

na kupunguza msongamano katika bandari ya Zanzibar.

6. Kamati inaishauri Serikali kuzipa kipaumbele kampuni za ndani hususani za wazawa

ambazo zinashiriki katika zabuni za miradi ya Serikali zenye uwezo unaofanana au

unaokaribiana na kampuni za nje kwa lengo la kuziendeleza kampuni hizo na

kuwahamasisha wawekezaji wa ndani.

KIKAO CHA PAMOJA BAINA YA KAMATI NA WAWEKEZAJI WA SEKTA YA

UTALII NA MAHOTELI

Kamati katika kuhakikisha inafanyia kazi maeneo yote yenye mchango mkubwa katika

uchumi wa Zanzibar ilifanya kikao cha pamoja na wawekezaji katika sekta ya utalii na

mahoteli kwa lengo la kujadili namna bora ya kuweka mazingira mazuri na kuhakikisha

makusanyo ya kodi za Serikali yanaongezeka. Miongoni mwa wawekezaji waliohudhuria

katika kikao ni pamoja na wawakilishi wa wawekezaji kutoka Hotel ya Park Hyatt,

Kiwengwa Strand Hotel, The Residence, Double Tree By Hilton, Nungwi Village na Nungwi

Royal Zanzibar pamoja na Taasisi mbali mbali za Serikali zinazohusiana na Sekta ya utalii.

Kwa upande wa Taasisi za Serikali zilizoshiriki katika kikao hicho ni pamoja na Bodi ya

Mapato Zanzibar (ZRB), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Wizara ya Biashara na

Viwanda na Wizara ya Fedha na Mipango.

MAMBO YALIYOJITOKEZA KATIKA KIKAO

1. Ukosefu wa barabara za lami zinazoelekea maeneo ya uwekezaji kwa baadhi ya

mahoteli yaliyopo kando kondo ya fukwe za bahari, hali inayopunguza hamasa ya

wageni kufika katika maeneo hayo.

2. Wingi wa kodi na tozo zinazotozwa na Serikali Kuu na Serikali za Wilaya hali

inayopelekea wawekezaji wa sekta ya utalii kupoteza muda mwingi katika kufuatilia

malipo ya kodi na tozo hizo.

3. Serikali kutowashirikisha kikamilifu wawekezaji katika uanzishwaji wa aina mpya ya

kodi na tozo mbali mbali zinazohusina na mahoteli na huduma nyengine zinazotolewa

na hoteli.

38

4. Ukusanyaji wa kodi na tozo nje ya muda wa saa za kazi hali ambayo inawafanya

wageni kukosa utulivu kutokana na mivutano baina ya walinzi wa mahoteli na

wasimamizi wa kodi.

5. Kuwepo kwa nyumba binafsi za makaazi zinazomilikiwa na wananchi kando kondo

ya mahoteli ambazo hukodishwa kwa wageni bila ya kufuata utaratibu na kutolipiwa

kodi yoyote, hali ambayo inaikosesha Serikali mapato na kuhatarisha usalama wa

wageni wanaokodishwa katika nyumba hizo.

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

1. Kamati inaishauri Serikali ihakikishe inazifanyia matengenezo barabara za ndani kwa

kuweka mazingatio maalum kwenye maeneo ya uwezekaji yenye hoteli na

yasiyofikiki kwa urahisi.

2. Kutokana na kuwepo kwa utitiri wa kodi na tozo katika sekta ya utalii na kwa lengo la

kuufanya mfumo wa kodi kuwa rafiki zaidi, Kamati inaishauri Serikali kuanzisha

mfumo wa kodi jumuishi (centralized) ambao utamuwezesha mlipa kodi kulipa kodi

mara moja kwa maeneo yote anayopaswa kulipia.

3. Kamati inaisisitiza Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) kufuata utaratibu na maadili ya

kazi katika utekelezaji wa majukumu yake, kwa lengo la kutowakwaza wawekezaji

wa hoteli kwa kuwagongea wageni wkati wa usiku wanapokuwa wamepumzika, na

badala yake kutafuta utaratibu mbadala utakaowawezesha kujiridhisha juu ya idadi

halisi ya wageni.

4. Kamati inaishauri Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) kuwachukulia hatua wananchi

wanaokodisha nyumba kwa wageni bila ya kufuata utaratibu, kwa lengo la kuwalinda

wawekezaji wa sekta ya utalii na kukusanya mapato ya Serikali yanayokosekana

katika eneo hilo.

KIKAO CHA PAMOJA BAINA YA KAMATI NA WAWEKEZAJI WA VIWANDA

VYA VINYWAJI VISIVYO NA KILEVI

Kamati ya Bajeti ilifanya kikao cha pamoja na wawekezaji wa viwanda vya vinywaji visivyo

na kilevi Zanzibar, kwa lengo la kusikiliza changamoto zao ikiwemo ugumu wa utekelezaji

wa Sheria ya Ushuru wa Bidhaa (Excise Duty).

39

Itakumbukwa kwamba, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Bajeti ya

2012/2013 iliamua kuongeza mapato ya Ushuru wa Bidhaa zinazozalishwa nchini kwa

kuongeza Ushuru wa Bidhaa katika vinywaji visivyo na kilevi. Kwa upande mwengine,

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanzisha Ushuru wa Bidhaa kama huo kwa vinywaji

visivyo na kilevi. Kwa mujibu wa Sheria ya Fedha ya mwaka 2016, kiwango cha Ushuru wa

Bidhaa (Excise Duty) ya “soft drinks” na maji ni TZS 58.0 kwa lita moja na kwa juisi ni TSH

9.5 kwa kila lita.

MAMBO YALIYOBAINIKA KATIKA KIKAO CHA PAMOJA BAINA YA KAMATI

NA WAWEKEZAJI WA VIWANDA VYA VINYWAJI VISIVYO NA KILEVI

1. Iwapo kiwango cha Ushuru wa Bidhaa kinachotajwa katika Sheria kitatekelezwa

kama kilivyo, gharama za uendeshaji wa viwanda Zanzibar zitaongezeka kwa

kiwango kikubwa. Aidha, kwa upande wa Zanzibar mzigo (burden) utakuwa mkubwa

zaidi ikilinganishwa na Tanzania bara ambako viwanda vyake vinanufaika na

uzalishaji mkubwa (Economies of Scale). Mfano kiwanda cha Coca cola, Pepsi, Azam

nk. Katika mazingira hayo, bidhaa zinazozalishwa Zanzibar hazitaweza kuhimili

ushindani katika masoko.

2. Viwanda vya Zanzibar ni vidogo na mali ghafi za bidhaa zinazozalishwa zinatoka nje

ya Zanzibar. Aidha, wataalamu katika sekta ya viwanda ni wachache, hali

inayopelekea viwanda vya Zanzibar kutopata faida kubwa ukilinganisha na viwanda

vikubwa vya Tanzania bara.

3. Kwa mujibu wa Ibara ya 4 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya

mwaka 1977 ambayo imeyataja Mambo ya Muungano, katika kifungu cha 10 (10th

item) jadweli la kwanza imeitaja TRA kuwa ndio taasisi pekee yenye mamlaka ya

kusimamia mapato yatokanayo na Ushuru wa Bidhaa Tanzania ikiwemo Zanzibar.

4. Kumekuwepo na uchereweshaji wa uingizaji wa bidhaa kutoka Zanzibar kwenda

Tanzania bara, kwa madai ya kukosa vibali vya Shirika la Viwango Tanzania (TBS)

na Wakala wa Chakula, Dawa na Vipodozi Tanzania (TFDA), licha ya kwamba

wamepata vibali vya Shirika la Viwango Zanzibar (ZBS) na Wakala wa Chakula,

Dawa na Vipodozi Zanzibar (ZFDA).

40

MAONI NA USHAURI WA KAMATI

Kwa lengo la kutekeleza Sera ya Viwanda kwa upande wa Zanzibar na kuvilinda viwanda

vya ndani, Kamati inaishauri Serikali kufanya mambo yafuatayo:

1. Kutoa msamaha maalum wa ushuru wa bidhaa kwa wazalishaji wa vinywaji visivyo

na kilevi au kutoza kiwango kidogo ambacho hakitaathiri uzalishaji wa bidhaa hizo

viwandani.

2. Kamati inaishauri Serikali, kuipa kipaumbele (upendeleo maalum) sekta ya viwanda

kutokana na umuhimu wake kwa uchumi wa Zanzibar. Endapo viwanda vitapunguza

au kusitisha uzalishaji kutapelekea kuathiri hali ya uchumi na fedha ikiwemo kupanda

kwa bei za bidhaa, kupungua kwa kiwango cha uzalishaji na mauzo, kukosekana kwa

ajira na hatimae kupungua pato la nchi.

3. Kamati inaishauri Serikali kuweka mipango madhubuti ya kuwasomesha vijana wetu

fani zinazohusiana na sekta ya viwanda ili Zanzibar iwe na wataalamu wa kutosha

katika sekta hiyo.

4. Kwa vile kuna makubaliano (MOU) baina ya ZBS na TBS na baina ya ZFDA na

TFDA wa kufanya kazi kwa pamoja. Kamati inaishauri Serikali kulifuatilia jambo hili

ili utekelezaji wa makubaliano hayo uanze mara moja. Hii itasaidia kuwapunguzia

gharama za ziada wafanyabiashara wa Zanzibar kuepuka faini za kuchelewesha kutoa

bidhaa zao bandarini Dar es Salaam kwa kuanza upya utaratibu wa kuomba vibali vya

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Wakala wa Chakula, Dawa na Vipodozi

Tanzania (TFDA) wakati tayari wameshapata vibali vya Shirika la Viwango Zanzibar

(ZBS) na Wakala wa Chakula, Dawa na Vipodozi Zanzibar (ZFDA).

41

SEHEMU YA TATU

HITIMISHO

Kamati inapenda kutoa shukurani za dhati kwa taasisi zote za Serikali na binafsi

zilizoshirikiana kwa muda wote wakati Kamati ikitekeleza majukumu yake. Aidha,

Kamati inawashukuru wadau wote walioalikwa na kufika mbele ya Kamati, kwani

michango na maoni yao imekuwa ni msaada muhimu katika kutekeleza majukumu ya

Kamati ya kuisimamia na kuishauri Serikali. Kamati inategemea Serikali itaifanyia kazi

taarifa hii na kuleta majibu muafaka juu ya utekelezaji wa maagizo ya Kamati.